Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Kwa Nini Nikatae Kufinyangwa na Vyombo vya Habari?​—Sehemu ya 2: Kwa Wavulana

Kwa Nini Nikatae Kufinyangwa na Vyombo vya Habari?​—Sehemu ya 2: Kwa Wavulana

 Vyombo vya habari huendeleza mawazo na mitazamo gani?

 Tazama maneno haya, kisha ujibu maswali yafuatayo.

Safu ya 1

Safu ya 2

Mwasi

Mwenye heshima

Mwenye Ubinafsi

Mshikamanifu

Mkali

Mwenye huruma

Mvivu

Mwenye bidii

Mzembe

Mwenye kuwajibika

Mwongo

Mnyoofu

  1.   Ni maneno gani yanayofafanua jinsi unavyowaona wavulana wanaoonyeshwa katika vyombo vya habari (kama vile katika sinema, televisheni, na matangazo ya biashara)?

  2.   Ni maneno gani yanayofafanua jinsi ambavyo wewe ungependa watu wakuone?

 Inaelekea kwamba ulipata majibu ya swali la kwanza katika safu ya 1 na majibu ya swali la pili katika safu ya 2. Ikiwa ni hivyo, hilo ni jambo zuri. Kwa nini? Kwa sababu hufanani na wavulana wanaoonyeshwa katika vyombo vya habari​—na hungependa kuwa kama wao. Fikiria ni kwa nini.

  •   Mara nyingi vyombo vya habari huonyesha wanaume wakiwa wajeuri na waasi. Kitabu Why Boys Don’t Talk​—and Why It Matters kinasema kwamba wanaume maarufu zaidi katika televisheni, sinema, na michezo ni wale “wenye nguvu nyingi na wenye hasira . . . Wanataka ionekane kwamba mwanamume halisi anapaswa kuwa mkali na mwasi.”

     Jambo la kufikiria: Je, kuwa na hasira kutakufanya uwe rafiki, mfanyakazi, au mume bora? Unapochokozwa, ni nini kitakachoonyesha kwamba una nguvu zaidi​—kulipuka kwa hasira au kujidhibiti? Ni nini kitakachothibitisha kwamba wewe ni mwanamume halisi?

     Biblia husema hivi: “Asiye mwepesi wa hasira ni bora kuliko mwanamume mwenye nguvu, naye anayezuia roho yake ni bora kuliko mtu anayeteka jiji.”​—Methali 16:32.

    Ukidhibiti hasira yako, una nguvu kuliko shujaa

  •   Vyombo vya habari huonyesha wanaume wakiwa wanapenda sana mambo ya ngono. Chris mwenye umri wa miaka 17 anasema hivi: “Katika sinema na televisheni, wavulana hubadilisha marafiki wasichana mara nyingi kuliko wanavyobadilisha mavazi yao.” Gary, mwenye umri wa miaka 18, anaongezea hivi: “Vyombo vya habari huonyesha kwamba mvulana wa kawaida hupenda sana mambo ya ngono.” Kwa mfano, baadhi ya sinema huonyesha kwamba mambo muhimu katika maisha ya mvulana ni kuponda raha, kunywa pombe, na kufanya ngono.

     Jambo la kufikiria: Je, ungependa kufanana na wavulana wanaoonyeshwa katika vyombo vya habari? Je, mwanamume halisi huwatendea wanawake kama vitu vya kutumiwa kwa ajili ya ngono, au huwatendea kwa heshima?

     Biblia husema hivi: “Kila mmoja wenu ajue jinsi ya kukiweza chombo chake mwenyewe katika utakaso na heshima, si katika hamu yenye tamaa ya ngono.”​—1 Wathesalonike 4:​4, 5.

  •   Vyombo vya habari huonyesha wavulana wakiwa wasiowajibika. Katika sinema na vipindi maarufu vya televisheni, mara nyingi wavulana matineja huonyeshwa wakiwa wavivu na wasioweza kufanya kazi zao vizuri. Labda ndiyo sababu baadhi ya watu wazima huwa na maoni kwamba wavulana hawatumainiki. Gary, aliyetajwa mwanzoni, anasema hivi: “Nilipofikisha umri wa miaka 16, ilikuwa vigumu kwangu kupata kazi kwa sababu wenye biashara katika eneo nililoishi walitaka kuajiri wanawake peke yao. Walihisi kwamba wavulana wote matineja hawawajibiki au kutumainika!”

     Jambo la kufikiria: Kwa nini haifai kufanya wavulana matineja waonekane kuwa wasiowajibika na wasiotumainika? Unaweza kuonyeshaje kwamba ni tofauti

     TBiblia husema hivi: “Usiache mtu yeyote audharau kamwe ujana wako. Badala yake, uwe kielelezo kwa waaminifu katika kusema, katika mwenendo, katika upendo, katika imani, katika usafi wa kiadili.”​—1 Timotheo 4:​12.

 Mambo unayopaswa kujua

  •   Vyombo vya habari vinaweza kukuathiri sana. Kwa mfano, vyombo vya habari vinaweza kukufanya uhisi kwamba unapaswa kuiga mitindo ya kisasa zaidi ili uwe maarufu. Colin, mwenye umri wa miaka 17 anasema hivi: “Matangazo ya biashara huonyesha jinsi wavulana wanavyopaswa kuvalia na wasichana wakiwang’ang’ania. Hilo linaweza kumchochea mtu anunue nguo hizo. Nimefanya hivyo mara kadhaa!”

     Jambo la kufikiria: Je, jinsi unavyovalia huonyesha jinsi ulivyo kikweli, au unaiga watu wengine? Ni nani hasa wanaofaidika unapotumia pesa kununua vitu vya kisasa zaidi?

     Biblia husema hivi: “Acheni kufanyizwa kulingana na mfumo huu wa mambo.”​—Waroma 12:2.

  •   Wasichana hawavutiwi unapoiga mawazo na mitazamo inayoendelezwa katika vyombo vya habari. Fikiria mambo ambayo baadhi yao wamesema:

    •  “Ninapendezwa na mvulana anayeridhika na jinsi alivyo kuliko yule asiyejiamini na anayependa kujionyesha mbele ya watu. Kwa kweli, mvulana ambaye sikuzote hupenda kujionyesha havutii hata kidogo!”​—Anna.

    •  “Watangazaji wa biashara hufanya wavulana wahisi kana kwamba wanahitaji vifaa fulani au kuwa na umbo fulani ili wavutie wasichana. Hata hivyo, kadiri wasichana wanavyoendelea kukomaa, wanaacha kuona mambo kijuu juu tu. Badala yake, wanaona sifa za ndani za mwanamume na kuchunguza jinsi anavyowatendea watu. Kwa mfano, wasichana huvutiwa na wanaume wanyofu na washikamanifu.”​—Danielle.

    •  “Mara nyingi, mvulana anayeonekana kuwa na umbo zuri sana huwa mwenye kiburi, na sipendi kuwa na rafiki kama huyo. Unaweza kuwa mvulana mwenye umbo linalovutia sana, lakini hatavutia ikiwa utu wako haufanani na umbo lako.”​—Diana.

     Jambo la kufikiria: Kuhusu mvulana Samweli, Maandiko yanasema kwamba “alikuwa akiendelea kukua na kupendwa na Yehova na vilevile na wanadamu.” (1 Samweli 2:​26) Ni mambo gani unayohitaji kufanyia kazi ili uwe na sifa kama hiyo?

     “Endeleeni kuwa kama wanaume.”​—1 Wakorintho 16:13.

 Mambo unayoweza kufanya

  •   Changanua mawazo na mitazamo inayoendelezwa katika vyombo vya habari. Fikiria maneno haya ya Biblia: “Kila kitu kilicho katika ulimwengu​—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani​—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu.”​—1 Yohana 2:16.

     Vyombo vya habari huendeleza tamaa ya kufuatilia mambo hayo na kuyaonyesha kuwa ya kawaida. Hivyo, jifunze kuchanganua mambo unayoona. Kwa kawaida, wafanya-biashara hubuni mambo hayo ili wapate pesa.

  •   Usifinyangwe na vyombo vya habari. Biblia husema hivi: “Mjivike utu mpya, ambao kupitia ujuzi sahihi unafanywa kuwa mpya kulingana na mfano wa Yule aliyeuumba”​—si kulingana na watu wanaoonyeshwa katika vyombo vya habari.​—Wakolosai 3:​10.

     Ili kukusaidia ufuate shauri hilo, fikiria tena sifa zilizoonyeshwa mwanzoni mwa makala hii​—sifa ambazo ungependa kuwa nazo. Kwa nini usianze sasa kuzisitawisha au kuziboresha?

  •   Tafuta vielelezo vinavyofaa. Biblia husema hivi: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima.” (Methali 13:20) Ni wanaume gani unaowafahamu ambao wameonyesha kwamba wana hekima? Wanaweza kuwa watu wa familia, kama vile baba au mjomba wako. Wanaweza kuwa pia marafiki au wanaume wakomavu unaowafahamu. Katika makutaniko ya Kikristo ya Mashahidi wa Yehova, kuna wanaume wengi ambao ni vielelezo vyema. Biblia ina vielelezo tunavyoweza kuiga, kama vile Tito, aliyewawekea vijana kielelezo kizuri cha kuiga.​—Tito 2:​6-8.

     Pendekezo: Tumia kitabu Igeni Imani Yao ili ujifunze kuhusu mifano bora ambayo wanaume wanaweza kuiga iliyo katika Biblia, kama vile Abeli, Noa, Abramu, Samweli, Eliya, Yona, Yosefu, na Petro.