Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Je, Kweli Kutumia Lugha Chafu Ni Vibaya?

Je, Kweli Kutumia Lugha Chafu Ni Vibaya?

“Nimezoea kusikia maneno machafu hata sasa hayanishangazi tena. Ninayaona ya kawaida tu.”​—Christopher, 17.

“Nilipokuwa mdogo, nilitumia maneno machafu mara nyingi. Lilikuwa zoea rahisi sana kuanza lakini gumu sana kuacha.”​—Rebecca, 19.

 Maswali

  •   Wewe unahisije wengine wanapotumia lugha chafu?

    •  Hata huwa sitambui​—kwangu ni kawaida tu.

    •  Hunisumbua kwa kiasi fulani​—lakini nakubali tu.

    •  Huniudhi​—siwezi kuzoea.

  •   Wewe hutumia lugha chafu mara ngapi?

    •  Sijawahi

    •  Mara moja moja

    •  Mara nyingi

  •   Kwa maoni yako, kutumia lugha chafu ni jambo zito kadiri gani?

    •  Si zito sana

    •  Ni zito sana

 Kwa nini ni muhimu

 Je, wewe huona kutumia lugha chafu kuwa jambo zito? Labda unaweza kusema, ‘Si sana. Kuna matatizo makubwa zaidi ulimwenguni ya kutuhangaisha. Na zaidi ya hilo, kila mtu hutumia lugha chafu!’ Je, hilo ni kweli?

 Amini usiamini, kuna watu wanaojizuia kutumia lugha chafu. Na wanajua mambo fulani muhimu ambayo watu wengine hawajui. Kwa mfano:

  •  Kutumia lugha chafu si maneno matupu. Usemi wako hufunua jinsi ulivyo. Hivyo, kutumia lugha chafu kunaweza kufunua kwamba hujali hisia za watu wengine. Je, kweli wewe ni mtu wa aina hiyo?

     Biblia inasema hivi: “Mambo yanayotoka katika kinywa hutoka moyoni.”​—Mathayo 15:18.

    Kutumia lugha chafu ni uchafuzi wa mazungumzo. Kwa nini uwaathiri wengine​—au wewe mwenyewe​—kwa kuyatumia?

  •  Kutumia lugha chafu kunaweza kuwafanya watu wakawa na maoni mabaya kukuhusu. Kitabu Cuss Control kinasema hivi: “Jinsi tunavyozungumza kunaweza kuamua rafiki zetu watakuwa watu wa aina gani, kiasi cha heshima tutakachopata kutoka kwa watu wa familia yetu na wafanyakazi wenzetu, ubora wa mahusiano yetu pamoja na watu wengine, tutakuwa na uvutano mzuri kadiri gani, kama tutapata kazi au kupandishwa cheo, na jinsi watu wasiotujua watakavyotuona.” Pia kinasema hivi: “Jiulize ikiwa mahusiano yako pamoja na watu wengine huenda yangekuwa bora zaidi ikiwa hungetumia lugha chafu.”

     Biblia inasema hivi: ‘Matukano na yaondolewe mbali.’​—Waefeso 4:​31.

  •  Kutumia lugha chafu hakukufanyi uonekane wa kisasa. Katika kitabu chake kinachoitwa How Rude! Dakt. Alex Packer anaeleza hivi: “Kusikiliza watu wanaotumia lugha chafu kunachosha.” Anaongezea kusema kwamba msamiati uliojaa maneno machafu “hauwezi kumruhusu mtu ajieleze kwa utambuzi, hekima, ucheshi, au huruma. Ikiwa usemi wako ni wa kizembe, hauna kina au ubunifu, bila shaka akili yako itakuwa hivyo pia.”

     Biblia inasema hivi: “Neno lililooza na lisitoke kinywani mwenu.”​—Waefeso 4:​29.

 Jambo unaloweza kufanya

  •  Jiwekee lengo. Kwa nini usijaribu kuacha kutumia lugha chafu ndani ya mwezi mmoja au kwa muda mfupi zaidi? Unaweza kuweka rekodi ya maendeleo yako kwenye chati au kalenda. Hata hivyo, ili uimarishe azimio lako, unahitaji kuchukua hatua za ziada. Kwa mfano:

  •  Epuka burudani zinazojaza akili yako lugha chafu. Biblia inasema hivi: “Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” (1 Wakorintho 15:33) “Mashirika” hayatii ndani watu tu bali pia burudani​—sinema unazotazama, michezo ya video unayocheza, na muziki unaosikiliza. Kenneth, mwenye umri wa miaka 17, anasema hivi: “Ni rahisi kuimba maneno ya wimbo unaopenda na kupuuza kabisa kwamba una lugha chafu​—kwa sababu tu una mdundo mzuri.”

  •  Jiendeshe kama mtu mkomavu. Watu wengine hutumia lugha chafu kwa sababu wanafikiri hilo huwafanya waonekane kuwa watu wazima. Ukweli ni kwamba hilo huwafanya waonekane watoto. Biblia inasema watu wakomavu ni wale ambao “nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.” (Waebrania 5:​14) Hawashushi viwango vyao ili tu “wafurahishe” watu.

 Kwa kweli, lugha chafu huchafua akili (na hewa) kwa mawazo yasiyo safi. Tayari ulimwengu umeshajaa uchafu! Kitabu Cuss Control kinapendekeza hivi: “Usiongeze uchafu zaidi. Fanya sehemu yako kwa kusafisha namna ya mazungumzo. Utahisi vizuri kujielekea, na watu wengine watahisi vizuri kukuhusu pia.”