Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Naweza Kukabilianaje na Msiba?

Naweza Kukabilianaje na Msiba?

 Msiba unaweza kumpata mtu yeyote. Biblia inasema hivi: “Si wenye mbio wanaoshinda katika mbio, wala wenye nguvu wanaoshinda katika pigano . . .  wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.” (Mhubiri 9:11) Hiyo inatia ndani baadhi ya vijana ambao wamepatwa na msiba. Wamekabilianaje na msiba huo? Fikiria mifano miwili.

 REBEKAH

 Wazazi wangu walitalikiana nikiwa na umri wa miaka 14.

 Nilijiambia talaka ya wazazi wangu haikuwa kweli, kwamba baba alihitaji tu wakati wa kuwa peke yake. Anampenda mama​—hawezi kumwacha. Hawezi​ kuniacha.

 Ilikuwa vigumu kwangu kuzungumza na yeyote kuhusu jambo hilo. Sikutaka kulifikiria. Nilikuwa mwenye hasira, ingawa sikutambua hivyo. Nilipata tatizo la kuhangaika, na kukosa usingizi.

  Nikiwa na umri wa miaka 19 mama yangu alikufa kwa sababu ya kansa. Alikuwa rafiki yangu wa karibu zaidi.

 Talaka ya wazazi wangu ilikuwa pigo, lakini kifo cha mama yangu kilikuwa pigo kubwa hata zaidi kwangu. Bado ninahuzunika. Imekuwa vigumu zaidi kwangu kupata usingizi, na bado nina mahangaiko.

 Hata hivyo, mambo kadhaa yamenisaidia. Kwa mfano, Methali 18:1 inatuonya tusijitenge na wengine, hivyo ninajitahidi kufuata shauri hilo.

 Pia, kwa kuwa mimi ni Shahidi wa Yehova, ninajitahidi kusoma machapisho yetu yenye kutia moyo yanayotegemea Biblia. Chapisho moja lililonisaidia wakati wa talaka ya wazazi wangu ni Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi. Ninakumbuka nikisoma sura yenye kichwa “Ninaweza Kuwa na Furaha Katika Familia ya Mzazi Mmoja?” kwenye Buku la 2.

 Andiko ambalo napenda zaidi na linalonisaidia kukabiliana na mahangaiko ni Mathayo 6:​25-34. Katika mstari wa 27, Yesu aliuliza hivi: “Ni nani kati yenu kwa kuhangaika anaweza kuongeza kipimo cha mkono mmoja a kwenye uhai wake?”

 Sote tutapatwa na misiba, lakini kielelezo cha mama kilinilifunza jinsi ya kukabiliana na magumu hayo kwa njia inayofaa. Alikabili hali ngumu​—talaka halafu ugonjwa usio na tiba​—licha ya hayo yote, alidumisha maoni yanayofaa, na imani yake kwa Mungu ilibaki ikiwa yenye nguvu hadi mwisho. Sitasahau mambo aliyonifunza kumhusu Yehova.

 Jambo la kufikiria: Kusoma Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia kunawezaje kukusaidia kukabiliana na msiba?​—Zaburi 94:19.

 CORDELL

 Nilishuhudia baba yangu akikata pumzi nikiwa na umri wa miaka 17. Kumpoteza baba ndilo jambo baya zaidi lililowahi kunipata maishani. Lilikuwa pigo kubwa kwangu.

 Sikuamini kuwa amekufa na kwamba ulikuwa mwili wa baba uliofunikwa na shuka. Nilijiambia, ‘Ataamka kesho.’ Nilikosa tumaini na nilivurugika sana.

 Sisi ni Mashahidi wa Yehova, na kutaniko letu lilitutegemeza sana baada ya kifo cha baba. Walitupikia, walijitolea kukaa nasi, na kututegemeza​—si kwa siku chache tu, bali kwa kuendelea. Hilo lilinisadikisha kwamba Mashahidi wa Yehova ni Wakristo wa kweli.​—Yohana 13:35.

 Andiko ambalo limenitia moyo sana ni 2 Wakorintho 4:​17, 18. Linasema hivi: “Kwa maana ingawa dhiki ni ya dakika na ni nyepesi, hiyo inatufanyizia utukufu wenye uzito mkubwa zaidi na zaidi na ni wa milele; huku tukiendelea kukaza macho yetu, si juu ya vitu vinavyoonekana, bali juu ya vitu visivyoonekana. Kwa maana vitu vinavyoonekana ni vya muda, lakini vitu visivyoonekana ni vya milele.”

 Mstari wa mwisho uliniimarisha sana. Kuteseka kwa baba kulikuwa kwa muda mfupi, lakini ahadi za Mungu za wakati ujao zitadumu milele. Kifo cha baba kilinipa nafasi ya kutafakari kuhusu maisha yangu na kubadili miradi yangu.

 Jambo la kufikiria: Misiba unayopata inawezaje kukusaidia kuchunguza upya miradi yako maishani?​—1 Yohana 2:17.

a Mkono mmoja ni sawa na sentimita 44.5, au inchi 17.5.