Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Je, Nibatizwe?—Sehemu ya 3: Kwa Nini Ninasitasita Kubatizwa?

Je, Nibatizwe?—Sehemu ya 3: Kwa Nini Ninasitasita Kubatizwa?

 Je, wazo la kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa linakufanya uwe na wasiwasi? Ikiwa ndivyo, makala hii itakusaidia kushinda woga huo.

Katika makala hii

 Vipi nikifanya kosa zito baada ya kubatizwa?

 Kwa nini wengine wana wasiwasi? Huenda unamfahamu mtu ambaye alitenda dhambi nzito na akahitaji kuondolewa kutanikoni. (1 Wakorintho 5:11-13) Huenda ukahofia kwamba hilo litakupata.

 “Nilipofikiria kuhusu kubatizwa, wazo la kukosea liliniogopesha. Niliwazia jinsi ambavyo hilo lingewaathiri sana wazazi wangu.”—Rebekah.

 Andiko la msingi: “Mtu mwovu na aiache njia yake . . . Na arudi kwa Yehova, ambaye atamwonyesha rehema, kwa Mungu wetu, kwa maana atasamehe kwa njia kubwa.”—Isaya 55:7.

 Fikiria hili: Ingawa wakosaji wasiotubu huondolewa kutoka kutanikoni, Yehova huwaonyesha rehema wale wanaotubu kwa unyenyekevu na kukubali kurekebishwa.—Zaburi 103:13, 14; 2 Wakorintho 7:11.

 Licha ya hilo, ukweli wa mambo ndio huu: Hata ingawa wewe si mkamilifu, unaweza kushinda vishawishi kwa msaada wa Mungu. (1 Wakorintho 10:13) Isitoshe, ni nani anayeamua jinsi utakavyotenda? Ni wewe? Au ni mtu mwingine?

 “Nilihofia kwamba ningefanya kosa zito baada ya kubatizwa, lakini nikatambua kwamba ningekuwa nikikosea ikiwa nisingebatizwa. Nilitambua kwamba sipaswi kuogopa mambo ambayo huenda yakatokea kesho yanizuie kufanya ninayopaswa kufanya leo.”—Karen.

 Jambo kuu: Unaweza kuamua kuepuka kufanya dhambi nzito—kama tu watumishi wengi wa Yehova wanavyoepuka.—Wafilipi 2:12.

 Je, unahitaji msaada zaidi? Ona makala “Ninaweza Kupinga Vishawishi Jinsi Gani?

 Vipi ikiwa ninaogopa wajibu unaotokana na kubatizwa?

 Kwa nini wengine wana wasiwasi? Kwa mfano, huenda unawafahamu vijana ambao wamehamia mbali na familia na marafiki ili kupanua utumishi wao kwa Yehova. Huenda ukawa na wasiwasi kwamba watu watatazamia ufanye vivyo hivyo.

 “Mkristo aliyebatizwa anaweza kupata mapendeleo zaidi, lakini watu fulani hawako tayari kujitoa au hali zao haziwaruhusu kufanya hivyo.”—Marie.

 Andiko la msingi: “Kila mmoja na achunguze matendo yake mwenyewe, kisha atakuwa na sababu ya kushangilia kuhusiana na yeye mwenyewe, na si kwa kujilinganisha na mtu mwingine.”—Wagalatia 6:4.

 Fikiria hili: Badala ya kujilinganisha na wengine, kazia fikira maneno ya Marko 12:30: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote.”

 Ona kwamba unapaswa kumtumikia Yehova kwa moyo wako wote—si wa mtu mwingine. Ikiwa kweli unampenda Yehova, utatafuta njia za kumtumikia kwa kadiri ya uwezo wako.

 “Ingawa ubatizo ni hatua muhimu, si mzigo mzito. Ukishirikiana na marafiki wazuri, watakusaidia. Kushughulikia majukumu mazito hatua kwa hatua kutakufanya uwe mwenye furaha. Ukiepuka kubatizwa utakuwa ukijidhuru mwenyewe.”—Julia.

 Jambo kuu: Sitawisha uthamini kuelekea upendo ambao Yehova amekuonyesha. Hilo litakuchochea kumpa kilicho bora.—1 Yohana 4:19.

 Je, unahitaji msaada zaidi? Ona makala “Je, Mimi Huchukua Mambo kwa Uzito?

 Vipi ikiwa ninahisi sistahili kumtumikia Yehova?

 Kwa nini wengine wana wasiwasi? Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote; wanadamu si kitu wanapolinganishwa naye! Huenda ukajiuliza ikiwa kweli Yehova anajua kwamba wewe upo.

 “Kwa sababu wazazi wangu ni Mashahidi wa Yehova, nilikuwa na wasiwasi kwamba nilikuwa ‘nimerithi’ tu urafiki wangu na Yehova kutoka kwao na kwamba Yehova hakuwa amenivuta kibinafsi.”—Natalie.

 Andiko la msingi: “Hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba aliyenituma amvute.”—Yohana 6:44.

 Fikiria hili: Uhakika wa kwamba unafikiria kubatizwa unaonyesha kwamba Yehova anakuvuta uwe na urafiki wa karibu naye. Je, isingefaa kukubali mwaliko huo?

 Kumbuka pia kwamba Yehova—si wewe au mtu mwingine—ndiye anayeweka viwango kwa ajili ya wale atakaowavuta kwake. Na Neno lake linatuhakikisha kwamba ‘ukimkaribia Mungu, atakukaribia.’Yakobo 4:8.

 “Uhakika wa kwamba unafahamu kumhusu Yehova na kwamba umevutwa kwake ni uthibitisho kwamba anakupenda. Kwa hiyo, akili yako inapokuambia hustahili kumtumikia, jikumbushe kwamba yeye hakubaliani na wazo hilo. Na sikuzote Yehova yuko sahihi.”—Selina.

 Jambo kuu: Ikiwa unatimiza viwango vya Biblia kwa ajili ya ubatizo, basi unastahili kumtumikia Yehova. Mbali na hilo, anastahili ibada yako.—Ufunuo 4:11.

 Je, unahitaji msaada zaidi? Ona makala “Kwa Nini Ninapaswa Kusali?