Hamia kwenye habari

Nifanye Nini Ikiwa Wazazi Wangu Wanataka Kutalikiana?

Nifanye Nini Ikiwa Wazazi Wangu Wanataka Kutalikiana?

Unachoweza kufanya

 Zungumza kuhusu mambo yanayokuhangaisha. Waeleze wazazi wako jinsi ulivyo na huzuni au jinsi ulivyovurugika. Huenda watakuambia kinachoendelea na kukupunguzia mahangaiko yako.

 Ikiwa wazazi wako hawawezi kukutegemeza kwa sasa, unaweza kuzungumza na rafiki mkomavu.—Methali 17:17.

 Zaidi ya yote, Baba yako wa mbinguni, “msikiaji wa sala” anaweza kukusikiliza. (Zaburi 65:2) Mfungulie moyo wako ‘kwa sababu anakujali.’—1 Petro 5:7.

Mambo ya kuepuka

Kupona kutokana na matokeo ya talaka ya wazazi wako ni kama kupona mkono uliovunjika—unakuwa na maumivu, hata hivyo, hatimaye utapona

 Usiwe na kinyongo. “Wazazi wangu walikuwa na ubinafsi,” anasema Daniel, ambaye wazazi wake walitalikiana alipokuwa na umri wa miaka saba. “Hawakutufikiria wala kufikiria hatua waliyochukua ingekuwa na matokeo gani kwetu.”

 Ni madhara gani ambayo yangeweza kutokea ikiwa Daniel angeamua kuweka kinyongo na kukasirika daima?—Dokezo: Soma Methali 29:22.

 Kwa nini ingefaa Daniel ajaribu kuwasamehe wazazi wake kwa sababu ya uchungu ambao wamemsababishia?—Dokezo: Soma Waefeso 4:31, 32.

 Epuka mazoea yanayoweza kukudhuru. “Sikuwa na furaha, nami nilikuwa nimeshuka moyo wazazi wangu walipotalikiana,” anakumbuka Denny. “Nilianza kupata matatizo shuleni nami nikaanguka mitihani mwaka mmoja. Kisha ... nikawa mtukutu darasani na kuanza kupigana-pigana.”

 Unafikiri, Denny alikuwa akijaribu kutimiza nini kwa kuwa mtukutu darasani, au kupigana-pigana?

 Kanuni ya Wagalatia 6:7 inaweza kuwasaidiaje watu kama vile Denny kuepuka mazoea yenye kudhuru?

 Majeraha ya kihisia yanaweza kuchukua muda mrefu kabla ya kupona. Kadiri maisha yako yanavyorudia hali ya kawaida, ndivyo utakavyoanza kutulia tena.