Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Kwa Nini Niombe Msamaha?

Kwa Nini Niombe Msamaha?

 Ungefanya nini ikiwa ungekabili hali zifuatazo?

  1.   Mwalimu anakukemea kwa sababu ya kusumbua darasani.

     Je, umwombe mwalimu msamaha—hata ikiwa unafikiri amekukemea kupita kiasi?

  2.   Rafiki yako anagundua kwamba umesema mambo mabaya kumhusu.

     Je, umwombe msamaha rafiki yako—hata ikiwa unafikiri jambo ulilosema lilikuwa sahihi?

  3.   Baba yako anakukasirisha kwa hiyo unazungumza naye kwa njia isiyo na heshima.

     Je, umwombe baba yako msamaha—hata ikiwa unafikiri yeye ndiye aliyekuwa na makosa?

 Jibu la maswali yote matatu ni ndiyo. Lakini kwa nini uombe msamaha, hata ikiwa unahisi kwamba ulikuwa na sababu nzuri ya kufanya ulichofanya?

 Kwa nini uombe msamaha?

  •   Kuomba msamaha ni ishara ya ukomavu. Unapokubali makosa yako, unaonyesha kwamba unasitawisha sifa muhimu utakazohitaji utakapokuwa mtu mzima.

     “Kuwa na unyenyekevu na subira kunaweza kutusaidia kuomba msamaha na kumsikiliza yule mtu mwingine.”—Rachel.

  •   Kuomba msamaha kunakuwezesha kufanya amani. Watu wanaoomba msamaha wanaonyesha kwamba wanahangaikia kufanya amani kuliko kuthibitisha kwamba hawajafanya makosa au kuonyesha yule mtu mwingine ndiye aliyekosea.

     “Hata ikiwa unahisi hujakosea, lengo linapaswa kuwa kufanya amani. Kusema ‘naomba msamaha’ hakugharimu chochote, lakini kunaweza kukusaidia udumishe urafiki wenu.”—Miriam.

  •   Kuomba msamaha kunakufanya ujihisi vizuri. Hisia unazopata unapomuumiza mtu mwingine zinaweza kuwa mzigo wenye kulemea. Lakini unapoomba msamaha, mzigo huo unakuondokea. a

     “Kuna nyakati ambazo nilizungumza kwa hasira na baba na mama. Nilijihisi vibaya, lakini ilikuwa vigumu kwangu kuomba msamaha. Hata hivyo, sikuzote nilipoomba msamaha nilijihisi vizuri kwa sababu hilo lilisaidia familia yetu kuwa na amani tena.”—Nia.

    Hisia unazopata unapomuumiza mtu zinaweza kuwa mzigo wenye kulemea; unapoomba msamaha, mzigo huo unakuondokea

 Je, kuomba msamaha kunahitaji jitihada? Ndiyo! Dena, msichana ambaye amehitaji kuomba msamaha mara nyingi kwa sababu ya kumtendea mama yake kwa njia isiyo na heshima, anasema hivi: “Si rahisi kusema, ‘naomba msamaha.’ Unahisi ni kana kwamba kuna kitu kimekwama kooni na maneno hayawezi kutoka!”

 Jinsi ya kuomba msamaha

  •   Ikiwezekana, omba msamaha uso kwa uso. Kuomba msamaha ukiwa mbele ya yule uliyomkosea kunampa nafasi ya kuona kwamba kwa kweli unasikitishwa na kosa lako. Lakini ukiomba msamaha kupitia ujumbe wa simu, huenda asihisi kwamba ombi lako linatoka moyoni. Hata ujumbe wako ukiambatanishwa na picha ndogo yenye uso wa mtu aliyehuzunika (emoji), huenda usionekane kuwa wa kweli.

     Dokezo: Ikiwa huwezi kuomba msamaha uso kwa uso, jaribu kupiga simu au kuandika ujumbe kwenye kadi. Njia yoyote utakayoamua kutumia, chagua maneno yako vizuri.

     Kanuni ya Biblia: “Moyo wa mwadilifu hutafakari kabla ya kujibu.”—Methali 15:28.

  •   Omba msamaha haraka. Ukisubiri muda mrefu bila kuomba msamaha, huenda hali itazidi kuwa mbaya na uhusiano wako na mtu uliyemuumiza utazidi kuzorota.

     Dokezo: Jiwekee lengo—kwa mfano, ‘Leo nitaomba msamaha.’ Amua mapema utaomba msamaha wakati gani kisha ufanye hivyo.

     Kanuni ya Biblia: “Suluhisha mambo upesi.”—Mathayo 5:25.

  •   Omba msamaha kutoka moyoni. Kusema tu “samahani basi kama nilikukosea” si kuomba msamaha! Msichana anayeitwa Janelle anasema, “Yule uliyemkosea atakuheshimu ikiwa ataona unakubali kosa lako.”

     Dokezo: Usiweke masharti unapoomba msamaha. Kwa hiyo, usiseme, “Nitaomba msamaha kwa kosa langu ikiwa wewe pia utaomba msamaha.”

     Kanuni ya Biblia: “Tufuatilie mambo yanayoleta amani.”—Waroma 14:19.

a Ikiwa ulipoteza au kuharibu kitu cha mwenzako, ni jambo la hekima kulipa au kurekebisha kitu kilichoharibika.