Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Je, Nibatizwe?​—Sehemu ya 1: Maana ya Ubatizo

Je, Nibatizwe?​—Sehemu ya 1: Maana ya Ubatizo

 Kila mwaka, vijana wengi wanaolelewa na Mashahidi wa Yehova hubatizwa. Je, unafikiria kuchukua hatua hiyo? Ikiwa ndivyo, kwanza unahitaji kuelewa maana ya kujiweka wakfu na kubatizwa.

 Ubatizo ni nini?

 Ubatizo unaotajwa katika Biblia unahusisha kuzamishwa kabisa ndani ya maji—wala si kunyunyiziwa maji—jambo lililo na maana ya pekee.

  •   Kuzamishwa ndani ya maji wakati wa ubatizo ni tangazo la hadharani la kwamba umeacha maisha ya kufanya mapendezi yako mwenyewe.

  •   Kuinuliwa kutoka ndani ya maji kunaonyesha kwamba umeanza maisha mapya ukiwa umekazia fikira kufanya mapenzi ya Mungu.

 Kwa kubatizwa, unaonyesha hadharani kwamba unatambua Yehova ana mamlaka ya kuweka viwango vya mema na mabaya, na unatangaza rasmi kwamba umeahidi kwa hiari kuishi kulingana na matakwa yake.

 Jambo la kufikiria: Kwa nini ufikirie kutangaza hadharani kwamba unataka kumtii Yehova katika maisha yako yote? Ona 1 Yohana 4:19 na Ufunuo 4:11.

 Kujiweka wakfu kunamaanisha nini?

 Kabla ya kubatizwa, unapaswa kujiweka wakfu kwa Yehova faraghani. Jinsi gani?

 Katika sala yako ya kibinafsi, unamwambia Yehova kwamba unaahidi kumtumikia milele na kwamba utafanya mambo anayotaka hata hali iweje na hata watu wengine waamue kufanya nini.

 Ubatizo ni tangazo la hadharani linaloonyesha kwamba ulijiweka wakfu. Unawaonyesha wengine kwamba umejikana mwenyewe na sasa wewe ni mali ya Yehova.—Mathayo 16:24.

 Jambo la kufikiria: Kwa nini maisha yako yanakuwa bora zaidi unapokuwa mali ya Yehova? Ona Isaya 48:17, 18 na Waebrania 11:6.

 Kwa nini ubatizo ni muhimu?

 Yesu alisema kwamba wanafunzi wake walipaswa kubatizwa. (Mathayo 28:19, 20) Hivyo, ubatizo bado ni takwa kwa Wakristo. Kwa kweli, Biblia inasema kwamba ni muhimu mtu abatizwe ili aweze kuokolewa.—1 Petro 3:21.

 Hata hivyo, nia yako ya kubatizwa inapaswa kuchochewa na upendo na uthamini wako kwa Yehova. Mtazamo wako unapaswa kuwa kama wa mtunga-zaburi aliyeandika hivi: “Nitamlipa Yehova nini kwa mema yote aliyonitendea? . . . Nami nitaliitia jina la Yehova. Nitamtimizia Yehova nadhiri zangu.”—Zaburi 116:12-14.

 Jambo la kufikiria: Yehova amekufanyia mambo gani mema, na unaweza kumlipa jinsi gani? Ona Kumbukumbu la Torati 10:12, 13 na Waroma 12:1.