Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Uumbaji au Mageuzi?​—Sehemu ya 3: Kwa Nini Uamini Uumbaji?

Uumbaji au Mageuzi?​—Sehemu ya 3: Kwa Nini Uamini Uumbaji?

“Ikiwa unaamini uumbaji, watu wanaweza kufikiri kwamba wewe ni mjinga, na unashikilia imani za kitoto ulizofundishwa na wazazi wako, au umepumbazwa na dini.”​—Jeanette.

 Je, unahisi kama Jeanette anavyohisi? Ikiwa ndivyo, unaweza kuanza kutilia shaka imani yako katika uumbaji. Kwa kweli, hakuna mtu anayependa kuonwa kuwa mjinga. Ni nini kinachoweza kukusaidia?

 Mambo yanayofanya iwe vigumu kuamini uumbaji

 1. Ukiamini uumbaji, watu watafikiri unapinga sayansi.

 “Mwalimu wangu alisema kwamba watu wanaoamini uumbaji ni wavivu sana ndio sababu hawawezi kueleza jinsi ulimwengu unavyofanya kazi.”​—Maria.

 Unalopaswa kujua: Walio na maoni kama hayo hawajui ukweli wa mambo. Wanasayansi maarufu kama vile Galileo na Isaac Newton waliamini katika Muumba. Imani yao haikupingana na upendo wao kwa sayansi. Vivyo hivyo, wanasayansi fulani leo hawaoni kwamba sayansi inapingana na imani katika uumbaji.

 Jaribu kufanya hivi: Chapa maneno (kutia ndani alama za kufungua na kufunga semi) “anaeleza kwa nini anamwamini Mungu” katika kisanduku cha kutafuta katika Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO ili upate mifano ya wanatiba na wanasayansi wanaoamini uumbaji. Ona mambo yaliyowasaidia kufikia mkataa huo.

 Jambo kuu: Kuamini uumbaji hakumaanishi kwamba unapinga sayansi. Kwa kweli, kujifunza mengi kuhusu ulimwengu unaotuzunguka kunaweza kuimarisha imani yako katika uumbaji.​—Waroma 1:​20.

2. Ikiwa unaamini masimulizi ya Biblia ya uumbaji, watu watafikiri una msimamo mkali wa kidini.

 “Watu wengi wanafikiri kwamba kuamini uumbaji ni mzaha tu. Wanahisi kwamba simulizi la kitabu cha Mwanzo ni hadithi tu.”​—Jasmine.

 Unalopaswa kujua: Mara nyingi watu huwa na maoni yasiyo sahihi kuhusu simulizi la Biblia la uumbaji. Kwa mfano, watu fulani wanaoamini uumbaji wanadai kwamba dunia iliumbwa hivi karibuni au wanadai kuwa kila kitu kilicho hai kiliumbwa katika siku sita zenye saa 24. Biblia haiungi mkono maoni hayo yote.

  •   Mwanzo 1:1 husema hivi: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” Jambo hilo halipingani na uthibitisho wa kisayansi kwamba dunia imekuwapo kwa mabilioni ya miaka.

  •   Neno “siku” kama linavyotumiwa katika kitabu cha Mwanzo linaweza kumaanisha vipindi virefu vya nyakati. Kwa kweli, katika Mwanzo 2:4 neno “siku” limetumiwa kufafanua siku zote sita za uumbaji.

 Jambo kuu: Simulizi la Biblia kuhusu uumbaji linapatana na mambo hakika ya kisayansi.

 Changanua imani yako

 Kuamini katika uumbaji hakumaanishi “kuamini jambo bila kufikiri.” Badala yake, kunategemea sababu zenye kusadikisha. Fikiria hili:

 Mambo yote tunayopitia maishani yanakufunza kwamba palipo na ubuni, pana mbuni. Unapoona kamera, ndege, au nyumba, unafikia mkataa sahihi kwamba mtu fulani alivibuni. Kwa nini usifikie mkataa huohuo sahihi unapochunguza jicho la mwanadamu, ndege aliye angani, au sayari yetu Dunia?

 Jambo la kufikiria: Mara nyingi wahandisi huiga mambo wanayoona katika uumbaji ili waboreshe vitu wanavyobuni, nao hudai kwa haki watu watambue kazi zao. Je, ni jambo linalopatana na akili kukubali mbuni wa kibinadamu na kazi zake na bado tusikubali kuwapo kwa Muumba na ubunifu Wake wa hali ya juu sana?

Je, ni jambo linalopatana na akili kufikiri kwamba ndege ya kubeba abiria ilibuniwa lakini ndege wa angani hakuumbwa?

 Vifaa vya kukusaidia kuchunguza uthibitisho

 Unaweza kuimarisha usadikisho wako katika uumbaji kwa kuchunguza uthibitisho unaopatikana katika vitu vya asili.

 Jaribu kufanya hivi: Chapa maneno (kutia ndani alama za kufungua na kufunga semi) “je, ni kazi ya ubuni?” katika kisanduku cha kutafuta cha Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO. Chagua baadhi ya vichwa vinavyokupendeza kutoka katika mfululizo wa gazeti la Amkeni! wenye kichwa “Je, Ni Kazi ya Ubuni?” Katika kila makala, ona jambo la pekee kuhusu uumbaji uliozungumziwa hapo. Jambo hilo linakuthibitishiaje kwamba kuna Mbuni?

 Jifunze zaidi: Tumia broshua zifuatazo kuchunguza zaidi uthibitisho wa uumbaji.

  •  Uhai—Ulitokana na Muumba?

    •   Dunia iko mahali panapofaa kabisa na imeumbwa kwa njia inayoweza kutegemeza uhai.​—Tazama ukurasa wa 4-​10.

    •   Mifano ya ubuni inapatikana katika uumbaji.​—Tazama ukurasa wa 11-​17.

    •   Simulizi la kitabu cha Mwanzo lililo katika Biblia linapatana na sayansi.​—Tazama ukurasa wa 24-​28.

  •  Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai

    •   Uhai haungeweza kutokea tu kutoka katika vitu visivyo hai.​—Tazama ukurasa wa 4-7.

    •   Vitu vilivyo hai ni tata sana hivi kwamba haviwezi kujitokeza tu bila mwongozo wowote.​—Tazama ukurasa wa 8-​12.

    •   Habari zilizo katika chembe za urithi ni za hali ya juu kuliko teknolojia ya kisasa.​—Tazama ukurasa wa 13-​21.

    •   Vitu vyote vilivyo hai havikutoka katika chanzo kimoja cha zamani. Rekodi ya wanyama wa zamani inaunga mkono kutokea kwa ghafla kwa vikundi vikuu vya wanyama, na si kwamba vilitokea hatua kwa hatua.​—Tazama ukurasa wa 22-​29.

 “Ulimwengu unanisadikisha kabisa kwamba kuna Mungu, kuanzia na wanyama duniani hadi katika ulimwengu na utaratibu uliomo.”​—Thomas.