Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninawezaje Kudhibiti Hasira Yangu?

Ninawezaje Kudhibiti Hasira Yangu?

 Maswali

  •  Unakasirika mara nyingi kadiri gani?

    •  mara chache sana

    •  pindi fulani

    •  kila siku

  •  Hasira yako ni kali kadiri gani?

    •  kiasi

    •  kali

    •  kali sana

  •  Ni nani ambaye mara nyingi hukukasirisha?

    •  mzazi

    •  mdogo wako

    •  rafiki

 Ikiwa unaona unahitaji kudhibiti hasira yako, makala hii itakusaidia! Kwanza, fikiria baadhi ya sababu za kubaki ukiwa mtulivu unapochokozeka.

 Kwa nini ni muhimu

 Afya yako. Methali 14:30 inasema hivi: “Moyo mtulivu ni uzima wa mwili wenye nyama.” Kinyume na hilo, gazeti la Journal of Medicine and Life linasema kwamba “hasira inaweza kuathiri moja kwa moja magonjwa ya moyo.”

 Rafiki zako. Biblia inasema hivi: “Usishirikiane na mtu yeyote mwenye mazoea ya kukasirika; wala usiende pamoja na mtu wa mifoko ya ghadhabu.” (Methali 22:24) Hivyo, ikiwa una tatizo la kudhibiti hasira yako, usishangae watu wakikuepuka. Mwanamke kijana anayeitwa Jasmine, anasema hivi: “Usipojifunza kudhibiti hasira yako, hutakuwa na marafiki.”

 Sifa yako. Ethan, mwenye umri wa miaka 17, anasema hivi: “Usipodhibiti hasira yako, wengine watatambua hilo na watakuwa na maoni yasiyofaa kukuelekea.” Jiulize hivi, ‘Ningependa watu wanioneje​—nikiwa mtu wa kufanya amani kwa utulivu au mtu anayelipuka kwa hasira wakati wowote?’ Biblia inasema hivi: “Yule ambaye si mwepesi wa hasira ana utambuzi mwingi, lakini anayekosa subira anainua upumbavu.”​—Methali 14:29.

Hakuna mtu anayependa kuwa karibu na mtu mwenye milipuko ya hasira

 Unachoweza kufanya

 Fikiria maandiko na maelezo yafuatayo, kisha ujiulize maswali yanayofuata.

  •   Methali 29:22: “Mtu mwenye hasira huchochea ugomvi, na mtu yeyote mwenye mwelekeo wa ghadhabu ana makosa mengi.”

     “Ilikuwa vigumu sana kwangu kudhibiti hasira nilipokuwa tineja. Watu wa ukoo wa upande wa baba wana tatizo hilohilo. Sisi huuita udhaifu wa kuzaliwa. Ni vigumu sana kwetu kudhibiti hasira!”​—Kerri.

     Je, mimi ni mwenye hasira? Ikiwa ninakubali kuwa nimesitawisha sifa nzuri, je, inapatana na akili kutetea kwamba kushindwa kudhibiti hasira ni udhaifu wa kuzaliwa?

  •   Methali 15:1: “Jibu, linapokuwa la upole, hugeuza ghadhabu, lakini neno linaloumiza hufanya hasira ipande.”

     “Siri ni kujifunza kudhibiti hisia zako. Ukisitawisha sifa ya upole na kuzingatia sifa nzuri, kudhibiti hasira hakutakuwa tatizo tena.”​—Daryl.

     Kwa nini ni muhimu kuzingatia ninavyoitikia ninapochokozeka?

  •   Methali 26:20: “Pasipo na kuni moto huzimika.”

     “Kwa kawaida ninapoitikia kwa fadhili, hilo humtuliza mtu yule mwingine na tunaweza kuwasiliana kwa utulivu.”​—Jasmine.

     Maneno au matendo yangu yanawezaje kuongezea kuni kwenye moto?

  •   Methali 22:3: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha, lakini wasio na uzoefu wameendelea mbele nao lazima waumie.”

     “Wakati mwingine ninahitaji tu kuondoka mahali hapo ili nipate muda wa kufikiria kilichotukia, kisha ninaweza kushughulika na jambo hilo baada ya kutulia.”​—Gary.

     Ni wakati gani unaofaa kuondoka mahali mlipo bila kumfanya mwenzako ahisi kana kwamba unampuuza?

  •   Yakobo 3:2: “Kwa maana sisi sote hujikwaa mara nyingi.”

     “Tunapaswa kujutia makosa yetu, hata hivyo, tunapaswa kujifunza kutokana nayo pia. Tunapaswa kuinuka tena tunapojikwaa na kuazimia kushughulikia hali vizuri zaidi wakati ujao.”​—Kerri.

 Dokezo: Jiwekee lengo. Azimia kubaki ukiwa mtulivu kwa kipindi fulani cha wakati​—labda kwa mwezi mmoja. Weka rekodi ya maendeleo unayofanya.