Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninaweza Kumalizaje Kazi za Shule?

Ninaweza Kumalizaje Kazi za Shule?

 “Inachosha sana kuwa macho saa 7:00 usiku ukifanya kazi za shule. Kitu unachofikiria ni kulala tu.”—David.

 “Nyakati fulani nilikuwa nikikaa macho mpaka saa 10:30 alfajiri nikisoma, kisha ningeamka saa 12:00 kamili ili niende shule. Kufanya hivyo kulikuwa kujiumiza tu.”—Theresa.

 Je, umelemewa na kazi nyingi za shule? Ikiwa ndivyo, makala hii itakusaidia.

 Kwa nini walimu huwapa wanafunzi kazi za kufanyia nyumbani?

 Kazi unazopewa ukafanyie nyumbani:

  •   zinaongeza kiwango cha ujuzi wako

  •   zinakufundisha jinsi ya kuwajibika

  •   zinaboresha uwezo wako wa kutumia wakati vizuri

  •   zinakusaidia kuelewa vizuri zaidi mambo uliyofundishwa darasani a

 “Kuwapa wanafunzi kazi za shule ni njia ya kuhakikisha kwamba watafanyia kazi mambo waliyojifunza badala ya kuyaruhusu yaingie kupitia sikio moja na kutokea sikio lingine.”—Marie.

 Masomo ya hesabu na sayansi hasa hukuza ustadi wako wa kutatua matatizo. Wataalamu wanasema kwamba hilo linaweza kukusaidia kuboresha mfumo wako wa neva ili uweze kufikiri zaidi. Kwa hiyo, kazi unazopewa ukafanyie nyumbani zinasaidia ubongo wako kufanya mazoezi!

 Huwezi kuepuka kupewa kazi za shule, iwe unatambua faida yake au la. Jambo zuri ni kwamba ingawa huwezi kudhibiti kiasi cha kazi za shule utakazopewa, unaweza kupunguza muda utakaotumia kuzikamilisha. Acha tuone jinsi unavyoweza kufanya hivyo.

 Mapendekezo ya jinsi ya kusoma

 Ikiwa unaona ni vigumu kukamilisha kazi za shule, huenda suluhisho likawa, si kutumia nguvu nyingi, bali kutumia akili zaidi. Jaribu mambo yafuatayo.

  •   Pendekezo la 1: Panga mapema. Biblia inasema: “Mipango ya wenye bidii hakika huleta mafanikio.” (Methali 21:5) Hakikisha kwamba una vifaa vyote ili utakapoanza kusoma usihitaji kusimama kila mara.

     Pia, chagua mahali ambapo hutakengeushwa unaposoma. Wengine hupenda kusoma katika chumba chenye mwanga wa kutosha na kisicho na kelele wakiwa nyumbani. Na wengine hupenda kusomea sehemu nyingine, labda wakiwa kwenye maktaba.

     “Kuwa na daftari la kuandikia ratiba yako kunaweza kukusaidia kupanga muda wako kwa busara. Unapojua vizuri kazi unayopaswa kufanya na muda unaopaswa kuimaliza, maisha yako hayatakuwa na mkazo sana.”—Richard.

  •   Pendekezo la 2: Panga kazi yako. Biblia inasema: “Mambo yote na yatendeke kwa . . . mpango.” (1 Wakorintho 14:40) Ukiwa na hilo akilini, chagua utaratibu utakaotumia kufanya kazi zako.

     Baadhi ya watu hupendelea kuanza na kazi ngumu zaidi. Wengine hupenda kuanza na kazi rahisi ili wajihisi vizuri, au wafurahi kwamba wamekamilisha kitu fulani. Chagua njia ambayo itakufaa.

     “Inasaidia sana kuwa na orodha ya mambo unayohitaji kufanya na kuamua utayafanya kwa mfuatano gani. Ukifanya hivyo, hutahisi kwamba umelemewa na kazi zako.”—Heidi.

  •   Pendekezo la 3: Anza kazi. Biblia inasema: “Iweni wenye bidii, msiwe wavivu.” (Waroma 12:11) Usiruhusu shughuli nyingine zikunyang’anye wakati unaohitaji kufanya kazi za shule hata ikiwa shughuli hizo zinavutia kadiri gani.

     Huenda watu wenye zoea la kuahirisha mambo wakakosa kutimiza kazi kwa wakati au kuzifanya haraka-haraka. Kufanya hivyo kunaweza kuathiri ubora wa kazi zao au kumfanya mtu asielewe masomo yake kwa kadiri inayofaa. Unaweza kujipunguzia mkazo usio wa lazima kwa kuanza kazi za shule haraka iwezekanavyo.

     Nilipofanya kazi zangu mara tu nilipotoka shuleni au nilipoanza mradi fulani mara tu nilipoupokea, sikuhitaji kuwa na wasiwasi kuuhusu baadaye na haukunizuia kufanya shughuli nyingine.”—Serina.

     DOKEZO: Fanya kazi zako za shule wakati uleule kila siku. Hilo litaboresha uwezo wako wa kujidhibiti na litakusaidia kudumisha ratiba yako.

  •   Pendekezo la 4: Usikengeuke. Biblia inasema: “Yakaze macho yako moja kwa moja mbele yako.” (Methali 4:25) Ili kufuata shauri hilo unaposoma, unahitaji kuepuka vitu vinavyoweza kukukengeusha hasa vifaa vya kielektroni.

     Kutumia mtandao na kutuma ujumbe kunaweza kukufanya utumie muda mwingi zaidi kumaliza kazi za shule. Lakini ukiwa makini, utagundua kwamba huna mkazo mwingi na pia una muda mwingi zaidi wa kufanya mambo.

     “Ni vigumu kukaza fikira kunapokuwa na simu, kompyuta, michezo ya video, na televisheni. Kinachonisaidia ni kuzima simu yangu na vitu vingine vyote vinavyoweza kunikengeusha fikira.”—Joel.

  •   Pendekezo la 5: Uwe na usawaziko. Biblia inasema: “Usawaziko wenu na ujulikane.” (Wafilipi 4:5) Punguza mkazo wa kufanya kazi za shule kwa kuwa na vipindi vya mapumziko. Nenda ukatembee, endesha baiskeli, au ukimbie.

     Ikiwa bado unahisi kwamba umelemewa na kazi za shule, zungumza na walimu wako. Wakiona kwamba unajaribu kufanya yote unayoweza, huenda wakachochewa kufanya mabadiliko.

     “Usiruhusu mkazo wa kazi za shule ukulemee. Tia jitihada. Kuna mambo fulani ambayo hupaswi kuyaruhusu yakupotezee usawaziko, na mojawapo ya mambo hayo ni kazi za shule.”—Julia.

 Maswali ya kujiuliza:

  •   Nitahitaji vifaa gani ili kufanya kazi za shule?

  •   Ni wakati gani unaofaa zaidi ili kufanya kazi za shule?

  •   Nikae wapi ili nifaulu kukaza fikira zaidi?

  •   Nifanye nini ili niepuke kuahirisha mambo?

  •   Ni mambo gani yanayoweza kunikengeusha?

  •   Ninaweza kufanya nini ili kuepuka vikengeusha fikira—iwe vya kielektroni au vya aina nyingine?

  •   Ninawezaje kuwa na usawaziko ninapofanya kazi za shule?

 JAMBO MUHIMU LA KUKUMBUKA: Hakikisha unaelewa kazi ya shule uliyopewa inahusisha nini. Ikiwa una maswali, muulize mwalimu kabla ya kuondoka darasani.

a Mambo makuu yametolewa katika kitabu School Power, cha Jeanne Schumm.