Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ingawa vituo vya burudani huandika na kuonyesha habari za kuwasiliana na pepo na wahusika wake kwa njia inayovutia, tunahitaji kujua madhara yanayotokana na mambo hayo

HABARI KUU | NI NINI CHANZO CHA MAMBO YA UCHAWI?

Biblia Inafundisha Nini Kuhusu Kuwasiliana na Pepo?

Biblia Inafundisha Nini Kuhusu Kuwasiliana na Pepo?

INGAWA watu wengi hawana uhakika kuhusu mambo ya uchawi na kuwasiliana na pepo, wakifikiri kwamba hizo ni mbinu au ufundi wa waandaaji wa hati za filamu, Biblia ina maoni tofauti na hayo. Inaonya waziwazi kuhusu kuwasiliana na pepo. Kwa mfano, andiko la Kumbukumbu la Torati 18:10-13 linasema hivi: “Asipatikane ndani yako . . . yeyote anayefanya uaguzi, mwenye kufanya uchawi au yeyote anayetafuta ishara za bahati au mlozi, au anayefunga wengine kwa kuwatakia maovu au yeyote anayetafuta shauri kwa mwenye kuwasiliana na pepo au mjuzi wa kubashiri matukio au yeyote anayeuliza habari kutoka kwa wafu.” Kwa nini? Andiko hilo linaongezea hivi: “Kwa maana kila mtu anayefanya mambo hayo ni chukizo kwa Yehova . . . [Unapaswa kujionyesha] kuwa huna kosa kwa Yehova Mungu wako.”

Kwa nini Biblia inakataza kabisa kuwasiliana na pepo kwa njia yoyote ile?

CHANZO CHAKE NI KIBAYA

Biblia inatueleza kwamba miaka mingi kabla ya Mungu kuumba dunia, aliumba mamilioni ya viumbe wa kiroho au malaika. (Ayubu 38:4, 7; Ufunuo 5:11) Kila malaika alipewa uhuru wa kuchagua, yaani, uwezo wa kuamua kufanya mema au mabaya. Baadhi ya malaika waliamua kumwasi Mungu, wakaacha makao yao huko mbinguni na kuja kusababisha matatizo duniani. Matokeo ni kwamba, dunia “ikajaa jeuri.”—Mwanzo 6:2-5, 11; Yuda 6.

Biblia inasema kwamba malaika hao wana ushawishi mkubwa, na wanapotosha mamilioni ya watu. (Ufunuo 12:9) Hata wanaitumia vibaya tamaa ya asili ya wanadamu ya kutaka kujua kuhusu wakati ujao.—1 Samweli 28:5, 7; 1 Timotheo 4:1.

Ni kweli, huenda nguvu fulani za uchawi zikaonekana kuwa zinawasaidia watu. (2 Wakorintho 11:14) Lakini, ukweli ni kwamba, malaika hao waovu wanajaribu kupofusha akili za watu zisiangaziwe nuru ya kweli kumhusu Mungu.—2 Wakorintho 4:4.

Hivyo basi, kulingana na Biblia, kuwasiliana na pepo ni zoea lenye madhara. Ndio sababu wale ambao walikuja kuwa wanafunzi wa Yesu walipofundishwa ukweli kuhusu mambo hayo, “wale waliozoea kufanya ufundi wa uchawi wakaleta pamoja vitabu vyao wakaviteketeza,” ingawa hilo liliwaletea hasara kubwa ya kiuchumi.—Matendo 19:19.

“Huenda idadi ya wasichana wanaoamini uchawi imeongezeka kwa sababu ya wachawi wenye ushawishi ambao ni mashuhuri wanaoonyeshwa kwenye televisheni, filamu, na vitabu.”—Gallup Youth Survey, 2014

Vivyo hivyo, wengi leo wameamua kuacha mambo ya uchawi na burudani zinazohusiana na uwasiliani pepo. Kwa mfano, Maria * alipokuwa na umri wa miaka 12, alionekana kuwa na uwezo wa kutabiri kuhusu hatari au mambo ya wakati ujao. Alisoma kadi za kubashiri kwa ajili ya wanafunzi wenzake, na kwa kuwa utabiri wake ulitimia, alianza kujihusisha zaidi na mambo ya ushirikina.

Maria alifikiri kwamba hiyo ni zawadi kutoka kwa Mungu ili awasaidie watu. Alikiri hivi: “Lakini kuna jambo lililonihangaisha. Niliweza kusoma kadi kwa ajili watu wengine tu. Sikuweza kusoma kwa ajili yangu, ingawa nilitamani sana kujua kuhusu wakati wangu ujao.”

Akiwa na maswali mengi magumu, Maria alisali kwa Mungu na kisha baadaye alikutana na Mashahidi wa Yehova ambao walianza kujifunza Biblia pamoja naye. Maria alijifunza katika Biblia kwamba uwezo wake wa kutabiri kuhusu wakati ujao haukutoka kwa Mungu. Pia, alijifunza kwamba wote wanaotaka kuwa rafiki za Mungu wanapaswa kuondolea mbali vitu vyote vinavyohusiana na pepo. (1 Wakorintho 10:21) Matokeo yalikuwa nini? Maria alitupa vitabu na vitu vyake vya uchawi. Sasa anawahubiria wengine kuhusu kweli sahihi aliyojifunza katika Biblia.

Michael alipokuwa kijana, alipenda kusoma vitabu vya hadithi za kusisimua vyenye wahusika wanaofanya mambo ya uchawi. Alisema hivi: “Nilipenda kujilinganisha na watu maarufu wa rika langu ambao pia walipenda kujua mambo ya ulimwengu wa kuwaziwa.” Pole kwa pole, Michael alikuwa mraibu wa kusoma vitabu vya uchawi na ibada za Kishetani. Anakiri hivi: “Udadisi ulinifanya nipende kusoma vitabu na kutazama filamu kuhusu mambo hayo.”

Lakini kujifunza Biblia kulimchochea Michael kuchunguza kwa makini mambo aliyokuwa akisoma. Anaeleza hivi: “Niliandika orodha ya vitu vyote vyenye uhusiano na pepo na kuviondolea mbali. Nilijifunza somo muhimu sana. Katika 1 Wakorintho 10:31, Biblia inasema hivi: ‘Fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.’ Sasa swali ambalo huwa ninajiuliza ni, ‘je, kile ninachosoma kinamletea Mungu utukufu?’ Ikiwa hakimletei, basi ninakiepuka.”

Kwa kufaa Biblia inafafanuliwa kuwa kama taa. Ni chanzo cha nuru ya pekee inayoweza kutusaidia kuelewa maana halisi ya uchawi. (Zaburi 119:105) Biblia pia inaeleza mambo mengi zaidi. Inaeleza kuhusu ahadi ya wakati ujao ambapo tutaishi katika dunia isiyokuwa na uvutano wa roho waovu. Badiliko hilo litaathiri jamii ya wanadamu kwa kiwango kikubwa. Kwa mfano, Zaburi 37:10, 11 inasema hivi: “Na bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena; nawe hakika utapaangalia mahali pake, naye hatakuwapo. Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”

^ fu. 10 Majina katika makala hii yamebadilishwa.