Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Nitahitaji Kufanya Nini Baada ya Ubatizo?​—Sehemu ya 2: Dumisha Utimilifu Wako

Nitahitaji Kufanya Nini Baada ya Ubatizo?​—Sehemu ya 2: Dumisha Utimilifu Wako

 Biblia inasema kwamba “Yehova hatawanyima jambo lolote jema wale wanaotembea kwa utimilifu.” (Zaburi 84:11) “Kutembea kwa utimilifu” kunamaanisha nini? Kunamaanisha kuishi katika njia ambayo inaonyesha unatimiza ahadi uliyompa Yehova ulipojiweka wakfu kwake. (Mhubiri 5:4, 5) Unawezaje kutembea kwa utimilifu baada ya ubatizo?

Katika makala hii

 Endelea kuvumilia matatizo

 Andiko la msingi: “Ni lazima tuingie katika Ufalme wa Mungu kupitia dhiki nyingi.”​—Matendo 14:22.

 Maana yake: Ni wazi kwamba Wakristo wote watakabili matatizo maishani mwao. Baadhi ya matatizo ambayo utakabili kama vile dhihaka na upinzani yatakupata hasa kwa sababu wewe ni Mkristo. Matatizo mengine kama vile ya kiuchumi au magonjwa yanawapata wanadamu wote.

 Mambo ya kutarajia: Nyakati nyingine utakabili mabadiliko maishani na huenda hali zikawa ngumu. Biblia inasema kwamba mambo mabaya yanaweza kumpata mtu yeyote, awe Mkristo au la.​—Mhubiri 9:11.

 Mambo unayoweza kufanya: Kwa kuwa unajua kwamba utakabili changamoto, unaweza kujitayarisha kukabiliana nazo. Zione changamoto kama fursa ya kuimarisha imani yako na kumtegemea Yehova zaidi. (Yakobo 1:2, 3) Baada ya muda, utahisi kama alivyohisi Mtume Paulo aliposema: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yule anayenipa nguvu.”​—Wafilipi 4:13.

 SIMULIZI HALISI. “Muda mfupi baada ya mimi kubatizwa, ndugu zangu waliacha kweli, wazazi wangu wakawa wagonjwa, kisha mimi pia nikawa mgonjwa. Ingekuwa rahisi kwangu kukata tamaa na kusahau kwamba nilipojiweka wakfu kwa Mungu, niliahidi kwamba ibada yake ingekuwa muhimu zaidi maishani mwangu. Hata hivyo, kukumbuka kwamba nimejiweka wakfu kulinisaidia kukabiliana na changamoto hizo.”​—Karen.

 Dokezo: Jifunze kumhusu Yosefu. Unaweza kusoma simulizi la maisha yake kwenye Mwanzo sura ya 37 na 39 hadi ya 41. Fikiria: Alikabiliana na matatizo gani ambayo hakutarajia, na alitendaje? Yehova alimsaidiaje Yosefu?

 Je, unahitaji msaada zaidi?

 Endelea kupinga vishawishi

 Andiko la msingi: “Kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe.”​—Yakobo 1:14.

 Maana yake: Nyakati nyingine sote tunashawishiwa na tamaa zisizofaa ambazo tusipozipinga zinaweza kutuongoza kufanya mambo mabaya.

 Mambo ya kutarajia: Baada ya kubatizwa, bado utakuwa na “tamaa za mwili.” (2 Petro 2:18) Huenda ukapatwa na tamaa ya kufanya ngono kabla ya kufunga ndoa.

 Mambo unayoweza kufanya: Fanya uamuzi wako sasa kabla ya kukabili kishawishi ili tamaa zako zisikuongoze kufanya uamuzi mbaya. Kumbuka Yesu alisema: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili.” (Mathayo 6:24) Unaweza kuchagua bwana wako atakuwa nani. Mchague Yehova. Hata tamaa mbaya iwe na nguvu kadiri gani, unaweza kuepuka kutenda kupatana nayo.​—Wagalatia 5:16.

 Dokezo: Jichunguze ili utambue uwezo wako na udhaifu wako. Chagua marafiki ambao wanakusaidia kuonyesha sifa nzuri. Epuka watu, mahali, na hali zinazofanya iwe vigumu kwako kufanya kilicho sawa.​—Zaburi 26:4, 5.

 Je, unahitaji msaada zaidi?

 Endelea kuongeza bidii yako

 Andiko la msingi: “Kila mmoja wenu awe na bidii ileile . . . mpaka mwisho, ili msiwe goigoi.”​—Waebrania 6:11, 12.

 Maana yake: Mtu ambaye hakazii fikira kazi yake anaweza kupunguza bidii na kuwa goigoi.

 Mambo ya kutarajia: Huenda baada ya kubatizwa ulikuwa na msisimko na bidii nyingi sana. Ulimpenda Yehova sana. Lakini baada ya muda, huenda ikawa vigumu kwako kuendelea kumtii Yehova katika kila jambo, na hilo linaweza kukuvunja moyo na kupunguza bidii yako.​—Wagalatia 5:7.

 Mambo unayoweza kufanya: Endelea kufanya lililo sawa hata ingawa pindi fulani unahisi kwamba hutaki kulifanya. (1 Wakorintho 9:27) Endelea kumkaribia Baba yako wa mbinguni kwa kujifunza kumhusu ili umfahamu vizuri na kwa kuzungumza naye mara nyingi katika sala. Pia endelea kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na wale wanaomtumikia Yehova.

 Dokezo: Kumbuka kwamba Yehova anakupenda sana na yuko tayari kukusaidia. Usifikie mkataa kwamba amekukasirikia ikiwa kwa muda mfupi umepunguza bidii yako. Biblia inasema: “Yeye humpa nguvu mtu aliyechoka na kuwapa uwezo kamili wale wasio na nguvu.” (Isaya 40:29) Atakubariki kwa kukusaidia kurudia tena bidii uliyokuwa nayo hapo awali.

 Je, unahitaji msaada zaidi?

 Jambo kuu: Ukitembea kwa utimilifu utafanya moyo wa Yehova ushangilie. (Methali 27:11) Atafurahi kwamba umechagua kuwa upande wake na atakupatia kila kitu unachohitaji ili kupinga mashambulizi ya Shetani.