Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninaweza Kuizoezaje Dhamiri Yangu?

Ninaweza Kuizoezaje Dhamiri Yangu?

 Dhamiri yako inaweza kulinganishwa na nini kati ya yafuatayo?

  •   dira

  •   kioo

  •   rafiki

  •   hakimu

 Jibu sahihi ni vyote vinne. Katika makala hii tutaeleza sababu.

 Dhamiri ni nini?

 Dhamiri yako ni hisi ya ndani inayokusaidia kutambua mema na mabaya. Biblia inasema ni kama “sheria iliyoandikwa katika moyo wa mwanadamu.” (Waroma 2:15, Contemporary English Version) Dhamiri njema inaweza kukusaidia kuchanganua njia unayotaka kufuata au ambayo tayari umefuata.

  •   Dhamiri yako ni kama dira. Inakuongoza katika njia inayofaa ili uepuke matatizo.

  •   Dhamiri yako ni kama kioo. Inakuonyesha maadili yako, na kufunua aina ya mtu uliye kwa ndani.

  •   Dhamiri yako ni kama rafiki mzuri. Inaweza kukupa ushauri unaofaa na kukusaidia kufanikiwa—ukiisikiliza.

  •   Dhamiri yako ni kama hakimu. Inakuhukumu unapotenda jambo baya.

Dhamiri nzuri inaweza kukusaidia kufanya uamuzi kwa hekima

 Jambo kuu: Dhamiri yako ni kifaa muhimu kinachoweza kukusaidia (1) kufanya maamuzi yenye hekima na (2) kusahihisha makosa yako.

 Kwa nini uizoeze dhamiri yako?

 Biblia inatuambia ‘tuwe na dhamiri njema.’ (1 Petro 3:16) Ni vigumu kudumisha dhamiri njema ikiwa haijazoezwa.

 “Nilikuwa na kawaida ya kuwadanganya wazazi wangu kuhusu mahali nilipokuwa. Mwanzoni dhamiri yangu ilinisumbua, lakini kadiri muda ulivyopita nilianza kuhisi kwamba sikuwa nikifanya jambo baya sana.”—Jennifer.

 Hatimaye, dhamiri ya Jennifer ilimchochea kuwaambia wazazi wake alichokuwa akifanya na akaacha kuwadanganya.

 Jambo la kufikiria: Dhamiri ya Jennifer ilipaswa kumchoma wakati gani?

 “Maisha yanakuwa na mkazo unapoishi maisha ya kinafiki. Dhamiri yako ikikuruhusu kufanya uamuzi mmoja mbaya, itakuwa rahisi kwako kufanya uamuzi mwingine mbaya.”—Matthew.

 Baadhi ya watu huipuuza dhamiri yao kabisa. Biblia inasema, “wamepotoka kabisa kimaadili.” (Waefeso 4:19) Tafsiri ya Biblia Habari Njema inasema: “Hawana aibu.”

 Jambo la kufikiria: Unafikiri watu wanaofanya mambo mabaya bila kuwa na hisia za hatia wana maisha bora zaidi? Hatimaye watapatwa na matatizo gani?

 Jambo kuu: Ili kuwa na dhamiri nzuri, unahitaji ‘kuzoeza nguvu zako za utambuzi kwa kuzitumia ili kutofautisha mambo yaliyo sawa na mambo yasiyo sawa.’—Waebrania 5:14.

 Unaweza kuzoezaje dhamiri yako?

 Ili kuzoeza dhamiri yako, unahitaji viwango ambavyo unaweza kuvitumia kupima matendo yako. Baadhi ya watu hufuata viwango vilivyowekwa na:

  •   familia na utamaduni

  •   watu wa rika lao

  •   watumbuizaji maarufu

 Hata hivyo, kiwango kinachowekwa na Biblia cha jinsi tunavyopaswa kuishi ndicho kiwango bora zaidi. Jambo hilo halishangazi kwa sababu Biblia ‘imeongozwa na roho ya Mungu,’ Muumba wetu, anayejua kinachotufaa zaidi.—2 Timotheo 3:16.

 Fikiria mifano kadhaa.

 KIWANGO: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”—Waebrania 13:18.

  •   Kiwango hicho kinaweza kuongozaje dhamiri yako unaposhawishiwa kuiba mtihani, kuwadanganya wazazi wako, au kuiba?

  •   Unafikiri unaweza kufaidikaje sasa na wakati ujao ikiwa dhamiri yako inakusukuma kuwa mnyoofu katika mambo yote?

 KIWANGO: “Ukimbieni uasherati.”—1 Wakorintho 6:18.

  •    Kiwango hicho kinaweza kuongozaje dhamiri yako unaposhawishiwa kutazama ponografia au kufanya ngono kabla ya kufunga ndoa?

  •   Unafikiri utafaidikaje sasa na wakati ujao ikiwa dhamiri yako inakusukuma kuukimbia uasherati?

 KIWANGO: “Mtendeane kwa fadhili, huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari.”—Waefeso 4:32.

  •    Kiwango hicho kinaweza kukuchocheaje ikiwa utakosa kuelewana na ndugu yako au rafiki yako?

  •   Unafikiri utafaidikaje sasa na wakati ujao ikiwa dhamiri yako inakusukuma kuwa mwenye kusamehe na mwenye huruma nyororo?

 KIWANGO: “Yehova . . . humchukia mtu yeyote anayependa ukatili.”—Zaburi 11:5.

  •    Kiwango hicho kinapaswa kukuongozaje unapochagua sinema, vipindi vya televisheni, au michezo ya video?

  •   Unafikiri utafaidikaje sasa na wakati ujao ikiwa dhamiri yako itakuchochea kukataa burudani zenye jeuri?

 SIMULIZI HALISI: “Nina marafiki ambao walikuwa wanacheza michezo ya video iliyohusisha jeuri, nami pia niliicheza. Kisha baba yangu akaniambia sipaswi kucheza michezo hiyo tena. Kwa hiyo, ningecheza michezo hiyo nilipowatembelea rafiki zangu. Niliporudi nyumbani, sikuzungumzia jambo hilo. Baba angeniuliza kilichokuwa kikinisumbua lakini nilisema niko sawa. Hata hivyo, siku moja nilisoma Zaburi 11:5 nami nikaanza kujisikia vibaya kuhusu jambo nililokuwa nikifanya. Nilitambua kwamba nilipaswa kuacha kucheza michezo hiyo ya video. Na kwa kweli niliacha kabisa. Mmoja wa rafiki zangu pia alichochewa kuacha kucheza michezo hiyo inayohusisha jeuri alipoona nimeacha kuicheza.”—Jeremy.

 Jambo la kufikiria: Dhamiri ya Jeremy ilianza kufanya kazi wakati gani, na ni wakati gani alianza kuisikiliza? Umejifunza nini kutokana na simulizi la Jeremy?

 Jambo kuu: Dhamiri yako inaonyesha wewe ni mtu wa aina gani na ni mambo gani yaliyo muhimu kwako. Dhamiri yako inasema nini kukuhusu?