Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninaweza Kukabilianaje na Kushuka Moyo?

Ninaweza Kukabilianaje na Kushuka Moyo?

 Utafanya nini?

 Fikiria mifano hii:

 Hakuna kitu kinachomfurahisha Jennifer tena. Analia kila siku bila sababu yoyote ya msingi. Anawaepuka watu na hali chochote. Ni vigumu kwake kulala au kukaza fikira. Jennifer anajiuliza: ‘Nimepatwa na nini? Kweli nitarudia hali yangu ya kawaida?’

 Mark alikuwa mwanafunzi bora shuleni. Lakini sasa anachukia shule, na alama zake katika mtihani zinashuka. Mark hafurahii michezo kama ilivyokuwa zamani. Rafiki zake wanashangazwa na hali yake. Wazazi wake wana hofu. Je, hayo ni mabadiliko ya kawaida​—au kuna jambo lingine?

 Je, mara nyingi wewe huhisi kama Jennifer au Mark? Ikiwa ndivyo, unaweza kufanya nini? Unaweza kujaribu kufanya mambo haya mawili:

  1.   Jaribu kukabiliana na tatizo lako

  2.   Zungumza na mtu mzima unayemwamini

 Unaweza kuvutiwa na Uamuzi wa A hasa ikiwa hupendi kuzungumza na wengine. Lakini, je, uamuzi huo unafaa? Biblia inasema hivi: “Wawili ni afadhali kuliko mmoja . . . kwa maana mmoja wao akianguka, yule mwingine anaweza kumwinua mwenzake. Lakini itakuwaje kwa yule aliye peke yake akianguka wakati ambapo hakuna mwingine wa kumwinua?”​—Mhubiri 4:​9, 10.

 Kwa mfano: Tuseme umepotea njia katika eneo lenye uhalifu mwingi. Ni usiku na watu usiowafahamu wamejificha katika kila pembe. Unaweza kufanya nini? Unaweza kujaribu kutafuta njia salama wewe mwenyewe. Hata hivyo, je, halingekuwa jambo la hekima kumwomba msaada mtu unayemwamini?

 Hisia za kushuka moyo ni hatari kama tu kuwa katika eneo hilo lenye uhalifu. Ni kweli kwamba baada ya muda na bila kutarajia hisia hizo zinaweza kuondoka zenyewe. Lakini ikiwa hisia za kushuka moyo zinaendelea kwa muda mrefu, ni vizuri kupata msaada.

 KANUNI YA BIBLIA: “Mtu anayejitenga na wengine . . . atashindana na hekima yote inayotumika.”​—Methali 18:1.

 Manufaa ya uamuzi wa B, yaani, kuzungumza na mzazi au mtu mzima unayemwamini, ni kwamba unaweza kufaidika kutokana na uzoefu wa mtu ambaye amewahi kukabiliana na hisia zisizofaa.

 Huenda ukasema hivi: ‘Lakini wazazi wangu hawaelewi hisia ninazokabili!’ Je, una uhakika kuhusu hilo? Hata ikiwa hali walizokabili walipokuwa matineja huenda zikatofautiana na zako, labda walikuwa na hisia kama zako. Nao wanajua jinsi ya kukabiliana nazo!

 KANUNI YA BIBLIA: “Je, hekima haimo katikati ya wazee na uelewaji katika wingi wa siku?”​—Ayubu 12:12.

 Somo: Ikiwa utamweleza siri hiyo mzazi au mtu mzima unayemwamini, inawezekana ukapata ushauri utakaokusaidia.

Kushuka moyo ni sawa na kupotea njia kwenye mtaa hatari. Ili uwe salama, pata msaada

 Vipi ikiwa ni tatizo linalohitaji kutibiwa?

 Ikiwa unahisi umeshuka moyo kila siku, huenda ukawa na hali inayohitaji kutibiwa, kama vile ugonjwa wa kushuka moyo sana.

 Kwa vijana, dalili za kushuka moyo sana ni sawa na mabadiliko ya hisia ya kawaida ambayo matineja hukabili, lakini hisia za kushuka moyo zinaweza kuwa kali zaidi na kuendelea kwa muda mrefu. Hivyo ikiwa hisia zako ni kali sana na zinaendelea kwa muda mrefu, kwa nini usizungumze na wazazi wako kuhusu kufanya uchunguzi wa afya yako?

 KANUNI YA BIBLIA: “Watu wenye afya hawahitaji tabibu, bali wenye kuugua ndio wanaomhitaji.”​—Mathayo 9:​12.

 Ikiwa itaonekana kwamba una ugonjwa wa kushuka moyo sana, hakuna haja ya kuaibika. Kushuka moyo ni tatizo la kawaida kwa vijana na linaweza kutibiwa! Marafiki wako wa kweli hawatakudharau.

 Dokezo: Uwe na subira. Itachukua muda kupona, na unaweza kutarajia siku fulani hali itakuwa nzuri na siku nyingine hali itakuwa mbaya. a

 Mpango wa kurudia hali ya kawaida

 Haidhuru ikiwa unahitaji kutibiwa, kuna mambo unayoweza kufanya ili ukabiliane na huzuni inayoendelea kwa muda mrefu. Kwa mfano, kufanya mazoezi kwa ukawaida, kula chakula chenye lishe, na kulala vya kutosha kunaweza kusaidia kutuliza hisia zako. (Mhubiri 4:6; 1 Timotheo 4:8) Pia, unaweza kuwa na daftari la kukusaidia kutunza rekodi kuhusu hisia zako, mambo unayotaka kufanya ili upone, hali zinazotokea na kukurudisha nyuma, na mafanikio unayopata.

 Iwe unakabiliwa na kushuka moyo sana au unapitia wakati mgumu kihisia, kumbuka jambo hili: Kwa kukubali msaada wa wengine na kuchukua hatua za kibinafsi ili upone, unaweza kukabiliana na kushuka moyo.

 Mistari ya Biblia ambayo inaweza kukusaidia

  •  “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.”​—Zaburi 34:18.

  •  “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza. Hatamwacha kamwe mwadilifu atikisike.”​—Zaburi 55:22.

  •  “Kwa maana mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika mkono wako wa kuume, Mwenye kukuambia, ‘Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.’”​—Isaya 41:13.

  •  “Msihangaike kamwe juu ya kesho”​—Mathayo 6:​34.

  •  “Maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu”​—Wafilipi 4:​6, 7.

a Ikiwa unafikiria kujiua, tafuta msaada haraka kutoka kwa mtu mzima unayemwamini. Kwa habari zaidi, ona mfululizo wenye sehemu nne wenye kichwa “Usikate Tamaa!” kwenye gazeti la Amkeni! la Aprili 2014