Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Je, Sheria za Nyumbani Zinahitajika?

Je, Sheria za Nyumbani Zinahitajika?

 Je, unahisi umebanwa na sheria ya nyumbani? Makala hii na daftari lililoambatanishwa litakusaidia kuzungumza na wazazi wako kuhusu hilo.

 Mtazamo unaofaa

 Uwongo: Unapoondoka nyumbani, hutakuwa chini ya sheria tena.

 Ukweli: Sheria bado zinaendelea kuwapo hata utakapoondoka nyumbani. Bado utahitajika kuwajibika kwa mtu fulani​—huenda kwa mwajiri, mwenye nyumba, au kwa serikali. “Nafikiri vijana ambao hawawezi kutii sheria nyumbani watapata shida sana watakapokuwa wakijitegemea,” anasema Danielle mwenye umri wa miaka 19.

 Biblia inasema hivi: ‘Tii serikali na mamlaka.’ (Tito 3:1) Kujifunza jinsi ya kushughulika na sheria ambazo wazazi wanaweka kunakutayarisha vizuri kwa ajili ya mambo utakayokabili utakapokuwa mtu mzima.

 Kile unachoweza kufanya: Jifunze kuangalia faida za sheria. Kijana anayeitwa Jeremy anasema hivi: “Sheria za wazazi wangu zilinisaidia kujua jinsi ya kuchagua marafiki na kutumia wakati wangu vizuri. Pia, sheria zilinisaidia kujiepusha kutazama sana televisheni na kucheza michezo mingi ya video na kuniwezesha kufanya kazi zenye kunufaisha, na ninafurahia kufanya baadhi ya kazi hizo mpaka leo.”

 Njia inayofaa ya kuzungumza

 Lakini namna gani ikiwa hukubaliani na sheria fulani? Kwa mfano, msichana anayeitwa Tamara anasema hivi: “Wazazi wangu waliniruhusu kwenda nchi nyingine, lakini sasa nimerudi nyumbani, hawaniruhusu hata niende kwenye jiji lililo umbali wa dakika 20 tu!”

 Ikiwa una tatizo kama hilo, je, itakuwa vibaya kuzungumza na wazazi wako kuhusu sheria hiyo? La hasha! Jambo kuu ni kujua wakati na jinsi ya kuzungumza nao kuhusu jambo hilo.

 Wakati. “Kijana anayeitwa Amanda anasema hivi: “Utakapokuwa umejiwekea rekodi nzuri ya uaminifu kwa kuonyesha kuwa unawajibika ndipo utakapokuwa na nafasi nzuri ya kuzungumza na wazazi wako kuhusu kurekebisha sheria fulani.”

 Msichana anayeitwa Daria aligundua kwamba hilo ni kweli. Anasema hivi: “Mama yangu alikubali kufanya marekebisho baada ya kuona kuwa ninaendelea kuwa mtiifu.” Kumbuka, kuaminika ni jambo unalofanyia kazi, si jambo unalodai.

Kuishi katika nyumba ambayo sheria za wazazi hazifuatwi kungekuwa sawa na kujaribu kutua ndege kwenye uwanja ambao sheria za waongoza-ndege hazifuatwi

 Biblia inasema hivi: “Shika amri ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako.” (Methali 6:​20) Kwa kufuata himizo hilo, utajiwekea rekodi nzuri ya uaminifu na kuwa na msingi wa kuzungumza nao.

 Jinsi. Kijana anayeitwa Steven anasema hivi: “Inafaa zaidi kuwa mwenye heshima na mtulivu unapowasiliana na wazazi wako kuliko kulalamika na kuzungumza kwa sauti kubwa.

 Daria, aliyenukuliwa mapema, anakubaliana na hilo kwa kusema hivi: “Nilipokuwa nikibishana na mama yangu hakuna jambo ambalo lingebadilika. Wakati mwingine angefanya sheria iwe ngumu hata zaidi.”

 Biblia inasema hivi: “Mtu mjinga huiachilia roho yake yote, lakini mwenye hekima huituliza mpaka mwisho.” (Methali 29:11) Kujifunza jinsi ya kujidhibiti kutakuletea manufaa, si nyumbani tu bali pia shuleni, kazini, na sehemu nyingine.

 Kile unachoweza kufanya: Tafakari kabla ya kuzungumza. Rekodi nzuri ya kutegemeka inaweza ikaharibiwa na hasira kali. Hiyo ndiyo sababu Biblia inasema hivi: “Yule ambaye si mwepesi wa hasira ana utambuzi mwingi.”​—Methali 14:29.

 Dokezo: Tumia daftari lililoambatanishwa kutafakari kuhusu sheria za nyumbani, na ikihitajika, zungumza na wazazi wako kuhusu habari hii.