Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Nifanye Nini Ikiwa Mzazi Wangu Ni Mgonjwa?

Nifanye Nini Ikiwa Mzazi Wangu Ni Mgonjwa?

 Vijana wengi hawahangaishwi na wazo la kuwatunza wazazi wao. Kwa sababu huenda miaka mingi itapita kabla ya wazazi wao kukabili matatizo ya afya.

 Lakini ikiwa baba au mama yako anakuwa mgonjwa ukiwa ungali kijana utafanya nini? Fikiria vijana wawili waliokabili hali hiyo.

 Kisa cha Emmaline

 Mama yangu ana ugonjwa wa kudumu na wenye maumivu makali unaoathiri viungo, ngozi, na mishipa ya damu unaoitwa Ehlers-Danlos syndrome (EDS).

 Ugonjwa huo hauna tiba, na kwa miaka kumi sasa hali ya mama imeendelea kuzorota. Nyakati nyingine kiasi chake cha damu mwilini kilishuka sana hivi kwamba uhai wake ulikuwa hatarini na nyakati nyingine maumivu yalikuwa makali sana hivi kwamba alitamani kufa.

 Familia yetu ni ya Mashahidi wa Yehova, na kutaniko tunaloshirikiana nalo limekuwa msaada mkubwa sana kwetu. Kwa mfano, hivi karibuni msichana aliye na umri kama wangu alitutumia kadi kutueleza kwamba anatupenda sana na kutuhakikishia yuko tayari kutusaidia wakati wowote. Inafariji sana kuwa na rafiki kama huyo.

 Biblia imenisaidia sana. Kwa mfano, andiko moja ninalopenda sana ni Zaburi 34:18 linalosema: “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo.” Andiko lingine ni Waebrania 13:6, linalosema: “Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa.”

 Andiko hilo la mwisho hunifariji sana. Hofu yangu kuu ni kwamba mama yangu atakufa. Ninampenda sana na kila siku ninashukuru kwamba yuko hai. Mstari huo wa Biblia unanisaidia kutambua kwamba ninaweza kukabiliana na wakati ujao nikiwa na uhakika hata hali ziweje.

 Lakini kuna jambo lingine linaloniogopesha. EDS ni ugonjwa wa kurithi. Mama yangu alirithi kutoka kwa mama yake, nami nimeurithi kutoka kwa mama yangu. Ndiyo, mimi pia nina ugonjwa wa EDS. Lakini Waebrania 13:6 inanihakikishia kwamba Yehova atakuwa “msaidizi wangu” katika hali hii pia.

 Ninajaribu kufurahia mambo ya sasa, kusahau yaliyopita, na kutohofia mambo ya wakati ujao. Ikiwa nitakazia fikira mambo ambayo mama yangu alikuwa akitimiza zamani na kuyalinganisha na jinsi ugonjwa wake unavyomwathiri, nitashuka moyo. Biblia inasema kwamba majaribu yanayotupata ni ‘ya dakika na ni mepesi’ yanapolinganishwa na tumaini la kuishi milele bila magonjwa.​—2 Wakorintho 4:​17; Ufunuo 21:​1-4.

 Mambo ya kufikiria: Ni nini kinachomsaidia Emmaline kudumisha mtazamo mzuri? Wewe unawezaje kudumisha mtazamo mzuri unapokabili hali ngumu?

 Kisa cha Emily

 Nilipokuwa katika shule ya sekondari, baba yangu alipatwa na ugonjwa wa kushuka moyo. Ni kana kwamba baba yangu alipotea kabisa na mtu mwingine akachukua nafasi yake. Tangu wakati huo, baba yangu amekuwa na huzuni, woga usio na msingi wowote, na kushikwa na wasiwasi ghafla. Amekuwa na ugonjwa huo kwa miaka 15 sasa. Lazima awe anajihisi vibaya kwa sababu ya kulemewa na hisia za huzuni ambazo anajua hazina sababu ya msingi!

 Sisi ni Mashahidi wa Yehova, na kutaniko letu limetutegemeza sana. Waamini wenzetu wametuonyesha fadhili na wanaelewa tunayopitia, na hakuna mtu ambaye amemfanya baba ahisi kwamba hatimizi jambo lolote kutanikoni. Kuona jinsi baba yangu anavyovumilia jaribu hilo kumenifanya nimpende hata zaidi.

 Ninakumbuka jinsi baba alivyokuwa zamani. Hakulemewa na mahangaiko, hakuwa anateseka, na alikuwa na furaha. Ninamkosa sana. Inanihuzunisha sana kumwona kila siku akipambana na adui ambaye yuko ndani ya fikira zake mwenyewe.

 Hata hivyo, baba hujitahidi sana kudumisha mtazamo mzuri. Hivi karibuni hali yake ilipokuwa mbaya sana, alihakikisha kwamba anasoma sehemu fulani ndogo ya Biblia kila siku, hata kama ni mistari michache tu. Kufanya hivyo kulimwimarisha sana. Ingawa hilo lilionekana kuwa jambo dogo lilimsaidia kwa njia kubwa sana. Ingawa kipindi hicho kilikuwa kigumu sana, kilinifanya nimheshimu baba yangu hata zaidi.

 Ninapenda sana andiko la Nehemia 8:10 linalosema: “Shangwe ya Yehova ndiyo ngome yenu.” Hilo ni kweli kabisa. Shangwe ninayopata ninaposhirikiana na wengine kutanikoni na kushiriki katika utendaji wa kutaniko, inasaidia kuponya moyo wangu ninapolemewa na hisia. Shangwe hiyo inanichangamsha siku nzima. Mfano wa baba yangu unanifundisha kwamba hata tukikabili hali gani, siku zote Yehova atatutegemeza.

 Mambo ya kufikiria: Emily amemsaidiaje baba yake ambaye ni mgonjwa? Unawezaje kumsaidia mtu aliye na ugonjwa wa kushuka moyo?