Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninaweza Kuchagua Jinsi Gani Mtu Mzuri wa Kumwiga?

Ninaweza Kuchagua Jinsi Gani Mtu Mzuri wa Kumwiga?

 “Jambo lililonisaidia nilipokabili matatizo shuleni, lilikuwa kufikiria mtu fulani niliyemheshimu sana ambaye alikabiliana na matatizo kama hayo. Kisha nilijaribu kufuata mfano wa mtu huyo. Kuwa na mtu wa kumwiga hufanya iwe rahisi kukabiliana na hali ngumu.”​—Haley.

 Mtu wa kumwiga anaweza kukusaidia kuepuka matatizo na kufikia malengo yako. Siri ni kuchagua mtu mzuri wa kumwiga.

 Kwa nini uchague kwa uangalifu?

  •   Uchaguzi wako wa mtu wa kumwiga unaweza kuathiri matendo yako.

     Biblia inawaambia Wakristo wawakazie fikira wale ambao ni mfano wa kuigwa, inasema hivi: “Nanyi mnapotafakari matokeo ya mwenendo wao, igeni imani yao.”​—Waebrania 13:7.

     Dokezo: Kwa kuwa uchaguzi wako wa mtu wa kumwiga utakuathiri kwa njia nzuri au mbaya, chagua wale ambao kwa kweli wana sifa zinazofaa, si watu mashuhuri au wa umri wako tu.

     “Nimejifunza mambo mengi kutoka kwa Mkristo mwenzangu anayeitwa Adam, yaani, kupitia mtazamo na mwenendo wake kwa ujumla. Inastaajabisha kwamba bado ninakumbuka mambo hususa aliyosema na kufanya. Hata hajui kwamba alikuwa na uvutano mkubwa kwangu.”​—Colin.

  •   Uchaguzi wako wa mtu wa kumwiga unaweza kuathiri jinsi unavyofikiri na unavyohisi.

     Biblia inasema hivi: “Msipotoshwe. Kushirikiana na watu wabaya huharibu tabia nzuri.”​—1 Wakorintho 15:33.

     Dokezo: Chagua mtu mwenye sifa nzuri, usimchague kwa sababu ya mwonekano wake wa kuvutia. Ukichagua vibaya huenda ukavunjika moyo.

     “Ukijilinganisha na watu warembo sana, utajihisi mdogo sana na usiyevutia kabisa. Hilo linaweza kufanya uhangaikie mwonekano wako zaidi.”​—Tamara.

     Jambo la kufikiria: Ni madhara gani unayoweza kupata kwa kuchagua wanamuziki na wanamichezo maarufu wawe watu wako wa kuwaiga?

  •   Uchaguzi wako wa watu wa kuwaiga unaweza kuathiri uwezekano wa kukusaidia au kukuzuia kufikia malengo yako.

     Biblia inasema: “Anayetembea na wenye hekima atakuwa na hekima.”​—Methali 13:20.

     Dokezo: Chagua mtu wa kumwiga ambaye matendo yake yanaonyesha sifa nzuri unazotaka kuzionyesha. Unapochunguza sifa hizo, unaweza kujifunza hatua hususa unazoweza kuchukua ili ufanikishe malengo yako.

     “Panga malengo yenye uhakika badala ya kusema ‘Ninataka kuchukua mambo kwa uzito,’ unaweza kusema, ‘Ninataka kuchukua mambo kwa uzito kama Jane. Anafika kwa wakati na kuchukua migawo yake kwa uzito.’”​—Miriam.

     Jambo kuu: Unapochagua mtu mzuri wa kumwiga, unaamua utakuwa mtu wa aina gani.

Kumfuata mtu mzuri wa kumwiga kunaweza kuwa njia ya mkato ya kufanikisha malengo yako!

 Jinsi ya kuchagua

 Unaweza kuchagua mojawapo ya njia hizi mbili.

  1.   Unaweza kuchagua sifa unayotaka kuifanyia kazi na kisha utafute mtu unayemheshimu mwenye sifa hiyo.

  2.   Unaweza kuchagua mtu unayemheshimu na kisha uchague sifa aliyo nayo ambayo ungependa kuisitawisha.

 Daftari linaloambatanishwa na makala hii linaweza kukusaidia kufanya hivyo.

 Watu wa kuwaiga wanatia ndani:

  •  Vijana wenzako. “Ningependa kumwiga rafiki yangu mkubwa. Anawajali sana watu wengine licha ya kuwa na shughuli. Yeye ni mdogo kuliko mimi, lakini ninaona ana sifa nzuri sana ambazo mimi sina, na zinanifanya nitake kufuata mfano wake.”​—Miriam.

  •  Watu wazima. Hao wanaweza kuwa wazazi wako au waabudu wenzako. “Pasipo na shaka, wazazi wangu ndio watu ninaotaka kuwaiga. Wana sifa nzuri sana. Ninaona makosa yao, lakini ninawaona wakiendelea kuwa waaminifu licha ya udhaifu wao. Nitakapokuwa na umri kama wao, ninatumaini wengine watasema hivyo kunihusu.”​—Annette.

  •  Wahusika katika Biblia. “Nimechagua watu kadhaa katika Biblia ambao ninataka kuwaiga, yaani, Timotheo, Ruthu, Ayubu, Petro, na msichana mdogo Mwisraeli, na kila mmoja nimemchagua kwa sababu fulani. Kadiri ninavyojifunza kuhusu wahusika katika Biblia ndivyo wanavyokuwa halisi zaidi kwangu. Nimefurahia sana kujifunza masimulizi katika kitabu Igeni Imani Yao, pamoja na sehemu yenye kichwa ‘Mfano wa Kuigwa’ inayopatikana katika mabuku yote mawili ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza​—Majibu Yafanyayo Kazi.”​—Melinda.

 Dokezo: Usiwe na mtu mmoja tu wa kumwiga. Mtume Paulo aliwaambia hivi Wakristo wenzake: “Mwendelee kuwaangalia wale wanaotembea katika njia inayopatana na mfano tuliowawekea.”​—Wafilipi 3:​17.

 Je, ulijua? Unaweza kuwa mfano wa kuigwa na watu wengine! Biblia inasema hivi: “Uwe mfano mzuri kwa waaminifu katika kusema, katika mwenendo, katika upendo, katika imani, na katika usafi wa kiadili.”​—1 Timotheo 4:​12.

 “Unaweza kuwa unajitahidi kufanyia kazi sifa fulani na wakati huohuo ukawasaidia wengine wawe na sifa nzuri. Huwezi kujua ni nani anayekutazama wala huwezi kujua jinsi mambo unayosema yanavyoweza kubadili maisha ya mtu mwingine.”​—Kiana.