Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Nifanye Nini Ikiwa Inaonekana Wengine Hawanipendi?

Nifanye Nini Ikiwa Inaonekana Wengine Hawanipendi?

 “Ni lazima watu wakukubali, la sivyo hutakuwa na marafiki, furaha, au kitu cha kutazamia. Utasahaulika na utakuwa mpweke.”—Carl.

 Je, ametia chumvi? Huenda. Hata hivyo, watu fulani hufanya jambo lolote ili waepuke hali ambayo Carl ameelezea. Ungefanya nini? Makala hii itakusaidia kupata njia bora zaidi ya kusuluhisha suala hilo.

 Kwa nini watu hutafuta kupendwa?

  •   Kwa sababu hawapendi kutengwa. “Niliona picha za rafiki zangu kwenye mtandao wa kijamii ambao walienda matembezi bila mimi. Hilo lilifanya nijiulize nina kasoro gani, nililemewa na mawazo ya kwamba hawakunipenda.”—Natalie.

     JAMBO LA KUFIKIRIA: Je, umewahi kuhisi kana kwamba rafiki zako wanakutenga? Ulifanya nini ili uwe sehemu ya kikundi hicho?

  •   Kwa sababu hawataki kuwa tofauti. “Wazazi wangu hawakuniruhusu niwe na simu. Vijana wenzangu wanaponiomba namba yangu, wao hushangaa sana ninapowaambia sina simu, wananiuliza: ‘Eti nini? Una miaka mingapi?’ Ninapowaambia kwamba nina umri wa miaka 13, wao hunihurumia.”—Mary.

     JAMBO LA KUFIKIRIA: Ni mipaka gani unayowekewa na wazazi wako inayokufanya uhisi tofauti na wengine? Unaweza kushughulikaje na hali hiyo?

  •   Kwa sababu hawataki kuonewa. “Watoto wenzangu shuleni hawawapendi watu wanaotenda tofauti, wanaozungumza tofauti, au hata wanaoabudu kwa njia tofauti. Ukiwa tofauti, inakuwa rahisi kuonekana na kuonewa.”—Olivia.

     JAMBO LA KUFIKIRIA: Je, umewahi kuonewa kwa sababu wewe unaonekana tofauti? Ulishughulikiaje hali hiyo?

  •   Kwa sababu hawataki kupoteza rafiki zao. “Nilijaribu kufanya mambo yaliyofanywa na kila kikundi nilichoshirikiana nacho. Nilizungumza kama wao. Nilicheka hata ikiwa jambo halikuchekesha. Hata nilishirikiana nao kuwadhihaki watu, ingawa nilijua nilikuwa nikiwaumiza hisia.”—Rachel.

     JAMBO LA KUFIKIRIA: Ni muhimu kadiri gani kwako kupendwa na vijana wenzako? Umewahi kubadili utu wako ili wakukubali?

 Unachopaswa kujua

  •   Kuwaiga wengine ili ukubalike kunaweza kukuletea matokeo mabaya. Kwa nini? Kwa sababu watu hutambua kwamba unaigiza. Brian mwenye umri wa miaka 20 anasema hivi: “Wanafunzi wenzangu hawakunipenda nilipokuwa nikiigiza kuwa kama wao, niligundua kwamba ni bora kushikamana na viwango vyako, kwa sababu watu wanatambua unapoigiza.”

     NJIA NZURI ZAIDI: Fikiria upya mambo unayopaswa kutanguliza maishani. Biblia inasema: “Mhakikishe mambo muhimu zaidi.” (Wafilipi 1:10) Hivyo, jiulize hivi, ‘Ni nini muhimu zaidi—kukubaliwa na watu wenye viwango tofauti na vyangu au kudumisha viwango vyangu?’

     “Kujaribu kuwa kama wengine ni kazi bure. Halitawafanya wakupende zaidi wala halitakufanya uwe mtu mzuri zaidi.”—James.

  •   Kutafuta kupendwa kunaweza kufanya upoteze utambulisho wako. Ukifanya hivyo, huenda ukawa mtu anayewafurahisha watu tu kwa kutenda kama watu wengine wanavyotaka utende. Kijana anayeitwa Jeremy anasema hivi: “Ningefanya jambo lolote ili kukubaliwa na kikundi fulani, hata ikiwa ningejiharibia sifa yangu. Kwa njia hiyo niliwaruhusu waniongoze kama walivyopenda. Niliishia kuwa kikaragosi chao.”

     NJIA NZURI ZAIDI: Tambua viwango vyako na uishi kupatana navyo, badala ya kuwa kama kinyonga anayebadilika rangi kulingana na mazingira yake. Biblia ina sababu nzuri za kusema hivi: “Usiufuate umati ili kutenda maovu.”—Kutoka 23:2.

     “Nilijaribu kupenda mambo yote waliyopenda—muziki, michezo, mavazi, vipindi vya televisheni, njia yao ya kujipamba . . . Nilijaribu kuwa kama wao. Nafikiri walitambua nilikuwa nikiigiza. Kila mtu alitambua jambo hilo, kutia ndani mimi mwenyewe. Niliishia kuhuzunika, kujihisi upweke, na hata sikujielewa. Nilipoteza utambulisho wangu. Nilijifunza kwamba huwezi kupatana na kila mtu unayekutana naye wala huwezi kumpendeza kila mtu. Hilo halimaanishi kwamba unapaswa kuacha kutafuta marafiki; unahitaji tu kujipa nafasi na muda wa kutambua utu wako na kukua.”—Melinda.

  •   Kutafuta kupendwa kunaweza kuathiri mwenendo wako. Kijana anayeitwa Chris alisema kwamba binamu yake alianza kutenda hivyo. Chris anasema: “Alianza kufanya mambo ambayo hakuwa akifanya zamani—kama vile kutumia dawa za kulevya—ili tu akubalike. Mwishowe akawa mraibu, na karibu aharibu maisha yake.”

     NJIA NZURI ZAIDI: Waepuke watu ambao mazungumzo na mwenendo wao unaonyesha hawana viwango vinavyofaa. Biblia inasema hivi: “Anayetembea na wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wapumbavu ataumia.”—Methali 13:20.

     “Nyakati fulani, ni vizuri kutia jitihada ili upendwe na watu. Lakini hupaswi kamwe kujitahidi hivi kwamba ufanye mambo ambayo unajua hayafai. Marafiki wazuri watakukubali kwa jinsi ulivyo.”—Melanie.

     Dokezo: Unapokutana na watu na unajaribu kuanzisha urafiki, usiwakazie fikira wale ambao wana mapendezi sawa na yako tu. Tafuta watu wenye viwango kama vyako—vya kiroho, kiadili, na wanaofuata kanuni zilezile maishani.

    Mitindo fulani ya nguo haipendezi unapoivaa. Vivyo hivyo, kuna watu ambao hawataboresha viwango vyako