Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninaweza Kuepukaje Uchovu wa Kupita Kiasi?

Ninaweza Kuepukaje Uchovu wa Kupita Kiasi?

 Je, unasumbuliwa na uchovu wa kupita kiasi? Ikiwa ndivyo, makala hii inaweza kukusaidia!

 Kwa nini unachoka kupita kiasi?

  •   Kulemewa na kazi. Mwanamke kijana anayeitwa Julie anasema hivi: “Katika kila shughuli maishani, tunaambiwa tufanye vizuri zaidi, tufanye maendeleo zaidi, tuwe na malengo ya juu na tupate mafanikio makubwa. Si rahisi kuishi chini ya mkazo huo!”

  •   Teknolojia. Tukiwa na simu za kisasa na vifaa vingine vya kielektroni, tunaweza kuwasiliana usiku na mchana, kwa kweli jambo hilo linaweza kutupa mkazo na baada ya muda, huenda tukachoka kupita kiasi.

  •   Kutolala vya kutosha. Mwanamke kijana anayeitwa Miranda anasema hivi: “Shule, kazi, na burudani hufanya vijana wengi waamke mapema sana na wachelewe kulala na wanafanya hivyo karibu kila wakati.” Mara nyingi hali hiyo huchosha sana.

 Kwa nini ni jambo zito?

 Biblia inasifu kufanya kazi kwa bidii. (Methali 6:​6-8; Waroma 12:11) Lakini haipendekezi tufanye kazi kiasi kwamba kila kitu maishani mwetu kinaathirika kutia ndani afya yetu.

 “Wakati fulani, niligundua kwamba sikuwa nimekula kwa siku nzima kwa sababu nilikuwa nikikazia fikira kutimiza majukumu mengi niliyokuwa nayo. Nilijifunza kwamba si vizuri kukubali kila jukumu ninalopata, yaani, kuwa na majukumu mengi mpaka ninaathiri afya.”​—Ashley.

 Biblia ina sababu nzuri ya kusema hivi: “Mbwa aliye hai ni afadhali kuliko simba aliyekufa.” (Mhubiri 9:4) Kufanya mambo mengi kupita kiasi kunaweza kufanya ufikiri una nguvu kama za simba kwa muda fulani. Lakini kujichosha kwa njia hiyo kunaweza kuwa na madhara makubwa kwa afya yako.

 Unaweza kufanya nini?

  •   Jifunze kukataa kazi. Biblia inasema hivi: “Wenye kiasi wana hekima.” (Methali 11:2) Watu wenye kiasi hujua mipaka yao na hawakubali kazi nyingi zaidi ya uwezo wao.

     “Waathiriwa wakuu wa kuchoka kupita kiasi ni wale wasioweza kukataa kazi, wale wanaojaribu kufanya kila kazi wanayopewa. Mtu mwenye kiasi hafanyi hivyo. Ikiwa mtu atafanya hivyo, baada ya muda atachoka kupita kiasi.”​—Jordan.

  •   Uwe na wakati wa kutosha wa kupumzika. Biblia inasema hivi: “Ni afadhali konzi moja ya pumziko kuliko konzi mbili za kazi ngumu na kukimbiza upepo.” (Mhubiri 4:6) Usingizi umekuwa ukiitwa “chakula cha ubongo,” lakini matineja wengi hawalali kwa saa nane hadi kumi kama inavyohitajiwa.

     “Ratiba yangu ilipokuwa na mambo mengi kupita kiasi, sikuwa na wakati wa kutosha wa kulala. Lakini wakati mwingine saa hizo za ziada za kulala ndizo ninazohitaji ili kuongeza ubora wa shughuli yangu na kuwa na furaha siku inayofuata.”​—Brooklyn.

  •   Panga mambo vizuri. Biblia inasema hivi: “Mipango ya wenye bidii hakika huleta mafanikio.” (Methali 21:5) Kujifunza kupanga vizuri muda na utendaji wako ni ujuzi utakaokusaidia katika maisha yako yote.

     “Mikazo mingi inaweza kuepukwa kwa kuandika ratiba. Ukiandika ratiba yako, ni rahisi kugundua mahali unapohitaji kufanya marekebisho ili kuepuka kuchoka kupita kiasi.”​—Vanessa.