Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Nifanye Nini Ikiwa Watu Wanaeneza Porojo Kunihusu?

Nifanye Nini Ikiwa Watu Wanaeneza Porojo Kunihusu?

 Kwa nini porojo inadhuru

 Porojo fulani hutolewa kwa nia mbaya—kwa mfano, mtu akisema uwongo kimakusudi ili akuchafulie jina. Hata ikiwa mtu anaeneza porojo ambayo haihusu jambo zito, porojo hiyo inaweza kumuumiza mwingine hisia​—hasa ikienezwa na mtu uliyemdhania kuwa rafiki yako wa karibu sana!​—Zaburi 55:12-​14.

 “Niligundua kwamba rafiki yangu alikuwa akieneza porojo kunihusu, akisema kwamba mimi siwajali wengine. Jambo hilo liliniumiza sana! Nilishindwa kuelewa kwa nini alisema jambo kama hilo.”​—Ashley.

 Ukweli wa Mambo: Iwe yule anayeeneza porojo kukuhusu ni rafiki yako au la, haipendezi hata kidogo unapojua kwamba watu wamekuwa wakisema mambo mabaya kukuhusu.

 Jambo baya ni kwamba​—huwezi kuzuia porojo

 Watu wanaweza kueneza porojo kwa sababu kadhaa, kutia ndani sababu hizi:

 Upendezi wa kweli. Wanadamu ni viumbe wanaopenda kuchangamana na wengine. Kwa hiyo ni jambo la kiasili kuzungumza kuhusu kitu au mtu fulani. Biblia yenyewe hututia moyo tuangalie “faida za kibinafsi” za wengine.​Wafilipi 2:4.

 “Kwa kawaida, kuzungumza kuhusu watu ndiyo mada inayosisimua zaidi!”​—Bianca.

 “Lazima nikiri kwamba ninapenda sana kujua mambo ambayo wengine wanafanya na kuzungumzia mambo hayo na watu wengine. Sijui ni kwa nini​—inasisimua tu.”​—Katie.

 Kukosa jambo la kufanya. Katika nyakati za Biblia, kulikuwa na watu ambao “hawakuwa wakitumia wakati wao wa starehe wakifanya chochote ila kuambiana jambo au kusikiliza jambo jipya.” (Matendo 17:21) Hivyo ndivyo ilivyo leo!

 “Hata wakati ambapo hakuna lolote la kuchangamsha, watu hubuni jambo fulani ili wawe na kitu cha kuzungumzia.”​—Joanna.

 Kutojiamini. Biblia ina sababu nzuri ya kutuonya dhidi ya mwelekeo wa kujilinganisha na wengine. (Wagalatia 6:4) Jambo la kusikitisha ni kwamba, watu wengine hukabiliana na tatizo la kutojiamini walilo nalo kwa kueneza habari mbaya kuwahusu wengine.

 “Mtu anayeeneza porojo hufunua jambo fulani kuhusu jinsi alivyo. Mara nyingi inafunua kwamba ana wivu na ndio maana anaeneza habari mbaya kuhusu mtu mwingine. Anaeneza porojo hiyo ili tu ajihisi vizuri na ajisadikishie mwenyewe kwamba yeye ni bora kuliko yule mwingine.”​—Phil.

 Ukweli wa mambo: Upende usipende, watu watazungumza kuhusu watu wengine​—kutia ndani wewe.

 Jambo zuri ni kwamba​—si lazima porojo ikudhoofishe hisia

 Huenda usifaulu kabisa kuwazuia watu kueneza porojo kukuhusu, hata hivyo unaweza kuchagua jinsi utakavyoitikia ukigundua kwamba mtu fulani ameeneza porojo kukuhusu. Ukigundua kwamba habari fulani kukuhusu imeenea, kuna angalau mambo mawili unayoweza kufanya.

 JAMBO LA 1: Puuza. Mara nyingi kupuuza jambo fulani ndio uamuzi bora kabisa​—hasa ikiwa habari zilizoenezwa ni za upuuzi. Fuata ushauri huu wa Biblia: “Usiwe na haraka kuudhika katika roho yako.”​—Mhubiri 7:9.

 “Habari zilienea kuwa nilikuwa nikimchumbia mvulana fulani​—mtu ambaye hata sikuwahi kukutana naye! Ulikuwa upuuzi mtupu na kwa hiyo niliamua kuupuza.”​—Elise.

 “Ukiwa na sifa nzuri ni rahisi kwako kukabiliana na porojo. Hata habari mbaya zikienezwa kukuhusu, ni watu wachache watakaoziamini, kwa sababu wanajua kwamba una sifa nzuri. Zitakusaidia uendelee kudumisha hadhi yako.”​—Allison.

 Dokezo: Andika (1) jambo ambalo lilienezwa kukuhusu na (2) jinsi ulivyohisi. ‘Ukishasema moyoni mwako,’ huenda ukatambua kwamba ni rahisi zaidi kuamua kulipuuza au kulisahau jambo hilo.​—Zaburi 4:4.

 JAMBO LA 2: Mfikie mtu aliyeanzisha porojo hiyo. Katika visa fulani huenda ukahisi kwamba habari mbaya sana kukuhusu imeenezwa hivi kwamba ukaamua kuchukua hatua ya kumfikia yule aliyeianzisha.

 “Unapowafikia watu wanaoeneza porojo kukuhusu, huenda ukawasaidia watambue kwamba hatimaye mambo wanayosema humfikia mtu wanayeeneza habari zake. Hilo huenda likakusaidia ujisafishie jina au hata kusuluhisha tatizo lenyewe.”​—Elise.

 Kabla ya kumfikia mtu anayeeneza porojo kukuhusu, fikiria kanuni zifuatazo za Biblia na ujiulize maswali yaliyoambatanishwa na kanuni hizo.

  •   “Yeyote anapojibu jambo kabla ya kulisikia, huo ni upumbavu na aibu kwake.” (Methali 18:13) ‘Je, nina habari zote zinazohusika? Je, inawezekana kwamba mtu aliyeniletea porojo hizo hakuelewa vizuri mambo aliyosikia?’

  •   ‘Uwe mwepesi wa kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.’ (Yakobo 1:​19) ‘Je, huu ndio wakati unaofaa wa kumfikia mtu anayeeneza porojo kunihusu? Je, nina uhakika kwamba ninatumia njia inayofaa kusuluhisha jambo hilo? Au ni afadhali zaidi nisubiri wakati fulani upite ili hisia zangu zitulie?’

  •   “Chochote ambacho mngetaka mtendewe na watu, ninyi nanyi watendeeni vivyo hivyo.” (Mathayo 7:​12, Holy Bible) ‘Ikiwa ningekuwa nimeeneza porojo kumhusu mtu mwingine, ningetaka mtu huyo anifikie kwa njia gani? Ningependa tuzungumzie tatizo hilo chini ya hali gani? Ningependa atumie maneno ya aina gani na azungumze kwa njia gani?’

 Dokezo: Kabla ya kumfikia yule anayeeneza porojo kukuhusu, andika mambo utakayomwambia. Kisha subiri juma moja au mawili, halafu urudie mambo uliyoandika uone kama kuna mabadiliko yoyote unayohitaji kufanya. Kisha zungumzia mambo hayo na mzazi wako au rafiki mkomavu na umwombe mashauri.

 Ukweli wa mambo: Kama ilivyo na mambo mengi maishani, huwezi kuwazuia watu wasieneze porojo. Lakini hilo halimaanishi kwamba ni lazima porojo ikudhibiti!