Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Nifanye Nini Ikiwa Nina Tatizo la Afya? (Sehemu ya 3)

Nifanye Nini Ikiwa Nina Tatizo la Afya? (Sehemu ya 3)

 Mara nyingi vijana huonekana wakiwa na afya nzuri na nguvu nyingi. Hata hivyo, baadhi ya vijana wanakabiliwa na matatizo makubwa ya afya. Je, unakabili matatizo ya afya? Ikiwa ndivyo, unaweza kufarijiwa na maelezo ya V’loria, Justin, na Nisa. Vijana hawa watatu ni Mashahidi wa Yehova. Ona jinsi wanavyoweza kukabiliana na matatizo ya afya.

 V’loria

 Nimeugua ugonjwa wa misuli na mfumo wa neva tangu nikiwa na umri wa miaka 14. Nilipofikia umri wa miaka 20, nilikuwa nikisumbuliwa pia na ugonjwa wa baridi yabisi, lupus, na lyme. Si rahisi kufanya mambo unayotaka unapokuwa dhaifu sikuzote. Nyakati fulani, nilipooza kuanzia kiunoni mpaka miguuni, hivyo nilihitaji kutumia kiti cha magurudumu.

 Pamoja na kuteseka kimwili, nilifadhaika sana kwa sababu ya kushindwa kufanya mambo madogo kama vile kuandika au kufungua chupa. Ningewaona watoto wakitembea na kujiuliza kwa nini nashindwa kutembea kama wao? Nilijihisi sifai.

 Ninashukuru kwamba nilipata msaada, kutoka kwa washiriki wa familia yangu na pia waabudu wenzangu kutoka kutaniko la Mashahidi wa Yehova. Mara nyingi akina ndugu na dada kutanikoni walinitembelea, jambo ambalo lilinisaidia nisiwe mpweke. Wengine walinialika kwenye tafrija, hata ingawa si rahisi kunibeba kutoka kwenye kiti changu cha magurudumu ili nipande na kushuka kutoka kwenye gari.

 Ndugu na dada wenye umri mkubwa kutanikoni walinisaidia sana kwa kuwa wanajua vizuri hisia za mtu aliye na matatizo ya afya. Wamenisaidia kukubali hali yangu na kutohisi hatia ninaposhindwa kutimiza mambo mengi kama wengine. Furaha yangu inaongezeka zaidi ninapohudhuria mikutano na kushiriki utumishi wa shambani. (Waebrania 10:25) Katika hali hizo, nimetambua kwamba ingawa ninaugua, siko tofauti na wengine.

 Ninajua wazi kuwa Yehova anatupa tunachohitaji ili tuvumilie. Kwa mfano, Biblia inasema kwamba hata ikiwa mtu anachakaa kwa nje, mtu wa ndani anafanywa “upya siku baada ya siku.” (2 Wakorintho 4:​16) Ndivyo ninavyohisi kuhusu hali yangu!

 Jambo la kufikiria: Ikiwa unasumbuliwa na tatizo zito la afya, kwa nini ni muhimu kushirikiana na wengine? Kama una afya nzuri, unawezaje kuwasaidia wanaougua?​—Methali 17:17.

 Justin

 Nilianguka sakafuni na sikuweza kuinuka. Kifua changu kilibana sana na nisingeweza kutembea. Nilikimbizwa hospitalini. Mwanzoni, madaktari walishindwa kutambua tatizo linalonisumbua. Lakini, baada ya kupatwa na hali hiyo mara kadhaa, waligundua tatizo linalonisumbua, yaani ugonjwa wa Lyme.

 Ugonjwa wa Lyme umeharibu kabisa mfumo wangu wa neva. Ingawa ni muda mrefu umepita tangu ugonjwa wangu ugunduliwe, bado mwili wangu unatetemeka, na nyakati nyingine hata ninashindwa kuzuia hali hiyo. Kuna siku nyingine mwili au vidole vyangu vinaniuma sana kiasi kwamba nashindwa hata kuvisogeza. Ni kana kwamba viungo vyangu vyote vimeshika kutu.

 Mara nyingi nilijiambia hivi, ‘Nimepata ugonjwa nikiwa mdogo sana,’ na hilo lilinikasirisha sana. Kila siku ningemlilia Mungu, na kumuuliza, “Kwa nini ninaumwa hivi?” Hata nilianza kufikiri kwamba Mungu ameniacha. Lakini nilitafakari kumhusu Ayubu anayetajwa katika Biblia. Ayubu hakuelewa sababu iliyofanya akabili mambo mengi mabaya, hata hivyo aliendelea kuwa mshikamanifu kwa Mungu. Ikiwa Ayubu aliweza kuwa mshikamanifu licha ya kukabili matatizo mengi, mimi pia ninaweza kuwa mshikamanifu.

 Wazee wa kutaniko langu wananisaidia sana. Wananitembelea mara nyingi na kuniuliza jinsi ninavyohisi. Mzee mmoja alinieleza kwamba ninaweza kumpigia simu wakati wowote ninaohitaji kuongea naye. Ninamshukuru Yehova kila siku kwa kunipatia marafiki hao!​—Isaya 32:​1, 2.

 Nyakati nyingine tunapokabili ugonjwa mbaya, tunaweza kusahau kwamba Yehova anajua vizuri hali yetu. Biblia inasema hivi: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza.” (Zaburi 55:22) Ninajitahidi kufanya hivyo kila siku.

 Jambo la kufikiria: Msaada wa wale wanaokupenda unawezaje kukusaidia kuvumilia tatizo la afya?​—Methali 24:10; 1 Wathesalonike 5:​11.

 Nisa

 Nilipokuwa kijana, iligunduliwa kuwa ninaugua ugonjwa wa Marfan yaani kasoro inayoathiri viungo vya mwili na kuvifanya viwe dhaifu. Pia Marfan inaweza kuathiri moyo, macho, na viungo vingine muhimu. Ingawa sipati maumivu kila siku, lakini siku nikihisi maumivu yanakuwa makali sana.

 Ilipogundulika nina ugonjwa huo, nililia sana. Nilikuwa na wasiwasi kwamba sitaweza tena kufanya mambo niliyofurahia. Kwa mfano, nilipenda sana kucheza muziki hivyo kufikiria kwamba siku moja nitashindwa kucheza kwa sababu ya maumivu au hata kushindwa kutembea kabisa, kulinifanya niogope sana wakati ujao.

 Dada yangu amenisaidia sana. Alinisaidia niache kujisikitia. Aliniambia kwamba sipaswi kuishi nikiwa na woga, kwa kuwa hali hiyo ingetawala maisha yangu kabisa. Alinitia moyo nisali kwa bidii, kwa sababu hakuna mtu anayejua vizuri hali yangu zaidi ya Yehova.​—1 Petro 5:7.

 Andiko moja linalonitia moyo sana ni Zaburi 18:6, linalosema hivi: “Katika taabu yangu niliendelea kumwita Yehova, nami niliendelea kumlilia Mungu wangu kwa ajili ya msaada. Kutoka katika hekalu lake aliisikia sauti yangu, nacho kilio changu cha msaada mbele zake sasa kikafika masikioni mwake.” Mstari huo umenisaidia kutambua kwamba ninaposali kwa Yehova ili kumuomba anisaidie kukabiliana na hisia zangu, yeye atanisikia na kunisaidia. Yuko tayari kunisaidia wakati wowote.

 Nimejifunza kwamba si kosa kuhisi vibaya na hata kukasirika tunapokabili majanga kwa sababu hizo ni hisia za kawaida. Hata hivyo sipaswi kuruhusu hisia hizo zitawale maisha yangu na kuharibu urafiki wangu na Mungu. Hasababishi matatizo yetu, na kamwe hatatuacha tukimtanguliza maishani mwetu.​—Yakobo 4:8.

 Jambo la kufikiria: Je, tunapaswa kumlaumu Mungu tunapoteseka?​—Yakobo 1:​13.