Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Je, Niache Shule?

Je, Niache Shule?

 “Sipendi shule!” Kama unahisi hivyo ni rahisi kufikiria kuacha shule. Makala hii itakusaidia kujifunza mambo yatakayokusaidia kuwa na mtazamo tofauti kuhusu shule.

 Kwa nini wengine huacha shule?

 Wataalamu wametaja mambo yafuatayo kuwa sababu za watu kuacha shule:

  •   Masomo magumu. ‘Ninazidi kufanya vibaya sana katika masomo yangu.’

  •   Kutojali. ‘Sioni faida ya kile ninachojifunza.’

  •   Hali ngumu ya kiuchumi. ‘Ninahitaji kufanya kazi ili kuitegemeza familia yangu.’

 Hesabu gharama

 Biblia inasema hivi: “Mwerevu hutafakari kila hatua.” (Methali 14:15) Andiko hilo linatufundisha nini? Ikiwa unafikiria kuacha shule, hakikisha unahesabu gharama kwanza.

 Jiulize:

  •   ‘Nikiacha shule nitafanya kazi gani wakati ujao?’

     “Tafakari hali itakuwaje wakati ujao utakapohitaji kufanya kazi ili kuitegemeza familia yako. Utafanyaje hivyo ikiwa waajiri wengi wanataka watu ambao angalau wawe wamehitimu elimu ya sekondari?”—Julia.

  •   ‘Je, kuacha shule kutaathiri uwezo wangu wa kushughulikia hali ngumu maishani?’

     “Shule inakutayarisha kukabiliana na maisha. Wakati ujao, watu utakaoshirikiana nao, vishawishi utakavyokabiliana navyo, na kazi utakayofanya itafanana na changamoto ulizokabili shuleni.”—Daniel.

  •   ‘Ikiwa nitaacha shule, je, nitakuwa na stadi zitakazonisaidia maishani?’

     “Ingawa mambo unayojifunza shuleni hayaonekani kuwa ya maana sasa, utakapokuwa na umri wa miaka 23 na unapanga bajeti, utakumbuka na kujiambia;‘ Afadhali ningalikuwa makini darasani katika kipindi cha hesabu.”—Anna.

 Njia bora zaidi

  •   Omba msaada. Biblia inasema: “Washauri wengi huleta mafanikio.” (Methali 11:14) Ikiwa bado unazidi kufanya vibaya katika masomo yako, omba msaada kutoka kwa mzazi, mwalimu, mshauri wa shule, au mtu mwingine mwenye umri mkubwa unayemwamini ili akupe madokezo yatakayokusaidia.

     “Ongea na mwalimu wako ikiwa hufanyi vizuri katika masomo yako. Huenda ukafikiri kwamba mwalimu wako ndiye chanzo cha tatizo, hata hivyo unaweza kuboresha hali yako kwa kuomba msaada.”—Edward.

  •   Fikiria mbele. Biblia inasema: “Ni afadhali mwisho wa jambo kuliko mwanzo wake.” (Mhubiri 7:8) Utakapomaliza shule, utakuwa na sifa na stadi zitakazokusaidia sana maishani.

     “Utakapokuwa mtu mzima, huenda usihitaji kuandika insha au kusoma kwa ajili ya mitihani, lakini uwezo wako wa kushughulikia matatizo unapokuwa shuleni, utakusaidia kukabiliana na changamoto baada ya kuhitimu shule.”—Vera.

    Kuacha shule ni sawa na kutoka nje ya mashua kabla haijatia nanga bandarini, ni afadhali ubaki kwenye mashua!

  •   Fikiria njia nyingine. Biblia inasema: “Wote walio na haraka kwa hakika watakuwa maskini.” (Methali 21:5) Usiwe mwepesi kufikia mkataa kwamba kuacha shule ndilo suluhisho pekee. Unaweza kumalizia elimu yako kwa kupitia mtandao au kufundishwa ukiwa nyumbani.

     “Shule inakufundisha kufanya kazi kwa bidii, kusuluhisha matatizo, na kushirikiana na wengine. Manufaa yake ni ya muda mrefu. Kumaliza shule ni jambo bora.”—Benjamin.

 Jambo kuu: Maliza shule na utakuwa umejitayarisha vizuri kupambana na majukumu ya utu uzima.