Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Je, Ni Urafiki wa Kawaida au wa Kimapenzi?—Sehemu ya 2: Ninaonyesha Ishara Gani?

Je, Ni Urafiki wa Kawaida au wa Kimapenzi?—Sehemu ya 2: Ninaonyesha Ishara Gani?

 Unapenda rafiki yako awe huru kuzungumza nawe anapohitaji kufanya hivyo. Na karibuni umekuwa ukizungumza mara nyingi na rafiki mmoja. Tatizo ni kwamba, rafiki huyo ni wa jinsia tofauti. Unajiambia hivi: ‘Sisi ni marafiki tu,’ ukifikiri rafiki huyo atafikiri kwa njia hiyo pia. Je, unapaswa kuhangaishwa na jambo hilo?

 Mambo yanayoweza kutokea

 Si vibaya kuwa na marafiki wa jinsia tofauti. Lakini itakuwaje ikiwa umesitawisha urafiki wa pekee pamoja na mtu huyo? Katika kisa kama hicho, anaweza kufikiri kwamba unataka kuanzisha urafiki wa kimapenzi.

 Je, hilo ndilo unalomaanisha? Ona njia kadhaa jambo hilo linavyoweza kutokea, hasa tusipokuwa waangalifu.

  •   Unamtendea mtu fulani kwa njia ya pekee.

     “Ingawa huwezi kudhibiti hisia za mtu mwingine, haifai kuchochea hisia za wengine kwa kudai kwamba ni marafiki tu, na kisha tunawapigia simu na kuzungumza nao kila wakati.”​—Sierra.

  •   Unakubali kutendewa kwa njia ya pekee.

     “Sikuanza kumtumia ujumbe msichana huyo, lakini kila mara aliponitumia ujumbe wa simu, nilijibu. Hatimaye ilikuwa vigumu kwangu kumweleza kwamba nilimwona kama rafiki wa kawaida tu.”​—Richard.

  •   Unachochea hisia za wengine.

     “Baadhi ya watu wanafikiri kuwachezea wengine kimapenzi ni mchezo. Wanachezea hisia za wengine bila kuchukua kwa uzito uhusiano huo. Nimeona jambo hilo mara nyingi, na sikuzote mtu fulani huumia.”​—Tamara.

 Jambo Kuu: Kuwasiliana mara kwa mara na kumwonyesha ufikirio mtu kupita kiasi kunatoa ishara ya kuvutiwa naye kimapenzi.

 Kwa nini ni muhimu?

  •   Linawaumiza wengine.

     Biblia inasema hivi: “Tarajio lililocheleweshwa linafanya moyo uwe mgonjwa.” (Methali 13:12) Wewe ungetarajia nini ikiwa mtu fulani angekuonyesha ishara kwamba anavutiwa nawe kimapenzi?

     “Kuna msemo usemao, ‘Kumwacha mtu kwenye ndoano.’ Unarejelea wakati mtu anaponasa samaki kwenye ndoano lakini hamchukui wala hamwachilii. Jambo hilo linaweza kutokea katika uhusiano. Ikiwa huna mpango wa kuanzisha urafiki wa kimapenzi lakini unaendelea kumwacha mwingine “kwenye ndoano,” utamsababishia maumivu mengi mtu huyo.”​—Jessica.

  •   Itaharibu sifa zako nzuri.

     Biblia inasema hivi: “Kuangalia, si faida za kibinafsi za mambo yenu wenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.” (Wafilipi 2:4) Mtu anayeangalia tu faida zake mwenye huchochewa na sifa gani? Mtazamo huo unawezaje kuharibu sifa nzuri za mtu?

     “Sivutiwi na wavulana wanaowachezea kimapenzi wasichana. Kuwachezea wengine kimapenzi ni dalili ya mwanzo ya kutokuwa mshikamanifu katika ndoa. Unafanya hivyo ili uhisi wewe ni wa maana lakini huo ni ubinafsi.”​—Julia.

 Jambo Kuu: Watu wanaoonyesha ishara za kuvutiwa kimapenzi na wengine bila kuwa na mpango wa kuendeleza uhusiano huo wanajiumiza na kuwaumiza wengine.

 Unachoweza kufanya

  •   Biblia inatuhimiza tuwatendee “wanaume vijana kama ndugu” na “wanawake vijana kama dada kwa usafi wote wa kiadili.” (1 Timotheo 5:​1, 2) Ikiwa unafuata kanuni hiyo, utalinda urafiki wako pamoja na watu wa jinsia tofauti.

     “Nikifunga ndoa, sitawachezea kimapenzi wenzi wa ndoa wa watu wengine. Kuwa na usawaziko ninaposhughulika na watu wa jinsia tofauti nikiwa mseja ndilo jambo litakalonisaidia nisiwachezee wengine kimapenzi nitakapofunga ndoa.”​—Leah.

  •   Biblia inasema hivi: “Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na kosa.” (Methali 10:19) Kanuni hiyo inatumika ama tunapozungumza na wengine au tunapotuma ujumbe wa simu​—kutia ndani ujumbe wenyewe na mawasiliano ya mara kwa mara.

     “Kwa kweli hakuna haja ya kutuma ujumbe kila siku kwa msichana kama huna mpango wa kuanzisha urafiki wa kimapenzi.”​—Brian.

  •   Biblia inasema hivi: “Hekima inayotoka juu kwanza kabisa ni safi kiadili.” (Yakobo 3:​17) Kumkumbatia mtu kunaweza kuonwa kwa njia safi kiadili​—au ishara ya kuvutiwa kimapenzi.

     “Ninajaribu kuwa na mazungumzo ya kirafiki lakini bila kuwachezea wengine kimapenzi kwa kuwakumbatia na kuwagusa.”​—Maria.

 Jambo Kuu: Chunguza kwa uangalifu jinsi unavyoshughulika na watu jinsia tofauti. “Ni vigumu kuwa na urafiki mzuri,” anasema msichana aitwaye Jennifer, “na usingependa kuharibu uhusiano huo kwa kuonyesha ishara zitakazowachanganya wengine.”

 Madokezo

  •    Uwe makini na maelezo ya wengine. Ikiwa mtu fulani anakuuliza, “Wewe na yule mna urafiki wa kimapenzi?” inaweza kumaanisha kwamba huenda mna uhusiano wa karibu sana.

  •    Uwatendee kwa njia ile ile rafiki zako wote wa jinsia tofauti. Usichague mtu mmoja na kumwonyesha uangalifu wa pekee sana.

  •   Uwe mwangalifu unapotuma ujumbe inapohusu, idadi ya jumbe , mambo unayoandika, na wakati unaotuma ujumbe huo. “Hakuna haja ya kutuma ujumbe wa simu kwa mtu wa jinsia tofauti saa sita za usiku,” anasema msichana aitwaye Alyssa.