Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Nitawaelezaje Wengine Msimamo Wangu Kuhusu Ngono?

Nitawaelezaje Wengine Msimamo Wangu Kuhusu Ngono?

“Eti nini​—wewe bado ni bikira?”

Ikiwa ungependa kumjibu mtu anayeuliza swali hilo kwa kumwambia ndiyo, mimi ni bikira, utamwambiaje hivyo kwa ujasiri? Makala hii itakusaidia!

 Bikira ni nani?

 Bikira ni mtu yeyote ambaye hajawahi kufanya ngono.

 Hata hivyo matendo ya ngono yanahusisha mambo kadhaa. Huenda wengine wakasema kwamba wao ni “mabikira” kwa sababu hawajahi kulala na mwanamume au mwanamke kwa njia ya asili kama Mungu alivyokusudia.

 Hata hivyo, neno “ngono” linatia ndani mambo kama vile kumpiga punyeto mtu mwingine, ngono ya mdomo, au ngono ya mkundu.

 Jambo kuu: Watu ambao wamewahi kufanya ngono​—ngono ya mdomo, ngono ya mkundu, au kumpiga punyeto mtu mwingine​—hawawezi kusema kwamba wao ni mabikira.

 Biblia husema nini kuhusu ngono?

 Biblia husema waziwazi kwamba ngono inapaswa kufanywa tu na mwanamume na mwanamke ambao wamefunga ndoa. (Methali 5:​18) Kwa hiyo, mtu yeyote ambaye angependa kumpendeza Mungu hapaswi kufanya ngono hadi atakapofunga ndoa.​—1 Wathesalonike 4:​3-5.

 Wengine wanasema kwamba mambo ambayo Biblia inasema yamepitwa na wakati na si muhimu katika ulimwengu wetu huu wa kisasa. Lakini kumbuka kwamba, ulimwengu huuhuu umejaa visa vingi sana vya talaka, mimba zisizotakiwa, na magonjwa ya zinaa. Kwa kweli mambo hayo yanaonyesha kwamba hatuwezi kamwe kujifunza maadili bora kutoka katika ulimwengu huu!​—1 Yohana 2:​15-​17.

 Unapochunguza kwa makini, bila shaka utatambua kwamba mambo ambayo Biblia inasema kuhusu maadili bora, yanapatana na akili. Kwa mfano: Tuseme mtu fulani angekupa dola 1,000 za Marekani. Je, ungepanda hadi juu kwenye paa ya nyumba yako na kisha kuanza kuzitupa chini pesa hizo ili mtu yeyote yule azichukue?

 Uamuzi unaokabili kuhusu kufanya ngono unafanana na hali hiyo. “Singependa kupoteza ubikira wangu kwa mtu ambaye hata jina lake huenda nisilikumbuke miaka mingi ijayo,” anasema msichana mwenye umri wa miaka 14 anayeitwa Sierra. Tammy, msichana mwenye umri wa miaka 17 anakubaliana na jambo hilo anaposema: “Ngono ni zawadi ya pekee sana ambayo mtu hapaswi kuichukulia kivivihivi.”

 Jambo kuu: Kiwango cha Biblia kwa wale ambao hawajafunga ndoa ni kudumisha ubikira na mwenendo safi.​—1 Wakorintho 6:​18; 7:​8, 9.

 Wewe binafsi una maoni gani kuhusu ngono?

  •   Je, unaamini kwamba maoni ya Biblia kuhusu ngono yanafaa au yanatubana sana?

  •   Je, unaamini kwamba ni sawa kwa watu wawili ambao hawajafunga ndoa kufanya ngono maadamu wanapendana sana?

 Baada ya kuchunguza jambo hilo kwa uangalifu, vijana wengi wamefikia mkataa kwamba ni jambo bora kudumisha ubikira wao na kuwa na mwenendo safi. Hawajutii kamwe uamuzi huo wala hawahisi kwamba wamekosa au kunyimwa chochote. Ona kile ambacho baadhi yao walisema:

  •  “Nafurahi sana kwamba mimi ni bikira! Hakuna tatizo lolote kuepuka maumivu ya kiakili, kimwili, na ya kihisia ambayo husababishwa na kufanya ngono kabla ya kufunga ndoa.”​—Emily.

  •  “Ninafurahi kwamba sina msururu wa mahusiano yaliyovunjika ya kimahaba, na ninajihisi vizuri kwamba sina magonjwa yanayoambukizwa kwa kufanya ngono na mtu mwingine.”​—Elaine.

  •  “Nimewahi kuwasikia wasichana wengine wa umri wangu na hata wale walionizidi kwa umri wakisema kwamba wanajuta kwamba walifanya ngono na kwamba angalau wangesubiri, nami singependa kamwe kufanya kosa kama hilo.”​—Vera.

  •  “Nimejionea watu wengi wakiendelea kubeba makovu na mizigo mizito ya kihisia kwa sababu ya kupoteza ubikira wao au kwa sababu ya kuwa na wapenzi kadhaa. Kwa maoni yangu, hayo ni maisha yenye kuhuzunisha kama nini.”​—Deanne.

 Jambo kuu: Unapaswa kujua msimamo wako kabla ya kushinikizwa au kushawishiwa na wengine ufanye ngono.​—Yakobo 1:​14, 15.

 Utawaelezaje wengine msimamo wako kuhusu ngono?

 Unapaswa kumjibuje mtu anayetaka kujua maoni au msimamo wako kuhusu ngono? Itategemea jinsi hali ilivyo.

 “Ikiwa kusudi la mtu lilikuwa kunifanyia mzaha, nisingeendelea kuyasikiliza maneno ya mtu huyo. Badala yake ningemwambia mtu huyo, ‘Jambo hilo halikuhusu hata kidogo,’ kisha ningeondoka.”​—Corinne.

 “Kwa kusikitisha, wanafunzi wengine shuleni wanafurahia sana kuwanyanyasa wengine. Siwaelezi wanafunzi kama hao msimamo wangu punde ninapotambua nia yao ya kuniuliza swali hilo.”​—David.

 Je, wajua? Nyakati nyingine, Yesu ‘hakuwajibu’ wadhihaki.​—Mathayo 26:62, 63.

 Lakini namna gani ikiwa mtu anayekuuliza anataka kwa unyoofu kufahamu msimamo wako? Ikiwa unaona kwamba huenda mtu huyo akaheshimu Biblia, basi unaweza kumsomea na kumfafanulia andiko la 1 Wakorintho 6:​18, ambalo linaonyesha kwamba mtu anayefanya ngono kabla ya kufunga ndoa anautendea dhambi, au kuudhuru, mwili wake mwenyewe.

 Iwe utamjibu mtu huyo moja kwa moja kwa kutumia Biblia au la, ni muhimu sana kwamba uzungumze kwa usadikisho. Kumbuka kwamba una kila sababu ya kujivunia uamuzi wako wa kuendelea kubaki safi kiadili.​—1 Petro 3:​16.

 “Unapojibu kwa usadikisho, hilo linaonyesha kwamba wewe mwenyewe unaamini kabisa mambo unayoamini na kwamba unafanya mambo hayo kwa sababu ni sahihi kuyafanya na si tu kwa sababu uliambiwa na mtu fulani uyafanye.”​—Jill.

 Jambo kuu: Ikiwa unasadiki kabisa kwamba msimamo wako kuhusu ngono ni sahihi, itakuwa rahisi kwako kuwaeleza wengine. Na huenda ukashangazwa na jinsi wengine watavyoitikia. “Wafanyakazi wenzangu wamenipongeza kwa sababu ya kuendelea kuwa bikira,” anasema Melinda mwenye umri wa miaka 21. “Hawalioni kuwa jambo la ajabu. Wanaona jambo hilo kuwa ishara ya kwamba nina sifa ya kujizuia na tabia njema.”

 Dokezo! Ikiwa unahitaji msaada wa kujua jinsi ya kumfafanulia mtu msimamo wako kuhusu ngono, pakua daftari yenye kichwa “Jinsi ya Kuwaeleza Wengine Msimamo Wako Kuhusu Ngono.” Pia, tazama kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza​—Majibu Yafanyayo Kazi.

 “Napenda sana maelezo yaliyo katika mabuku yote mawili ya kitabu ‘Vijana Huuliza.’ Kwa mfano, ukurasa wa 187 katika Buku la 1 unaonyesha jinsi kufanya ngono kabla ya kufunga ndoa ni kama kumpa mtu mkufu wa bei ghali bila kumtoza malipo yoyote. Unajishushia heshima. Ukurasa wa 177 unaonyesha kwamba kufanya ngono kabla ya kufunga ndoa ni kama kuchukua mchoro mzuri na kuutumia kama mkeka wa mlangoni. Lakini mfano ninaoupenda sana ni ule unaopatikana kwenye ukurasa wa 54 katika Buku la 2. Kuna picha yenye maelezo yanayosema: ‘Kufanya ngono kabla ya ndoa ni kama kufungua zawadi kabla ya kukabidhiwa.’ Ni kama kuiba kitu cha mtu mwingine, yaani, yule utakayefunga naye ndoa wakati ujao.”​—Victoria.