Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Je, Mimi Huchukua Mambo kwa Uzito?

Je, Mimi Huchukua Mambo kwa Uzito?

 Kadiria kiwango chako!

  •  Mimi . . . nyakati zote, nyakati nyingi, mara kadhaa, au hakuna wakati

    •  ninakuwa mnyoofu

    •  ninategemeka

    •  ninafika kwa wakati

    •  ninafanya kazi kwa bidii

    •  ninafuata utaratibu

    •  ninawasaidia wengine

    •  ninafuata haki

    •  ninawaheshimu wengine

    •  ninawajali wengine

  •   Ni sifa gani inayofafanua utu wako vizuri?

     Endelea kutimiza sifa hiyo.​—Wafilipi 3:​16.

  •   Ni sifa gani unayohitaji kufanyia kazi?

 Habari ifuatayo itakusaidia unapojitahidi kufanya maendeleo.

 Kuchukua mambo kwa uzito kunamaanisha nini?

 Watu wanaochukua mambo kwa uzito hutimiza majukumu yao nyumbani, shuleni, na katika jamii. Wanatambua kwamba mambo wanayofanya yanaathiri wengine. Kwa hiyo, wanapokosea, wao hukubali makosa yao, wanaomba msamaha, na wanajitahidi kurekebisha mambo.

 Biblia inasema: “Kila mmoja ataubeba mzigo wake mwenyewe.”​—Wagalatia 6:5.

 Kwa nini nichukue mambo kwa uzito?

  Mtu anayechukua mambo kwa uzito atatumia vipawa vyake kwa hekima na watu watamheshimu zaidi, watamtendea kama mtu mzima na kumpa uhuru na mapendeleo.

 Biblia inasema: “Je, umemwona mtu stadi katika kazi yake? Yeye atasimama mbele ya wafalme.”​—Methali 22:29.

  Kwa kawaida mtu anayechukua mambo kwa uzito ni mkarimu na kwa sababu hiyo anaweza kufurahia urafiki wa watu wengine.

 Biblia inasema: “Muwe na mazoea ya kuwapa watu, na watu watawapa ninyi.”​—Luka 6:38.

  Mtu anayechukua mambo kwa uzito huhisi kwamba anatimiza mambo na anajivunia mambo hayo, na hilo humfanya awe na ujasiri.

 Biblia inasema: “Lakini kila mmoja na athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, kisha atakuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe peke yake.”​—Wagalatia 6:4.

 Ninawezaje kuchukua mambo kwa uzito zaidi?

 Ili upate jibu la swali hilo, angalia maelezo yafuatayo. Ni maneno gani yanayofafanua vizuri jinsi unavyohisi?

 “Mimi hukasirika sana kwa sababu wazazi wangu wananitendea kama mtoto eti wakitaka kujua niko wapi kila wakati!”​—Kerri.

 “Wazazi wangu huniruhusu niende na marafiki wangu bila tatizo lolote.”​—Richard.

 “Ninapowatazama watoto wengine wenye umri kama wangu kisha nione mambo wanayofanya mimi hujiuliza: ‘Mbona wazazi wangu hawaniruhusu nifanye mambo hayo?’”​—Anne.

 “Wazazi wangu huniacha nifanye chochote ninachotaka. Ninawashukuru sana kwa kunipa uhuru.”​—Marina.

 Jambo kuu: Vijana fulani hupewa uhuru mwingi kuliko wengine. Kwa nini iwe hivyo?

 Ukweli wa mambo: Utapewa uhuru zaidi ikitegemea unaaminika kwa kadiri gani.

 Kwa mfano, fikiria kile ambacho wawili kati ya vijana waliotajwa mapema walisema.

 Richard: “Wakati fulani wazazi wangu walikuwa na shaka ikiwa nitatumia uhuru wanaonipa kwa njia nzuri. Lakini sasa wananiamini kwa sababu nimeutumia vizuri. Siwaambii wazazi wangu uwongo kuhusu mahali ninapoenda na pia ninawaambia ninaenda na nani. Kwa kawaida, mimi huwaambia wazazi wangu ninapanga kufanya nini hata ikiwa hawajaniuliza.”

 Marina: “Niliwadanganya wazazi wangu mara mbili, na pindi zote mbili waligundua uwongo huo. Tangu wakati huo sijawahi kuwadanganya tena. Kwa mfano, mimi huwaeleza waziwazi ninafanya nini, na pia mimi huwapigia simu ninapokuwa nje. Siku hizi wananiamini zaidi.”

Unatanguliza nini​—kazi za nyumbani au burudani?

 Je, ungependa kutendewa kama Richard na Marina wanavyotendewa? Basi jichunguze katika sehemu zifuatazo:

MAISHA YAKO YA NYUMBANI

  •   Je, wewe humaliza kazi unazopewa nyumbani?

  •   Je, wewe hurudi nyumbani kwa wakati ambao umeambiwa urudi?

  •   Je, wewe huwatendea wazazi wako pamoja na ndugu na dada zako kwa heshima?

 Ni jambo gani kati ya hayo matatu unayohitaji kufanyia kazi?

 Biblia inasema: “Watiini wazazi wenu”​—Waefeso 6:1.

ELIMU YAKO

  •   Je, wewe humaliza kazi mlizogawiwa shuleni kwa wakati?

  •   Je, unajitahidi kuboresha maksi zako?

  •   Je, una mazoea mazuri ya kujifunza?

 Ni jambo gani kati ya hayo matatu unayohitaji kufanyia kazi?

 Biblia inasema: “Hekima ni ulinzi.” (Mhubiri 7:12) Kupata elimu nzuri kutakusaidia uwe na hekima.

SIFA YAKO

  •   Je, wewe ni mnyoofu unapozungumza na wazazi wako na watu wengine?

  •   Je, wewe hutumia pesa kwa hekima?

  •   Je, watu wanajua kwamba wewe ni mwenye kutegemeka?

 Ni jambo gani kati ya hayo matatu unayohitaji kufanyia kazi?

 Biblia inasema: ‘Vaa utu mpya.’ (Waefeso 4:​24) Unaweza kuboresha sifa zako na pia jina lako.

 Pendekezo: Chagua jambo moja ambalo unahitaji kufanyia maendeleo. Zungumza na wengine ambao wanafaulu kutimiza sifa hiyo. Andika mambo hususa ambayo unaweza kufanya ili kuiboresha, kisha chunguza maendeleo yako kwa mwezi mmoja. Andika katika kitabu maendeleo yako na udhaifu. Baada ya mwezi huo mmoja kagua maendeleo uliyofanya.