Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ni Nini Kitakachonichochea Kufanya Mazoezi?

Ni Nini Kitakachonichochea Kufanya Mazoezi?

 Kwa nini nahitaji kufanya mazoezi?

 Katika nchi fulani, vijana wanatumia muda mfupi kufanya mazoezi ya aina fulani, na hivyo wanahatarisha afya yao. Biblia inaonyesha wazi kwamba “mazoezi ya kimwili ni yenye faida.” (1 Timotheo 4:8) Zingatia mambo yafuatayo:

  •   Mazoezi yanaweza kuboresha mtazamo wako. Kufanya mazoezi kunatokeza kemikali za ubongo (endorphins) zinazofanya ustarehe na kupata furaha. Watu fulani wanasema mazoezi ni dawa ya kupunguza hisia za kushuka moyo.

     “Nikikimbia asubuhi, siku nzima ninatimiza mambo mengi na ninakuwa na furaha zaidi. Kukimbia kunaboresha hisia zangu.”—Regina.

  •   Mazoezi yanaboresha mwonekano wako. Kufanya mazoezi kwa usawaziko kutakusaidia kuwa na nguvu zaidi, kuwa na afya zaidi, na kujiamini zaidi.

     “Ninafurahi kwamba sasa ninaweza kujiinua kwenye chuma kilichowekwa juu ya kichwa—mwaka uliopita hata singeweza kufanya hivyo hata mara moja! Zaidi ya yote, ninafurahi kujua kwamba ninautunza mwili wangu.”—Olivia.

  •   Mazoezi yanaweza kukusaidia uishi maisha marefu. Kufanya mazoezi kunaboresha mifumo ya kupumua na ya moyo. Pia, mazoezi yanayofanywa ili kuboresha uwezo wa mwili kufyonza na kusafirisha oksijeni yanazuia ugonjwa wa mishipa kuziba—ugonjwa unaowaua wanaume na wanawake.

     “Tunapokuwa na ratiba ya kufanya mazoezi ya kuboresha afya, tunamwonyesha Muumba wetu kwamba tunathamini mwili aliotupa.”—Jessica.

 Jambo kuu: Mazoezi yana faida kubwa kwa afya yetu ya wakati ujao, na pia yana faida sasa. Kijana anayeitwa Tonya anasema, “Hutawahi kusema, ‘Laiti nisingeenda matembezi hayo au nisingalikimbia.’ Sijawahi kujuta ninapoacha kutoa udhuru na kufanya mazoezi.”

Gari lisilotunzwa mwishowe litaacha kufanya kazi; ndivyo ilivyo na mwili wako unapopuuza kufanya mazoezi

 Ni nini kinachonizuia kufanya mazoezi?

 Kuna vipingamizi kadhaa ambavyo vinaweza kutolewa:

  •   Sina hamu. “Nafikiri watu wanapokuwa vijana wanahisi kwamba hawawezi kufa. Ni vigumu kuwazia wakati ambapo utakuwa na matatizo ya afya. Unafikiri hayo ni matatizo ya watu wazee.”—Sophia.

  •   Sina muda. “Kwa kuwa nina ratiba yenye mambo mengi, lazima nipange muda wa kula na kulala, lakini sikuzote imekuwa vigumu zaidi kupata muda wa kufanya mazoezi.”—Clarissa.

  •   Sijajiandikisha katika ukumbi wa kufanya mazoezi. “Ni bei ghali kupata mazoezi ya kutosha—unahitaji kulipa ili kujiandikisha katika ukumbi wa mazoezi!”—Gina.

 Jambo la kufikiria:

 Ni nini kipingamizi chako kikuu cha kufanya mazoezi? Kushinda kipingamizi kutahitaji jitihada, lakini utapata matokeo mazuri sana.

 Ninaweza kufanya nini ili nipate mazoezi ninayohitaji?

 Hapa kuna madokezo kadhaa:

  •   Ni jukumu lako kutunza afya yako.—Wagalatia 6:5.

  •   Epuka visingizio. (Mhubiri 11:4) Kwa mfano, si lazima ujiandikishe kwenye ukumbi wa kufanya mazoezi ili uanze kufanya mazoezi. Tafuta jambo unalofurahia kufanya, na uliingize katika ratiba yako.

  •   Ili ujue unachoweza kufanya, waulize wengine wanafanya mazoezi ya aina gani.—Methali 20:18.

  •   Uwe na ratiba hususa. Jiwekee malengo na kupima maendeleo ili uyadumishe.—Methali 21:5.

  •   Mtafute mtu mnayeweza kufanya mazoezi pamoja. Kuwa na mwandamani wa mazoezi kutakuchangamsha na kukusaidia kudumisha ratiba.—Mhubiri 4:9, 10.

  •   Fahamu kwamba kutakuwa na vipingamizi, lakini usikate tamaa unapovikabili.—Methali 24:10.

 Uwe na usawaziko

 Biblia inatuambia kwamba kila mmoja, awe ni mwanamume au mwanamke anapaswa kuwa “mwenye kiasi katika mazoea.” (1 Timotheo 3:2, 11) Hivyo, uwe na usawaziko inapohusu kufanya mazoezi. Watu wanaopita kiasi katika mazoezi mara nyingi wanaonekana kuwa wenye majivuno. Kijana anayeitwa Julia anasema hivi: “Misuli ya mwanamume inapozidi uwezo wake wa kufikiri, havutii hata kidogo.”

 Pia, jihadhari na matangazo ya kuchochea watu wafanye mazoezi yanayosema maneno kama “Unapohisi kwamba utakufa ukiendelea, fanya mara 10 zaidi.” Ushauri kama huo unaweza kukuumiza kimwili na pia kufanya upoteze mwelekeo kuhusu “mambo muhimu zaidi” maishani.—Wafilipi 1:10.

 Pia mbinu hizo za kumchochea mtu, zinaweza kumvunja moyo. Kijana anayeitwa Vera anasema hivi: “Wasichana wengi wanakuwa na picha za watu wengine ambao wangependa kufanana nao, na wanaangalia picha hizo wanapohisi uvivu wa kufanya mazoezi. Lakini wanaishia kujilinganisha na picha hizo na kuvunjika moyo. Ni afadhali zaidi kuwa na lengo la kuboresha afya, si mwonekano tu.”