Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninawezaje Kuacha Kuishi Maisha Maradufu?

Ninawezaje Kuacha Kuishi Maisha Maradufu?

 Nyakati nyingine, baadhi ya waabudu wa Mungu hujiuliza ikiwa kweli kuna faida kutumia wakati na jitihada kuishi kulingana na kanuni za Biblia. (Zaburi 73:2, 3) Huenda hata wakaanza kufanya mambo yanayopingana na sheria ya Yehova huku wakiwaficha waabudu wenzao mwenendo wao mbaya.

 Makala hii imekusudiwa kuwasaidia wale ambao wameanza kuishi maisha kama hayo lakini wangependa kuacha.

Kwenye ukurasa huu

 Ni nini maana ya kuishi maisha maradufu?

 Kuishi maisha maradufu kunamaanisha kwamba unapokuwa na vijana wenzako humtii Yehova, unafanya mambo unayojua ni kosa; lakini unapokuwa na waabudu wenzako, unajifanya kana kwamba unataka kumtumikia Yehova. Ni kana kwamba unaishi maisha yenye sehemu mbili, na kila sehemu ni ya kinafiki.

 “Ukiishi maisha maradufu inamaanisha kwamba unaficha jambo fulani, kwa hiyo, hakuna anayefahamu wewe ni nani hasa. Bila shaka, kuishi maisha maradufu ni usaliti maradufu.”​—Erin.

 Je, wajua? Kuishi maisha maradufu kunaweza kuhusisha kufanya mambo faraghani ambayo unajua Yehova hapendi.

 “Nilipokuwa na umri wa miaka 14, nilianza kutazama picha chafu kwenye Intaneti. Nilipokuwa mbele ya watu, nilijifanya ninachukizwa na ponografia, lakini moyoni nilijua kwamba sikuchukizwa nayo.”​—Nolan.

 Kanuni ya Biblia: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia mmoja na kumpenda mwingine, au atashikamana na mmoja na kumdharau mwingine.”​—Mathayo 6:24

 Je, kuishi maisha maradufu kunamaanisha mimi ni mtu mbaya?

 Si lazima iwe hivyo. Ni kweli kwamba baadhi ya watu wameamua hawataki kuishi kulingana na viwango vya Biblia. Lakini je, hilo ni kweli kukuhusu? Au je, kuna sababu inayokufanya uishi maisha hayo, kama vile:

  •   Unaogopa kuonekana kuwa tofauti na vijana wenzako.

  •   Unahisi mapendezi yako yanapatana zaidi na ya wanafunzi wenzako kuliko na yale ya vijana walio katika kutaniko lako.

  •   Unahisi huna nguvu na uwezo wa kufuata sheria zote za Yehova.

 “Ninafikiri kwamba baadhi ya vijana wanaoishi maisha maradufu wanajihisi wakiwa wamestarehe wanapokuwa na watu ambao hawana viwango vya Kikristo kwa sababu wanataka tu kukubaliwa, na mtu yeyote yule.”​—David.

 Bila shaka, hizo si sababu nzuri za kuishi maisha maradufu. Hata hivyo, zinatusaidia kuelewa jinsi hata watu wazuri wanaweza kunaswa na mtego huo. Ikiwa jambo hilo limekupata, unaweza kufanya nini?

 Ninawezaje kuacha kuishi maisha maradufu?

  1.  1. Chunguza maisha yako sasa hivi. Jiulize: ‘Je, kweli hivi ndivyo ninavyotaka kuishi? Nikiendelea kuishi hivi, matokeo yatakuwaje?’

     Kanuni ya Biblia: “Mtu mwerevu huona hatari . . . , lakini wajinga husonga mbele na kupata madhara.”​—Methali 27:12.

  2.  2. Uwe mnyoofu. Zungumzia hali yako na wazazi wako au na rafiki mkomavu anayeheshimu sheria za Yehova. Watafurahi kwamba uliwaomba msaada. Na watakuwa na shangwe kwamba unataka kufanya jambo linalofaa!

    Ikiwa umeanguka katika shimo refu la maisha maradufu, omba msaada

     “Lilikuwa jambo gumu sana kwangu kuwafunulia wengine makosa niliyokuwa nimefanya, lakini mara tu nilipofanya hivyo, nilihisi vizuri sana.”​—Nolan.

     Kanuni ya Biblia: “Anayefunika makosa yake hatafanikiwa, lakini yeyote anayeyaungama na kuyaacha ataonyeshwa rehema.”​—Methali 28:13.

  3.  3. Kubali matokeo. Kumbuka kwamba ikiwa umekuwa ukiwaficha wazazi wako jambo fulani na pia kulificha kutaniko, umefanya iwe vigumu kwako kuaminika. Kwa sababu hiyo, huenda wazazi wako au wazee wa kutaniko wakakuwekea vizuizi fulani. Kubali matokeo hayo, na uazimie kujiendesha “kwa unyoofu katika mambo yote” kuanzia sasa na kuendelea.​—Waebrania 13:18.

     Kanuni ya Biblia: “Sikiliza mashauri na ukubali nidhamu, ili uwe na hekima wakati wako ujao.”​—Methali 19:20.

  4.  4. Sitawisha imani yenye nguvu kwamba Mungu anakupenda. Kwa kuwa Yehova anatupenda, anafahamu kabisa kila jambo tunalofanya. Kwa hiyo, ikiwa unaisha maisha maradufu, anajua na hilo linamhuzunisha. Hata hivyo, “kwa sababu yeye [anakujali],” anatamani kukusaidia kurekebisha maisha yako.​—1 Petro 5:7.

     Kanuni ya Biblia: “Macho ya Yehova yanaenda huku na huku duniani kote ili adhihirishe nguvu zake kwa niaba ya wale ambao moyo wao ni kamili kumwelekea yeye.”​—2 Mambo ya Nyakati 16:9.