Matendo ya Mitume 24:1-27

  • Mashtaka dhidi ya Paulo (1-9)

  • Paulo ajitetea mbele ya Feliksi (10-21)

  • Kesi ya Paulo yacheleweshwa kwa miaka miwili (22-27)

24  Siku tano baadaye kuhani mkuu Anania+ akashuka pamoja na baadhi ya wazee na msemaji wa hadharani* aliyeitwa Tertulo, nao wakawasilisha kesi yao dhidi ya Paulo mbele ya gavana.+  Alipoitwa, Tertulo akaanza kumshtaki, akisema: “Kwa kuwa tunafurahia amani nyingi kupitia kwako, na kwa busara yako mabadiliko yanatokea katika taifa hili,  nyakati zote na kila mahali tunatambua jambo hilo kwa shukrani nyingi sana, ewe Mtukufu Feliksi.  Lakini ili nisitumie muda wako mwingi, ninakuomba kwa fadhili zako utusikilize kwa ufupi.  Kwa maana tumemwona mtu huyu kuwa msumbufu,*+ akichochea uasi+ miongoni mwa Wayahudi wote katika dunia yote inayokaliwa, naye ni kiongozi wa madhehebu ya Wanazareti.+  Pia alijaribu kulichafua hekalu, basi tukamkamata.+ 7 * ——  Wewe mwenyewe utakapomhoji, utagundua mambo haya yote ambayo tunamshtaki.”  Ndipo Wayahudi pia wakajiunga katika shambulio hilo, wakisisitiza kwamba mambo hayo ni ya kweli. 10  Gavana alipomtolea Paulo ishara ili azungumze, akajibu: “Ninajua vema kwamba umekuwa mwamuzi wa taifa hili kwa miaka mingi, nami nafurahi kujitetea mbele yako.+ 11  Unaweza kujihakikishia kwamba hazijapita zaidi ya siku 12 tangu nilipopanda kwenda kuabudu huko Yerusalemu;+ 12  nao hawakunipata hekaluni nikibishana na mtu yeyote wala kuchochea kikundi chenye ghasia, katika masinagogi au kotekote jijini. 13  Wala hawawezi kukuthibitishia mambo wanayonishtaki sasa hivi. 14  Lakini ninakiri jambo hili kwako, kwamba kulingana na njia wanayoiita ‘madhehebu,’ hivyo ndivyo ninavyomtolea utumishi mtakatifu Mungu wa mababu zangu,+ kwa kuwa ninaamini mambo yote yaliyo katika Sheria na yaliyoandikwa katika Manabii.+ 15  Nami nina tumaini kwa Mungu, tumaini ambalo watu hawa pia wanatazamia, kwamba kutakuwa na ufufuo+ wa waadilifu na wasio waadilifu pia.+ 16  Kwa sababu hiyo sikuzote ninajitahidi kudumisha dhamiri safi* mbele za Mungu na wanadamu.+ 17  Sasa baada ya miaka kadhaa, nilirudi ili kuleta zawadi za rehema+ kwa taifa langu na kutoa matoleo. 18  Nilipokuwa nikishughulikia mambo hayo, walinikuta hekaluni nikiwa nimetakaswa kisherehe,+ lakini sikuwa na umati wala sikuwa ninasababisha fujo. Lakini kulikuwa na Wayahudi fulani kutoka mkoa wa Asia 19  ambao wanapaswa kuwa hapa mbele yako ili wanishtaki ikiwa kwa kweli wana jambo lolote dhidi yangu.+ 20  Au uwaambie watu walio hapa waseme wenyewe kosa walilopata nilipokuwa nimesimama mbele ya Sanhedrini, 21  isipokuwa jambo hili moja nililosema kwa sauti kubwa nilipokuwa nimesimama kati yao: ‘Mimi ninahukumiwa leo mbele yenu kwa sababu ya ufufuo wa wafu!’”+ 22  Hata hivyo, Feliksi, akiwa anajua vizuri ukweli kuhusu Njia hii,+ akaahirisha kesi yao kwa kusema: “Lisia kamanda wa jeshi atakapokuja, nitaamua mambo haya yanayowahusu.” 23  Naye akamwagiza ofisa wa jeshi kwamba mtu huyo awekwe chini ya kizuizi lakini apewe uhuru fulani, na watu wake waruhusiwe kumhudumia. 24  Siku kadhaa baadaye Feliksi akaja na Drusila mke wake, aliyekuwa Myahudi, akawatuma watu wamwite Paulo naye akamsikiliza akizungumza kuhusu imani katika Kristo Yesu.+ 25  Lakini Paulo alipokuwa akiongea kuhusu uadilifu na kujizuia* na hukumu itakayokuja,+ Feliksi akaogopa na kumwambia: “Kwa sasa unaweza kwenda, lakini nitakapopata nafasi nitakuita tena.” 26  Wakati huohuo alitumaini kwamba Paulo angempa pesa. Kwa hiyo, akamwita mara nyingi na kuzungumza naye. 27  Lakini miaka miwili ilipokwisha, Porkio Festo alichukua nafasi ya Feliksi; na kwa sababu Feliksi alitamani kukubaliwa na Wayahudi,+ akamwacha Paulo akiwa amefungwa.

Maelezo ya Chini

Au “mwanasheria.”
Tnn., “tauni.”
Au “dhamiri isiyo na lawama.”
Au “kujidhibiti; kujiweza.”