Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninaweza Kupinga Vishawishi Jinsi Gani?

Ninaweza Kupinga Vishawishi Jinsi Gani?

 Mtume Paulo aliandika hivi: “Ninapotaka kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami.” (Waroma 7:​21) Umewahi kuhisi kama mtume Paulo? Ikiwa ndivyo, makala hii inaweza kukusaidia kupinga kishawishi cha kutenda kulingana na tamaa mbaya.

 Unachopaswa kujua

 Ukishinikizwa na vijana wenzako unaweza kushawishiwa kufanya mambo mabaya. Biblia inasema kwamba “watu wabaya hupotosha maadili.” (1 Wakorintho 15:33, maelezo ya chini) Kushinikizwa na watu wengine au vyombo vya habari kunaweza kuchochea tamaa ya moyo wako ambayo inaweza kukushawishi ufanye mambo mabaya na hata kusababisha ‘ufuate umati ili kutenda maovu.’​—Kutoka 23:2.

 “Shinikizo la kutaka upendwe na kukubaliwa linaweza kukuongoza ufanye chochote wengine wanachofanya ili tu ukubaliwe nao.”​—Jeremy.

 Jambo la kufikiria: Kwa nini inaweza kuwa vigumu kupinga kishawishi ikiwa unajali sana jinsi wengine wanavyofikiri kukuhusu?​—Methali 29:25.

 Jambo kuu: Usikubali vijana wenzako wakushinikize upuuze viwango vyako.

 Unachoweza kufanya

 Elewa mambo unayoamini. Ikiwa hujui mambo unayoamini, unaweza kuwa kama kikaragosi ambacho kinaongozwa na watu wengine. Ni jambo bora zaidi kufuata himizo hili la Biblia: “Hakikisheni mambo yote; shikamaneni na yaliyo mema.” (1 Wathesalonike 5:​21) Kadiri unavyoelewa mambo unayoamini, ndivyo inavyokuwa rahisi zaidi kuishi kulingana na mambo hayo na kupinga kishawishi cha kutenda kinyume na mambo unayoamini.

 Jambo la kufikiria: Kwa nini unaamini kwamba viwango vya Mungu vya maadili vimekusudiwa kukunufaisha?

 “Nimegundua kwamba wakati wowote ninaposhikamana na kile ninachoamini na kushinda kishawishi, wengine wananiheshimu zaidi.”​—Kimberly.

 Mfano wa kuigwa katika Biblia: Danieli. Inawezekana Danieli alikuwa bado tineja “[alipoazimia] moyoni mwake” kwamba angetii sheria za Mungu.​—Danieli 1:8.

Ikiwa hujui mambo unayoamini, unaweza kuwa kama kikaragosi ambacho kinaongozwa na watu wengine

 Tambua udhaifu wako. Biblia inaeleza kuhusu “tamaa za ujana”​—ni tamaa ambazo zinakuwa na nguvu hasa unapokuwa kijana. (2 Timotheo 2:​22) Zinatia ndani si tamaa ya ngono tu, bali pia tamaa ya kukubaliwa na wengine, na tamaa ya uhuru wa kujifanyia maamuzi kabla ya kufikisha umri wa kufanya hivyo.

 Jambo la kufikiria: Biblia inasema kwamba “kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe.” (Yakobo 1:​14) Ni tamaa gani iliyo na ushawishi mkubwa kwako?

 “Uwe mnyoofu kwa kutambua tamaa zenye ushawishi mkubwa kwako. Fanya utafiti kuhusu jinsi ya kukabiliana na tamaa hizo, na uandike mambo unayoweza kutumia. Kwa njia hiyo, utajua jinsi ya kupinga kishawishi utakapokikabili wakati ujao.”​—Sylvia.

 Mfano wa kuigwa katika Biblia: Daudi. Nyakati fulani alifanya maamuzi kwa kushinikizwa na wengine au na tamaa zake mwenyewe. Lakini Daudi alijifunza kutokana na makosa yake na alijaribu kuboresha mambo. Alisali hivi kwa Yehova: “Umba moyo safi ndani yangu . . . na uweke roho mpya ndani yangu, iliyo imara.”​—Zaburi 51:10.

 Shinda vishawishi. Biblia inasema hivi: “Usiache ushindwe na uovu.” (Waroma 12:21) Hilo linamaanisha usikubali kishawishi kikushinde. Unaweza kuchagua kufanya jambo linalofaa.

 Jambo la kufikiria: Unaweza kuhakikisha jinsi gani kwamba unafanya jambo linalofaa katika hali inayokushawishi ufanye jambo lisilofaa?

 “Ninafikiria jinsi nitakavyohisi nikitenda kulingana na jinsi tamaa yangu inavyonishawishi. Je, nitahisi vizuri? Labda, lakini kwa muda mfupi tu. Je, bado nitaendelea kuhisi vizuri hata baada ya muda mrefu kupita? Hapana, badala yake nitahisi vibaya sana. Je, hilo litakuwa na faida? La!”​—Sophia.

 Mfano wa kuigwa katika Biblia: Paulo. Ingawa alikubali kwamba alikuwa na mwelekeo mbaya, Paulo aliushinda. Aliandika hivi: “Ninautia nidhamu sana mwili wangu, na kuuongoza kama mtumwa.”​—1 Wakorintho 9:​27, maelezo ya chini.

 Jambo kuu: Wewe ndiye unayeamua jinsi ya kukabiliana na kishawishi.

 Kumbuka, vishawishi ni vya muda mfupi. Melissa mwenye umri wa miaka 20 anasema hivi: “Mambo mengi ambayo yalikuwa vishawishi vikubwa kwangu wakati nilipokuwa shuleni, sasa si mambo ya muhimu hata kidogo kwangu. Kukumbuka hilo kunanihakikishia kwamba vishawishi vya sasa pia vitapita na siku moja nitatafakari na kutambua kwamba maisha yangu yamekuwa bora kwa sababu nilivipinga.”