Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Vipi Ikiwa Nimevunja Sheria Fulani ya Nyumbani?

Vipi Ikiwa Nimevunja Sheria Fulani ya Nyumbani?

 Karibu familia zote zina sheria—sheria zinazohusu mambo kama vile muda wa kurudi nyumbani, matumizi ya teknolojia, na jinsi ya kujiendesha na kuwatendea wengine.

 Vipi ikiwa utavunja sheria fulani? Huwezi kubadilisha jambo hilo, lakini unaweza kuzuia hali isiwe mbaya zaidi. Makala hii itakusaidia kufanya hivyo.

 Mambo ambayo hupaswi kufanya

  •   Ikiwa wazazi wako hawajui kama umevunja sheria fulani, unaweza kushawishika kuficha jambo hilo.

  •   Ikiwa wanajua kwamba umevunja sheria, unaweza kushawishika kutafuta visingizio au kumlaumu mtu mwingine.

 Hizo si njia bora za kushughulikia tatizo. Kwa nini? Kwa sababu kujaribu kuficha kosa lako au kutafuta visingizio visivyo na msingi ni ishara ya kwamba bado wewe ni mtoto. Ni kana kwamba unawaambia wazazi wako bado unahitaji kukua zaidi.

 “Kusema uwongo hakukusaidii. Baada ya muda, ukweli utajulikana na adhabu utakayopewa itakuwa kali zaidi kuliko ungesema kosa lako mapema.”—Diana

 Njia bora zaidi ya kushughulikia tatizo

  •   Kubali kosa lako. Biblia inasema: “Anayefunika makosa yake hatafanikiwa.” (Methali 28:13) Wazazi wako wanajua kwamba huwezi kuwa mkamilifu. Lakini swali ni, Unaweza kuwa mnyoofu?

     “Wazazi wako watakuonea huruma ikiwa utasema kweli. Ukisema kweli, watakuamini zaidi kwa unyoofu wako.”—Olivia

  •   Omba msamaha. Biblia inasema: “Mjivike unyenyekevu.” (1 Petro 5:5, Maelezo ya chini.) Unahitaji kuwa mnyenyekevu ili uweze kusema “Nisamehe”na kujizuia kuanza kuorodhesha visingizio.

     “Watu ambao hutoa visingizio mara kwa mara hudhoofisha dhamiri yao. Hatimaye, hata wakifanya jambo baya hawatajisikia vibaya tena.”—Heather

  •   Kubali matokeo ya kosa lako. Biblia inasema: “Sikilizeni nidhamu.” (Methali 8:33) Epuka kunung’unika, na ukubali adhabu yoyote ambayo utapewa na wazazi wako.

     “Kadiri unavyozidi kunung’unika unapopewa adhabu, ndivyo unavyofanya hali yako iwe mbaya zaidi. Jaribu kukubaliana na vizuizi ulivyowekewa, na usikazie fikira mambo ambayo huwezi kufanya kwa wakati huo.”—Jason

  •   Jitahidi kufanya wazazi wako waanze kukuamini tena. Biblia inasema: ‘Vua utu wa zamani unaopatana na mwenendo wenu wa zamani.’ (Waefeso 4:22) Anza kufanya mambo ambayo yanaonyesha kwamba unaweza kuaminika tena.

     “Ukiwa na kawaida ya kufanya maamuzi kwa hekima na kuwaonyesha wazazi wako kwamba hutarudia makosa uliyofanya, hatimaye watakuamini tena.”—Karen

 DOKEZO: Ili kuonyesha kwamba unaweza kuaminika tena, fanya zaidi ya kile ambacho wazazi wako wamekwambia ufanye. Kwa mfano, unapoenda mahali fulani, wataarifu unapokuwa njiani ukirudi—hata ikiwa hutachelewa. Ni kana kwamba unawaambia, ‘Ninataka mniamini tena.’