Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Kwa Nini Ujifunze Lugha Nyingine?

Kwa Nini Ujifunze Lugha Nyingine?

 Kujifunza lugha nyingine kunaweza kukusaidia kupima ikiwa una uwezo wa kujitia nidhamu na ikiwa una unyenyekevu. Je, jitihada hizo zina faida? Vijana wengi wamejibu ndiyo! Makala hii inaeleza kwa nini wanajitahidi kujifunza lugha.

 Kwa nini ujifunze?

 Watu wengi hujifunza lugha nyingine kwa sababu ni takwa katika masomo yao shuleni. Wengine wanajifunza kwa sababu zao za kibinafsi. Kwa mfano:

  •   Anna, msichana kutoka nchini Australia, aliamua kujifunza Kilatvia​—lugha ya asili ya mama yake. Anna anasema hivi: “Familia yetu inapanga kutembelea Latvia, hivyo ningependa kuwa na uwezo wa kuwasiliana na ndugu zangu wa ukoo tutakapowatembelea.”

  •   Gina, Shahidi wa Yehova kutoka Marekani, alijifunza Lugha ya Ishara ya Marekani (ASL) na akahamia Belize ili kupanua huduma yake. Anasema hivi: “Viziwi wanaweza kuwasiliana na watu wachache sana. Kwa hiyo, wanashukuru sana ninapowaambia kwamba nilijifunza Lugha ya Ishara ya Marekani ili niwafundishe Biblia katika lugha yao!”

 Je, wajua? Biblia ilitabiri kwamba habari njema ya Ufalme wa Mungu itahubiriwa kwa watu wa “kila taifa na kabila na lugha.” (Ufunuo 14:6) Vijana wengi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova wamejifunza lugha nyingine ili kupanua huduma yao katika eneo la kwao au katika nchi nyingine, na hilo linaonyesha kwamba unabii huo umetimia.

 Changamoto za kujifunza lugha

 Si rahisi kujifunza lugha mpya. Tineja anayeitwa Corrina anasema hivi: “Nilifikiri ilimaanisha tu kujifunza maneno mapya lakini nikagundua kwamba inahusisha pia kujifunza utamaduni mpya na njia mpya ya kufikiri. Kwa kweli, kujifunza lugha kunachukua muda mrefu.”

 Pia, unahitaji kuwa mnyenyekevu. Kijana anayeitwa James, ambaye alijifunza Kihispania anasema hivi: “Unahitaji kuwa tayari kujicheka mwenyewe, kwa sababu utafanya makosa mengi sana. Hiyo ni sehemu ya kujifunza.”

 Jambo kuu: Ikiwa utafaulu kukabiliana na vipingamizi na pia uwe tayari kuaibika unapokosea, inaelekea kwamba utafanikiwa kujifunza lugha nyingine.

 Dokezo: Usikate tamaa wengine wanapofanya maendeleo haraka kuliko wewe. Biblia inasema hivi: “Kila mmoja na athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, kisha atakuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe peke yake, na si kwa kujilinganisha na mtu yule mwingine.”​—Wagalatia 6:4.

 Faida za kujifunza lugha

 Kuna faida nyingi za kujifunza lugha mpya. Kwa mfano, kijana anayeitwa Olivia, anasema hivi; “Unapojifunza lugha nyingine, unapanuka na kupata marafiki wapya.”

 Kijana anayeitwa Mary alitambua kwamba kujifunza lugha mpya kumemchochea ajiamini zaidi. Anasema hivi: “Ni vigumu sana kwangu kujivunia jambo lolote ninalofanya, lakini sasa, kwa kuwa ninajifunza lugha mpya, nimekuwa nikifurahi sana kila ninapojifunza neno jipya. Kujifunza lugha kunafanya nijisikie vizuri sana.”

 Gina, aliyenukuliwa awali, ametambua kwamba kuwafundisha watu Biblia katika lugha ya ishara kumefanya afurahie zaidi kazi ya kuhubiri. Anasema hivi: “Ninahisi nimepata baraka kubwa ninapoona watu wakiwa na shangwe ninapozungumza nao katika lugha yao!”

 Jambo kuu: Kujifunza lugha nyingine kunaweza kukusaidia upate marafiki wapya, ujiamini zaidi, na kutakufanya uthamini zaidi kazi ya kuhubiri. Ndiyo njia bora ya kuwafikishia habari njema watu “kutoka mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.”​—Ufunuo 7:9.