Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Je, Kuwasiliana na Pepo Kuna Madhara?

Je, Kuwasiliana na Pepo Kuna Madhara?

 Una maoni gani?

  •   Je, mtu anaweza kupata madhara yoyote kwa kuchunguza nyota, kuwaendea wabashiri, au kutumia vitu vinavyohusiana na uaguzi?

  •   Je, hadithi kuhusu kuwasiliana na roho ni za kubuniwa tu​—eti kuna ushindani kati ya wema na ubaya​—au je, ni mambo halisi na hatari?

 Makala hii itachunguza kwa nini kuwasiliana na pepo kunaweza kuvutia na kwa nini tunapaswa kujihadhari.

 Kwa nini kunavutia?

 Watu wanaotayarisha sinema, vipindi vya televisheni, michezo ya video, na vitabu wamepata pesa nyingi sana kwa kukazia mambo yanayohusisha kuwasiliana na pepo. Kwa sababu hiyo, vijana wengi wamependezwa na mambo kama vile elimu ya nyota, roho waovu, watu wanaowanyonya wengine damu, na uchawi. Kwa nini? Sababu zinatia ndani:

  •   Udadisi: Ili kuchunguza ikiwa kweli kuna ulimwengu wa roho

  •   Mahangaiko: Ili kufahamu ni nini kitakachotukia wakati ujao

  •   Uhusiano: Ili kujaribu kuwasiliana na mpendwa aliyekufa

 Huenda sababu hizo zisiwe mbaya. Kwa mfano, ni jambo la kawaida kujiuliza wakati ujao utakuwaje au kumkosa mpendwa wetu aliyekufa. Lakini kuna hatari ambazo unapaswa kuzifahamu.

 Kwa nini ujihadhari?

 Biblia inatoa maonyo makali dhidi ya kufanya chochote kinachohusiana na kuwasiliana na pepo. Kwa mfano, inasema:

 “Asipatikane miongoni mwenu . . . mtu yeyote anayefanya uaguzi, mtu yeyote anayefanya uchawi, mtu yeyote anayetafuta ishara za ubashiri, mlozi, mtu yeyote anayewafunga wenzake kwa uchawi, mtu yeyote anayetafuta ushauri kutoka kwa watu wanaowasiliana na roho, mpiga ramli, au mtu yeyote anayetafuta habari kuhusu wafu. Kwa maana mtu yeyote anayefanya mambo haya ni chukizo kwa Yehova.”​—Kumbukumbu la Torati 18:10-​12.

 Kwa nini Biblia inashutumu vikali kuwasiliana na pepo?

  •   Kuwasiliana na pepo kunaonyesha tunawaunga mkono. Biblia inafundisha kwamba malaika fulani walimwasi Mungu na kujifanya wenyewe kuwa maadui wake. (Mwanzo 6:2; Yuda 6) Malaika hao waovu wanaoitwa roho waovu, huwapotosha watu kupitia wapiga-ramli, wanajimu, na waaguzi. Kushiriki matendo hayo kutatufanya tuwe maadui wa Mungu.

  •   Kuwasiliana na pepo kunaendeleza wazo la uwongo kwamba kuna wanadamu fulani ambao wanaweza kutabiri wakati ujao. Hata hivyo, ni Mungu peke yake anayeweza kusema hivi: “Tangu mwanzo ninatabiri matokeo, na tangu zamani za kale mambo ambayo bado hayajafanywa.”​—Isaya 46:10; Yakobo 4:13, 14.

  •   Kuwasiliana pepo kunaendeleza imani ya uwongo kwamba wafu wanaweza kuwasiliana na walio hai. Hata hivyo, Biblia inasema hivi: “Waliokufa hawajui jambo lolote kamwe . . . Hakuna kazi wala mipango wala ujuzi wala hekima Kaburini.”​—Mhubiri 9:​5, 10.

 Kwa sababu hizo, Mashahidi wa Yehova wanaepuka mazoea yanayohusiana na kuwasiliana na pepo. Pia wanaepuka burudani zinazoonyesha mizuka, watu wanaowanyonya wengine damu, na nguvu zisizo ya asili. Msichana anayeitwa Maria anasema hivi: “Ikiwa inatia ndani chochote kinachohusiana na roho waovu, sipaswi kuitazama.” a

Kama tu mhalifu anavyojaribu kukupumbaza kwamba yeye ni mtu tofauti, roho waovu hujifanya kuwa wapendwa wako waliokufa

 Unachoweza kufanya

  •   Lifanye liwe azimio lako “kudumisha dhamiri safi” mbele za Yehova kwa kuepuka zoea lolote au burudani inayohusisha kuwasiliana na pepo.​—Matendo 24:16.

  •   Haribu chochote unachomiliki ambacho kinahusiana na roho waovu. Soma Matendo 19:19, 20, uone mfano mzuri uliowekwa na Wakristo wa karne ya kwanza kuhusu jambo hilo.

Kumbuka: Unapopinga mazoea na burudani za kuwasiliana na pepo, unachukua msimamo upande wa Yehova. Na hilo huufanya moyo wake ushangilie!​—Methali 27:11.

a Hilo halimaanishi kwamba hadithi zote za kubuniwa zinahusiana moja kwa moja na kuwasiliana na pepo. Hata hivyo, Wakristo hutumia dhamiri yao iliyozoezwa na Biblia kuepuka zoea lolote au burudani inayohusiana na roho waovu.​—2 Wakorintho 6:​17; Waebrania 5:​14.