Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Kwa Nini Ujiepushe na Ponografia?

Kwa Nini Ujiepushe na Ponografia?

 Je, unaweza kujiepusha na ponografia?

 Ikiwa unatumia Intaneti, utarajie kwamba lazima utakutana na aina fulani ya ponografia. “Hata si lazima uitafute,” anasema Hayley mwenye umri wa miaka 17. “Yenyewe inakufuata ulipo.”

 Hata wale wanaoazimia kujiepusha na ponografia wanaweza kushawishiwa. “Nilijiambia kwamba ningekuwa mwangalifu, lakini nilishindwa,” anasema Greg, aliye na umri wa miaka 18. “Usiwahi kusema haitatokea kwako.”

 Leo, ni rahisi sana kupata habari za ponografia kuliko wakati mwingine wowote. Kutokana na kuanzishwa kwa njia ya kutuma ujumbe na picha za ngono kupitia simu, vijana wengi wanatengeneza na kusambaza ponografia yao.

 Jambo kuu: Unakabili hali ngumu zaidi kuliko hali ambayo wazazi wako au wazazi wa wazazi wako walikabili walipokuwa na umri kama wako. Lakini swali ni, Je, unaweza kujiepusha na ponografia?​—Zaburi 97:10.

 Jibu ni ndiyo​—ikiwa utaamua kufanya hivyo. Lakini kwanza unahitaji kuamini kabisa kwamba ponografia ni mbaya. Tuchunguze mambo machache ya uwongo na ya kweli kuhusu ponografia.

 Uwongo na ukweli

 Uwongo: Ponografia haiwezi kunidhuru.

 Ukweli: Ponografia hudhuru akili yako kama vile ambavyo sigara hudhuru mapafu yako. Inakuchafua. Ponografia huharibu kitu ambacho Mungu aliumba ili kiwe kifungo chenye nguvu na kinachodumu kati ya watu wawili. (Mwanzo 2:​24) Baada ya muda, inaweza hata kukufanya upuuze tofauti kati ya lililo sawa na lililo baya. Kwa mfano, wataalamu fulani wanasema kwamba wanaume wanaozoea kutazama ponografia wana mwelekeo wa kuunga mkono vitendo vya ukatili kuelekea wanawake.

  Biblia inaeleza kuhusu watu fulani wanaokuja “kuishiwa ufahamu wote wa maadili.” (Waefeso 4:19) Dhamiri zao zinaacha kufanya kazi hivi kwamba hawaumii wanapofanya mambo maovu.

 Uwongo: Ponografia inaweza kukufundisha kuhusu ngono.

 Ukweli: Ponografia inakufundisha kuhusu pupa. Inakufanya uwaone watu kama vyombo tu na kwamba kazi yao ni kutosheleza tu tamaa zako za kibinafsi. Si ajabu utafiti mmoja ulionyesha kwamba wale wanaozoea kutazama ponografia wana mwelekeo wa kutoridhika kingono baada ya kufunga ndoa.

  Biblia huwaambia Wakristo waepuke “uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani,”​—mambo yote ambayo ponografia inachochea.​—Wakolosai 3:5.

 Uwongo: Wale wanaojiepusha na ponografia wanaona ngono kuwa kitu cha kuaibikia.

 Ukweli: Watu wanaojiepusha na ponografia wana maoni yanayofaa kuelekea ngono. Wanaona ngono kuwa zawadi iliyoumbwa na Mungu ili kuimarisha kifungo kati ya mwanamume na mwanamke waliofunga ndoa na wanaowajibika kwa mwenzi wao. Wale wenye maoni kama hayo wana mwelekeo wa kuridhika zaidi kingono baada ya kufunga ndoa.

  Biblia inaeleza waziwazi kuhusu ngono. Kwa mfano, inawaeleza hivi waume: “Ushangilie pamoja na mke wa ujana wako . . . Upendo wake na ukufurahishe sikuzote.”​—Methali 5:​18, 19.

 Jinsi ya kujiepusha na ponografia

 Vipi ikiwa unahisi kwamba kishawishi cha kutazama ponografia ni chenye nguvu sana? Daftari yenye kichwa “Jinsi ya Kujiepusha na Ponografia” inaweza kukusaidia.

 Uwe na uhakika kwamba unaweza kushinda kishawishi cha kutazama ponografia. Pia, unaweza kujifunza kuacha kutazama ponografia ikiwa tayari umeanza zoea hilo. Utafaidika sana kwa kuchukua hatua hiyo.

 Mfikire Calvin, ambaye anakiri kwamba alianza kutazama ponografia alipokuwa na umri wa miaka 13 hivi. “Nilijua ni makosa,” Calvin anasema, “lakini sikuweza kushinda kishawishi cha kutazama ponografia. Na baada ya kuitazama, ningehisi vibaya sana. Mwishowe, baba yangu alijua​—na kusema kweli, nilipata kitulizo kwelikweli! Hatimaye, nilipata msaada niliohitaji.”

 Calvin amejifunza kujiepusha na ponografia. Anasema hivi: “Lilikuwa kosa kubwa kutazama ponografia, kosa ambalo ninalipia mpaka sasa, kwa sababu picha nilizotazama bado ziko akilini mwangu. Na wakati mwingine ninashawishika kufikiria ingekuwaje ikiwa ningetazama ponografia tena. Hata hivyo, ninafikiria jinsi nilivyo na furaha, nilivyo safi, na jinsi wakati ujao wangu ulivyo mzuri ninapofanya mambo kulingana na sheria za Yehova.”