Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Je, Nijichanje Chale?

Je, Nijichanje Chale?

 Kuna uvutio gani?

 “Nafikiri baadhi ya michoro mwilini ni yenye kuvutia,” anasema kijana anayeitwa Ryan.

 Sababu ya kutaka kujichanja chale huenda ikaathiri maoni yako kuhusu chale (tattoo). Kwa mfano, kijana anayeitwa Jillian anasema hivi: “Msichana fulani niliyesoma naye shuleni, alifiwa na mama yake akiwa na umri mdogo. Hivyo alipokuwa kijana, msichana huyo alichora jina la mama yake nyuma ya shingo yake. Nafikiri inapendeza kuwa na mchoro kama huo.”

 Hata hivyo, unapaswa kutafakari kwa kina sana kabla ya kuamua kuchora kitu chochote cha kudumu kwenye mwili wako! Unapaswa kujiuliza maswali gani kabla ya kujichanja chale? Na unapaswa kutumia kanuni gani za Biblia zitakazokusaidia kufanya maamuzi yanayofaa?

 Unapaswa kujiuliza maswali gani?

 Nitapata madhara gani ya afya? Tovuti ya Kliniki ya Mayo inasema kwamba “Kwa kuwa ngozi huchanika mtu anapojichanja chale, anaweza kupata magonjwa ya ngozi na matatizo mengine. Wakati mwingine uvimbe unaoitwa granuloma hujitokeza pembeni ya mchoro huo. Kujichanja chale mwilini kunaweza pia kusababisha uvimbe unaoitwa keloid​—unaosababishwa na kukua sana kwa tishu za makovu.” Zaidi ya hayo, tovuti hiyo ilisema hivi: “Ikiwa kifaa kinachotumika kuchanja chale kina damu iliyo na viini, unaweza kuambukizwa magonjwa yanayopitishwa kwa damu.”

 Kujichanja chale kutaathirije sifa yako? Upende usipende, watu huamua wewe ni mtu wa aina gani kutokana na jinsi unavyoonekana. Unaweza kuonekana kuwa mtu mkomavu au la, au mtu mwenye kutegemeka au asiyetegemeka. Kijana anayeitwa Samantha anasema, “Ninapomwona mtu aliyejichanja mwilini, mara moja ninamhusianisha na watu wanaopenda kutumia vileo na kujihusisha katika burudani.”

 Melanie, mwenye umri wa miaka 18, anaeleza jambo lingine. Anasema: “Kwa maoni yangu, chale zinaficha uzuri wako wa asili. Ni kana kwamba wale wanaojichora hawataki kujulikana wao ni watu wa aina gani hasa, hivyo wanaficha utu wao kwa kujichanja chale.”

 Je, utaendelea kuipenda chale hiyo? Baada ya muda au kadiri siku zinavyosonga mchoro huo unaweza kupoteza ubora wake kwa sababu ya kunenepa au uzee. Kijana anayeitwa Joseph anasema, “Nimeona jinsi chale zinavyoonekana baada ya makumi ya miaka kupita, hazivutii tena.”

 Allen mwenye umri wa miaka 21 anasema: “Mara nyingi chale hupitwa na wakati. Jambo lililokuwa muhimu kwa mtu wakati huo huenda lisiwe muhimu tena baada ya miaka kadhaa kupita.”

 Allen ametaja jambo muhimu sana. Ukweli ni kwamba watu wanapozidi kukua, maoni, mapendezi, na hisia zao hubadilika​—lakini alama walizochora mwilini hazibadiliki. Msichana anayeitwa Teresa anasema, “Nisingependa kujuta baadaye kwamba nina alama ya kudumu inayonikumbusha hisia fulani za kipumbavu nilizokuwa nazo.”

 Ni kanuni gani za Biblia zinazohusika?

 Mtu mkomavu hufikiria mambo yote kabla ya kufanya uamuzi. (Methali 21:5; Waebrania 5:​14) Hivyo, chunguza kanuni za Biblia zifuatazo zitakazokusaidia kufanya maamuzi yanayofaa kuhusu kujichanja chale.

  •  Wakolosai 3:​20: “Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika kila jambo, kwa maana hilo linapendeza vema katika Bwana.”

      Unaweza kupata madhara gani ikiwa unaishi na wazazi wako lakini hutaki kutii mwongozo wao?

  •  1 Petro 3:​3, 4: “Kujipamba kwenu kusiwe kule kusuka nywele kwa nje na kule kujivika mapambo ya dhahabu au kuvaa mavazi ya nje, bali kuwe yule mtu wa siri wa moyoni katika vazi lisiloharibika la roho ya utulivu na ya upole.”

      Unafikiri ni kwa nini Biblia inakazia kuhusu “yule mtu wa siri wa moyoni”?

  •  1 Timotheo 2:9: “Wanawake wajipambe kwa . . . kiasi na utimamu wa akili.”

      Neno “kiasi” linamaanisha nini? Kwa nini sifa ya kiasi ni yenye kuvutia zaidi kuliko michoro mwilini?

  •  Waroma 12:1: “Mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri.”

      Kwa nini Mungu anajali kuhusu jinsi unavyoutendea mwili wako?

 Kwa kufuata kanuni hizo, watu wengi wameamua kutojichanja chale. Wamepata jambo lingine bora zaidi kuliko chale. Teresa aliyenukuliwa mapema, anasema: “Ikiwa kuna maneno au msemo fulani unaoupenda au mtu ambaye ni muhimu kwako, basi uishi kupatana na maneno hayo au umwambie mtu huyo jinsi alivyo muhimu kwako. Badala ya kujichanja mwilini, ishi kupatana na kile unachoamini.”