Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Nifanye Nini Nikikosa Kitu cha Kufanya?

Nifanye Nini Nikikosa Kitu cha Kufanya?

 Kwa watu fulani, hakuna jambo baya kama kukaa nyumbani bila kuwa na shughuli ya kufanya au mahali pa kwenda. Kijana anayeitwa Robert anasema, “Pindi kama hizo, ninaketi tu nikiwa nimeduwaa bila kujua cha kufanya.”

 Je, umewahi kuhisi hivyo? Ikiwa ndivyo, makala hii inaweza kukusaidia!

 Unachopaswa kujua

  •   Huenda teknolojia isikusaidie.

     Kutumia Intaneti ni njia moja ya kupitisha wakati, lakini huenda isikusaidie kutumia uwezo wako wa kufikiri, na hivyo kuchangia hisia za kuchoshwa na maisha. Jeremy, mwenye umri wa miaka 21, anasema, “Unajikuta unakodolea macho skrini na akili ikitangatanga.”

     Mwanamke kijana anayeitwa Elena anakubaliana na hilo. Anasema, “Teknolojia ina mipaka. Inakukengeusha usifikirie ulimwengu halisi, lakini ukiweka kifaa chako cha kielektroni chini, unachoshwa na maisha hata zaidi!”

  •   Mtazamo unaweza kubadili mambo.

     Je, kuwa na mengi ya kufanya kunafanya usichoshwe na maisha? Mengi yanategemea unapendezwa kwa kadiri gani na jambo unalofanya. Kwa mfano, mwanamke kijana anayeitwa Karen anakumbuka hivi: “Shule ilinichosha sikuzote ingawa nilikuwa na mengi ya kufanya mchana kutwa. Unahitaji kujihusisha kabisa katika kile unachofanya ili kisikuchoshe.”

 Je, ulijua? “Kutokuwa na jambo la kufanya” si kipingamizi ni fursa, yaani, ni udongo wenye rutuba unaoweza kukuza ubunifu.

Wakati ulio nao ni udongo wenye rutuba utakaoruhusu ubunifu ukue

 Unachoweza kufanya

 Panua mawazo yako. Kutana na marafiki wapya. Anza kufanya jambo jipya unalopenda. Fanya utafiti kuhusu habari usizojua. Watu wanaopendezwa na mambo mengi hawachoki hata wakiwa peke yao​—na si rahisi wawachoshe wengine!

 Kanuni ya Biblia: “Jambo lolote unalofanya kwa mkono wako, lifanye kwa nguvu zako zote.”​—Mhubiri 9:​10.

 “Nilianza kujifunza Kichina cha Mandarin, na kufanya mazoezi kila siku kumenifanya nigundue kwamba nilikosa nafasi kama hiyo ya kujifunza. Ninafurahia kuwa na miradi ya kufanya. Inafanya akili yangu iwe na mengi ya kutafakari na inanisaidia kutumia muda wangu kwa njia yenye manufaa.”​—Melinda.

 Kazia fikira malengo yako. Ukitambua kusudi la kile unachofanya, utapendezwa zaidi na jambo hilo. Hata kazi za shule zinaweza kufurahisha unapotambua malengo yako.

 Kanuni ya Biblia: “Hakuna jambo bora analoweza kufanya mtu kuliko . . . kufurahia kazi yake ngumu.”—Mhubiri 2:​24.

 “Nilipokaribia kumaliza masomo, nilikuwa nikisoma kwa saa nane kila siku kwa sababu nilikuwa nyuma ya ratiba. Ilinichosha? Hapana, sikuchoka nilipozikazia fikira. Nilifikiria matokeo​—kuhitimu​—na hilo lilinichochea.”​—Hannah.

 Kubali mambo usiyoweza kubadili. Hata mambo yanayosisimua sana yanahusisha mambo fulani ya kujirudia au ya kawaida. Na hata marafiki bora wanaweza kubadili mipango, na kukuacha ukizubaa. Badala ya kuathiriwa na hali unazokabili na kuvunjika moyo, jitahidi kuwa na mtazamo mzuri.

 Kanuni ya Biblia: “Mtu aliye na moyo mchangamfu huwa na karamu daima.”​—Methali 15:15.

 “Rafiki mmoja aliniambia nijifunze kufurahia muda ninaokuwa peke yangu. Alisema kwamba kujifunza kusawazisha kuwa pamoja na watu wengine na kuwa peke yako ni ustadi wenye thamani maishani ambao kila mtu anapaswa kujifunza.”​—Ivy.