Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Kutuma Ujumbe Mchafu?

Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Kutuma Ujumbe Mchafu?

 Ujumbe mchafu unatia ndani nini?

 Kutuma ujumbe mchafu, katika Kiingereza “Sexting,” kunatia ndani kutuma ujumbe wa maneno, picha, na video za ngono kupitia simu ya mkononi. Mtu mmoja alisema hivi: “Siku hizi imekuwa kawaida kuwasiliana kwa njia hiyo. Mwanzoni mnatumiana ujumbe wa kawaida lakini baada ya muda mnaanza kutumiana picha zinazochochea hamu ya ngono.”

 Kwa nini watu hufanya hivyo? Wakili mmoja mwenye uzoefu aliripotiwa katika gazeti The New York Times akisema kuwa vijana fulani hufikiri kwamba “kuwa na picha ya mpenzi wako akiwa uchi kwenye simu huwaonyesha wengine kuwa unafanya ngono.” Kijana mmoja hata alisema kwamba hiyo ni njia ya “kufanya ngono isiyo na madhara kwa kuwa huwezi kupata mimba au magonjwa ya zinaa.”

 Zifuatazo ni sababu nyingine zinazowafanya vijana watume ujumbe mchafu:

  •   Ili kumchezea kimapenzi mtu ambaye wangependa kuanzisha uhusiano pamoja naye.

  •   Kwa sababu wametumiwa picha na mtu mwingine akiwa uchi wanahisi wanashinikizwa kufanya hivyo pia.

 Kuna madhara gani mtu anapotuma ujumbe mchafu?

 Mara tu unapotuma picha kupitia simu, huna uwezo wa kudhibiti jinsi itakavyotumiwa​—au jinsi itakavyoathiri sifa yako. Amanda Lenhart, mtaalamu wa utafiti na mwandishi katika Kituo cha Utafiti cha Pew, aliandika hivi katika ripoti yake kuhusu kutuma ujumbe mchafu: “Siku hizi imekuwa rahisi sana kwa watu kutuma na kuhifadhi uthibitisho wa mwenendo usiofaa.”

 Katika visa fulani

  •    Mtu aliyetumiwa picha ya rafiki yake akiwa uchi amezisambaza kwa marafiki wake ili kuwafurahisha.

  •    Wavulana wametuma picha za msichana akiwa uchi ili kulipiza kisasi kwa sababu ya uhusiano wao kuvunjika.

 JE, WAJUA? Katika visa vingi, kutuma picha za kijana akiwa uchi kumeonwa kuwa sawa na kumtendea mtoto vibaya kingono au kusambaza ponografia ya watoto. Vijana fulani ambao hawajatimia umri wa miaka 18 wamehukumiwa kwa uhalifu wa ngono.

 Biblia inasema nini?

 Biblia haiwakatazi watu kufurahia ngono ndani ya ndoa. (Methali 5:18) Hata hivyo, inasema mambo waziwazi kuhusu matendo ya ngono kati ya watu ambao hawajafunga ndoa. Ona mistari ya Biblia ifuatayo:

  •   “Uasherati na ukosefu wa usafi wa kila namna au pupa visitajwe hata kidogo katikati yenu, . . . wala mwenendo wa aibu wala maneno ya kipumbavu wala mizaha michafu.”​—Waefeso 5:3, 4.

  •   “Viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani.”​—Wakolosai 3:5.

 Mistari hiyo haionyi tu kuhusu “uasherati” (ngono nje ya ndoa) bali pia inaonya kuhusu mambo kama vile “uchafu” (neno lililo na maana pana linalomaanisha aina yoyote ya ukosefu wa maadili) na “hamu ya ngono” (maneno ambayo hayamaanishi hisia za kawaida za kimahaba ambazo zinaweza kutoshelezwa katika ndoa bali kuwaka tamaa ambazo zinaweza kuongoza kwenye mwenendo usiofaa).

 Jiulize:

  •   Kwa nini kutuma picha za mtu akiwa uchi ni aina ya “uchafu”?

  •   Kufanya hivyo kunachocheaje ‘hamu isiyofaa ya ngono’?

  •   Kwa nini ni tamaa yenye “madhara” kuona au kusambaza picha za mtu akiwa uchi?

 Mistari ya Biblia ifuatayo inaonyesha sababu nyingine zenye kusadikisha kwa nini mtu anapaswa kuepuka kutuma ujumbe mchafu.

  •   “Fanya kabisa yote unayoweza ili ujitoe kwa Mungu ukiwa mtu aliyekubaliwa, mfanyakazi asiye na lolote la kuonea aibu.”​—2 Timotheo 2:​15.

  •    “Mnapaswa kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu!”​—2 Petro 3:11.

 Mistari hiyo inafafanua matokeo mazuri ya kuwa na maadili yanayofaa. Unapojiendesha kwa njia inayofaa, huhitaji kuogopa kwamba siku moja utajutia mambo unayofanya.​—Wagalatia 6:7.

 Jiulize:

  •    Mimi ni mtu wa aina gani?

  •    Je, ninajali sifa ya wengine?

  •    Je, ningependa kujifurahisha na jambo linalowaumiza wengine?

  •    Kutuma ujumbe mchafu kunaweza kuathirije sifa yangu?

  •    Kutuma ujumbe mchafu kunawezaje kuwafanya wazazi wangu waache kuniamini?

 SIMULIZI HALISI “Rafiki yangu mmoja alikuwa akificha uhusiano wake na mvulana fulani. Siku moja alimtumia picha yake akiwa uchi, naye mvulana huyo akamtumia yake pia. Hata kabla ya saa 48 kwisha, baba ya msichana huyo akaamua kuchunguza simu hiyo. Alipoona ujumbe wote waliokuwa wametumiana, alihuzunika sana. Msichana huyo alikiri makosa yote alipohojiwa na baba yake. Najua yeye mwenyewe anajutia mambo aliyofanya, lakini wazazi wake walishangazwa na kukasirika sana! Hata hawana uhakika ikiwa wanaweza kumwamini tena.”

 Ukweli wa mambo: Kutuma ujumbe mchafu kunamshushia heshima yule anayetuma ujumbe huo pamoja na yule anayetumiwa. “Jambo hilo hunifanya nijichukie na nisijiheshimu,” anasema msichana mmoja ambaye rafiki yake wa kiume alimshinikiza amtumie picha yake akiwa uchi.

 Kwa kuwa kutuma ujumbe mchafu kunaweza kudhuru maadili yako na ya wengine na hata kufanya mshtakiwe mahakamani, ni jambo linalofaa kufuata mashauri haya ya Biblia:

  •   “Zikimbie tamaa zinazotukia ujanani.”​—2 Timotheo 2:22.

  •   “Uyafanye macho yangu yapite ili yasione jambo lisilofaa.”​—Zaburi 119:37.

 Wewe ungefanya nini?

 Fuata mashauri ya Biblia kushughulikia hali halisi ifuatayo. Soma maneno ya Janet, kisha ufanye uamuzi ambao unafikiri ungefaa zaidi.

 “Wakati fulani nilikutana na mvulana, nikampa namba ya simu naye akanipa yake. Hata kabla ya juma moja kwisha alikuwa akiniomba nimtumie picha yangu nikiwa na mavazi ya kuogelea.”​—Janet.

 Unafikiri Janet angefanya nini? Wewe ungefanya nini?

  •  UAMUZI WA 1 Huenda ukasema: ‘Hakuna ubaya kumtumia picha hiyo. Isitoshe, ikiwa tungeenda kuogelea, angeniona nikiwa na mavazi ambayo hayajafunika mwili wangu wote.’

  •  UAMUZI WA 2 Huenda ukasema: ‘Sijui kijana huyu anataka nini. Acha nimtumie picha ambayo haionyeshi uchi sana nione atafanya nini.’

  •  UAMUZI WA 3 Huenda ukasema: ‘Huyu kijana anataka tu kufanya ngono na mimi. Nitafuta ujumbe wake.’

 Bila shaka unakubali kwamba uamuzi wa 3 ndio unaofaa, sivyo? Biblia inasema: “Mtu mwangalifu huona hatari akajificha, lakini wajinga hujitokeza mbele wakaumia.”​—Methali 22:3, Biblia Habari Njema.

 Kisa cha Janet kinaonyesha sababu kuu ambayo mara nyingi huwafanya watu watume ujumbe mchafu na kujihusisha katika aina nyingine za mwenendo usiofaa: Je, unachagua marafiki wako kwa hekima? (Methali 13:20) Msichana mmoja anayeitwa Sarah anasema, “Shirikiana na watu ambao unajua hawatavumilia mwenendo usiofaa.” Msichana anayeitwa Delia anakubaliana na maneno hayo. Anasema: “Watu fulani wanaojifanya kuwa marafiki hawakusaidii kudumisha viwango vya juu vya maadili, wanajaribu kukufanya upotoke. Ikiwa mwenendo wao unaenda kinyume na sheria za Mungu, wanakutia moyo ufanye jambo unalojua kuwa ni kosa. Hao si watu ambao ungependa kushirikiana nao, sivyo?”