Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Nifanye Nini Ili Niache Kufikiria Kuhusu Ngono Muda Wote?

Nifanye Nini Ili Niache Kufikiria Kuhusu Ngono Muda Wote?

 “Mimi huanza ghafla kufikiria kuhusu ngono na ninashindwa kufikiria jambo lingine lolote. Ni kana kwamba mtu mwingine anaongoza mawazo yangu.”—Vera.

 “Inaonekana haiwezekani kudhibiti mawazo kuhusu ngono. Nafikiri ni rahisi zaidi kwangu kuruka kama ndege kuliko ya kufanya hivyo.”—John.

 Je, umewahi kuhisi kama za Vera au John? Ikiwa ndivyo, makala hii itakusaidia.

 Kwa nini mawazo hayo hayafai?

 “Mjomba aliniambia kwamba Mungu asingenipa tamaa ya kufanya ngono ikiwa hakutaka niitosheleze,” anasema kijana anayeitwa Alex.

 Sehemu fulani ya maneno ya mjomba wa Alex ni ya kweli—Mungu ndiye aliyetupa tamaa ya ngono, na alifanya hivyo kwa sababu nzuri. Ikiwa wanadamu wasingalifanya ngono, jamii ya wanadamu isingalikuwepo leo. Ikiwa ndivyo, basi, kwa nini uhangaike sana kuhusu kuepuka kufikiria mambo ya ngono? Kuna sababu mbili nzuri:

  •   Biblia inafundisha kusudi la Mungu ni kwamba ngono inapaswa kufanywa na mwanamume na mwanamke waliooana tu.—Mwanzo 1:28; 2:24.

     Ikiwa unaheshimu viwango hivyo na hujafunga ndoa, kufikiria kuhusu ngono kutakukatisha tamaa tu. Hata kunaweza kufanya uingie katika kishawishi cha kufanya ngono—uamuzi ambao wengi wamesema kwamba walijutia baadaye.

  •   Kuepuka kufikiria sana kuhusu ngono kutakusaidia kukuza sifa ya kujizuia, na sifa hiyo ni muhimu sana maishani.1 Wakorintho 9:25.

 Sifa hiyo itakusaidia ufanikiwe zaidi maishani, sasa na wakati ujao. Kwa kweli, uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba watoto walio na sifa ya kujizuia hawakuwa na matatizo mengi baadaye maishani iwe ni ya kiafya, kiuchumi, au na wenye mamlaka. a

 Kwa nini ni vigumu?

 Homoni zinaweza kufanya iwe vigumu kuacha kufikiria kuhusu ngono. Mbali na hilo tunaishi katika ulimwengu unaofikiria ngono muda wote.

 “Inaonekana kwamba kila kipindi cha televisheni kinaonyesha ngono kabla ya ndoa kuwa jambo zuri, bila kuonyesha hatari zozote. Ni rahisi kuwa na mawazo yasiyofaa wakati ambapo ngono haramu zinaonyeshwa kuwa hazina madhara yoyote.”—Ruth.

 “Ninapokuwa kazini, ninawasikia watu wakitumia lugha chafu sana wanapozungumzia ngono, na ninaanza kuwa mdadisi. Maadili mapotovu yanafanywa kuwa ya kawaida sana hivi kwamba ni vigumu kuyafikiria kuwa mabaya.”—Nicole.

 “Ni rahisi kujisahau unapoangalia picha kwenye mtandao wa kijamii. Picha moja tu ya ngono inaweza kubaki akilini mwako na inakuwa vigumu sana kuisahau!”—Maria.

 Mambo kama hayo yanaweza kukufanya uhisi kama mtume Paulo alivyohisi. Aliandika hivi: “Ninapotaka kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami.”—Waroma 7:21.

Usiruhusu mawazo yasiyofaa yajenge kiota juu ya kichwa chako

 Unachoweza kufanya

 Elekeza fikira zako kwenye mambo mengine. Jaribu kukazia fikira mambo mengine badala ya ngono. Hilo linaweza kutia ndani kitu fulani unachopenda kufanya, mchezo fulani, mazoezi, au utendaji wowote unaoweza kukusaidia kukazia fikira jambo lingine. Kijana mwanamke anayeitwa Valerie anasema hivi: “Kusoma Biblia kunanisaidia. Biblia ina mawazo ya juu, na unapoyafikiria, huna muda mwingi wa kufikiria mambo mengine.”

 Ni kweli kwamba huenda mawazo kuhusu ngono yakaingia akilini mwako. Lakini una mamlaka kuhusu hatua utakayochukua. Ukipenda, una uwezo wa kuyaondoa.

 “Mawazo yangu yanapofuata mkondo huo, ninajitahidi kufikiria jambo lingine. Pia, ninajaribu kutambua kitu kilichofanya nianze kupata mawazo yasiyofaa—iwe ni wimbo au picha ninayohitaji kufuta.”—Helena.

 Kanuni ya Biblia: “Mambo yoyote yaliyo ya uadilifu, mambo yoyote yaliyo safi kiadili . . . endeleeni kuyafikiria mambo hayo.”—Wafilipi 4:8.

 Tafuta marafiki wazuri. Ikiwa marafiki wako wanazungumzia ngono wakati wote, itakuwa vigumu kudumisha mawazo safi.

 “Nilipokuwa tineja, nilipambana na fikira zisizofaa, na sababu kuu iliyochangia tatizo hilo ni watu nilioshirikiana nao. Unapokuwa na watu wanaochochea tamaa zisizofaa, unakazia fikira hisia zako—na hilo linafanya hali iwe mbaya zaidi.”—Sarah.

 Kanuni ya Biblia: “Anayetembea na wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wapumbavu ataumia.”—Methali 13:20.

 Epuka burudani zisizofaa. Ni wazi kwamba kila sehemu ya ulimwengu wa burudani inakazia ngono. Nicole anasema, “Katika kisa changu, muziki unachangia sana. Muziki unaweza kuchochea tamaa hivi kwamba ninaanza kulemewa nazo.”

 “Nilianza kutazama sinema na vipindi vya televisheni vilivyoonyesha mahusiano ya kingono. Muda si muda, nikaanza kufikiria sana kuhusu ngono. Ilikuwa rahisi kujua chanzo cha mawazo hayo. Mara tu nilipoacha kuzitazama, sikuwa na mawazo mengi kuhusu ngono. Kuchagua burudani kunafanya iwe rahisi kupinga mawazo yasiyofaa.”—Joanne.

 Kanuni ya Biblia: “Uasherati na kila namna ya ukosefu wa usafi au pupa visitajwe kamwe miongoni mwenu, kama inavyowafaa watu watakatifu.”—Waefeso 5:3.

 Jambo kuu: Watu fulani wanafikiri kwamba tamaa yao ya ngono ni muhimu sana hivi kwamba haipaswi na haiwezi kudhibitiwa. Lakini Biblia haisemi hivyo. Inatuheshimu kwa kusema kwamba tunaweza kudhibiti fikira zetu.

 Kanuni ya Biblia: “Mnapaswa kuendelea kufanywa upya katika nguvu zinazoongoza akili zenu.”—Waefeso 4:23.

a Hata watu waliofunga ndoa wanahitaji sifa ya kujizuia—hiyo ni sababu nyingine nzuri ya kusitawisha sifa hiyo ukiwa bado mseja.