Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Kwa Nini Uwe Mnyoofu?

Kwa Nini Uwe Mnyoofu?

 Kwa nini baadhi ya watu si wanyoofu?

 Katika ulimwengu wetu, unyoofu huonwa kuwa udhaifu. Isitoshe, huenda wengine wakafikiri hivi:

  •   ‘Nisipowadanganya wazazi wangu, huenda nikanyimwa uhuru.’

  •  Nisipoiba mtihani, huenda nisifaulu.’

  •  Nisipoiba kifaa hiki, nitahitaji kuhifadhi pesa ili nikinunue.’

 ‘Pamoja na hayo, shida iko wapi?’ huenda wengine wakakuuliza. ‘Kwani watu wote ni wanyoofu?’

 Jibu la swali hilo ni hapana. Watu wengi, kutia ndani idadi kubwa ya vijana, wanaamini kwamba unyoofu una faida, na wana sababu nzuri ya kuamini hivyo. Biblia inasema “lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia.” (Wagalatia 6:7) Kwa maneno mengine, sikuzote matendo yetu yana matokeo​—iwe ni mazuri au mabaya.

 Kwa mfano, ona baadhi ya matokeo mabaya ambayo watu wamepata kwa sababu ya kusema uwongo.

  “Nilimdanganya mama yangu kuhusu kijana fulani niliyekuwa nawasiliana naye. Alikuwa na uthibitisho wa kutosha kwamba ninasema uwongo. Mara ya tatu nilipomdanganya kuhusu jambo hilo, Mama alishindwa kuvumilia. Nilizuiwa kutoka nyumbani kwa majuma mawili na sikuruhusiwa kutumia simu yangu ya mkononi au kutazama televisheni kwa mwezi mmoja. Sikuwadanganya tena wazazi wangu toka wakati huo!”​—Anita.

 Jambo la kufikiria: Kwa nini huenda ikachukua muda mrefu kwa Anita kuaminiwa tena na mama yake?

 Biblia inasema hivi: “Sasa kwa kuwa mmeuondolea mbali uwongo, semeni kweli kila mmoja wenu na jirani yake.”​—Waefeso 4:25.

  “Niliwadanganya wazazi wangu na kufikiri hawatajua. Hatimaye waligundua kwamba nilidanganya siku waliponiambia nirudie tena kuwaeleza kilichotukia. Ilikuwa tofauti kabisa na ukweli hivi kwamba nisingeweza kukumbuka mambo niliyoeleza kuhusu tukio hilo. Kwa kawaida unapoeleza ukweli, hupati tatizo hilo!”​—Anthony.

 Jambo la kufikiria: Anthony angewezaje kuepuka hali hiyo yenye kuaibisha?

 Biblia inasema hivi: “Midomo ya uwongo ni chukizo kwa Yehova, lakini wanaotenda kwa uaminifu ni furaha kwake.”​—Methali 12:22.

  “Nina rafiki ambaye hupenda kutia chumvi mambo anayosema. Hukuza mambo na kupotosha habari. Ninampenda na ninajitahidi nisimwelewe vibaya. Lakini si rahisi kumwamini au kumtegemea.”​—Yvonne.

 Jambo la kufikiria: Kutia chumvi na uwongo “mdogo” kunawezaje kuharibu sifa nzuri ya rafiki ya Yvonne?

 Biblia inasema hivi: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”​—Waebrania 13:18.

Msingi wenye ufa unaweza kudhoofisha jengo zima; vivyo hivyo, kukosa unyoofu kunaweza kuharibu sifa yako nzuri

 Faida ya kuwa mnyoofu

 Sasa fikiria matokeo mazuri unayoweza kupata ukiwa mnyoofu.

  “Mwanamke aliyekuwa akitembea mbele yangu aliangusha pesa. Nilimwita na kumrudishia pesa zake. Alinishukuru sana. Alisema hivi: ‘Umefanya jambo zuri. Watu wengi hawawezi kufanya hivyo.’ Nilihisi vizuri kutambulika kuwa mtu anayefanya mambo mazuri!”​—Vivian.

 Jambo la kufikiria: Huenda kwa nini mwanamke huyo alishangazwa na unyoofu huo? Vivian alifaidikaje kwa kuwa mnyoofu?

 Biblia inasema hivi: ‘Wenye furaha ni wale . . . wanaotenda uadilifu wakati wote.’​—Zaburi 106:3.

  “Familia yetu hufanya kazi za usafi, na wakati mwingine tunaposafisha ofisi, tunaona sarafu kwenye sakafu. Jambo hilo likitukia, tunaweka sarafu hiyo katika meza iliyo karibu. Mfanyakazi mmoja alitaka kuudhika kwa sababu tulikuwa wanyoofu sana​—‘Haina thamani yoyote!’ alisema. Lakini matokeo yakawaje? Alituamini sikuzote.”​—Julia.

 Jambo la kufikiria: Huenda unyoofu wa Julia utamfaidishaje atakapohitaji mtu wa kumdhamini kwa ajili ya kazi nyingine?

 Biblia inasema hivi: “Fanya kabisa yote unayoweza ili ujitoe kwa Mungu ukiwa mtu aliyekubaliwa, mfanyakazi asiye na lolote la kuonea aibu.”​—2 Timotheo 2:​15.

  “Nilipokea mshahara wa saa 80 badala ya saa 64. Ingawa ningefaidika kama ningebaki nao, kwa kweli nisingeweza kufanya hivyo. Nilimweleza meneja jambo hilo, na alishukuru sana. Kampuni ina mafanikio, lakini nisingeweza kubaki na pesa hizo kwa kuwa kufanya hivyo ni sawa na kuiba.”​—Bethany.

 Jambo la kufikiria: Je, kuna tofauti yoyote kati ya kuibia shirika na kumwibia mtu?

 Biblia inasema hivi: “Mtu mwenye hila ni chukizo kwa Yehova, lakini urafiki Wake uko pamoja na watu wanyoofu.”​—Methali 3:32.