Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Je, Tuvunje Urafiki Wetu? (Sehemu ya 2)

Je, Tuvunje Urafiki Wetu? (Sehemu ya 2)

 Kwanza, chagua kikao kinachofaa. Ni kikao gani kinachofaa?

 Fikiria jinsi ambavyo wewe mwenyewe ungependa kutendewa. (Mathayo 7:12) Je, ungependa kujulishwa uamuzi huo mbele ya watu? Sivyo.

 Isipokuwa iwe lazima, haingefaa kuvunja urafiki huo kwa kuacha ujumbe kwenye mashine ya kujibu simu, kutuma ujumbe mfupi kwenye simu, au kupitia barua-pepe. Badala yake, chagua mahali na wakati unaofaa ili kuzungumzia jambo hilo zito.

 Unapaswa kusema nini? Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo ‘wasemezane kweli.’​—Waefeso 4:25.

 Hivyo, njia bora ni kutumia busara na kuwa thabiti. Sema waziwazi kwa nini unahisi kwamba urafiki huo hautadumu.

 Huhitaji kutaja orodha ndefu ya makosa au kumshambulia kwa mashtaka. Badala ya kusema, “Wewe hufanyi” hili au lile au “Hujapata kamwe” kufanya hivi au vile, afadhali kutumia maneno yanayoonyesha hisia zako kama vile, “Mimi ninahitaji mtu ambaye . . . ” au “Mimi ninaona kwamba hatuwezi kuendelea kuwa marafiki kwa sababu . . . ”

 Huo si wakati wa kuyumba-yumba au kushawishiwa ubadili maoni yako. Kumbuka kwamba kuna sababu nzito ambazo zimekusukuma ufikie uamuzi wa kuvunja urafiki huo. Kwa hiyo, uwe mwangalifu rafiki yako akijaribu kutumia ujanja kubadili maoni yako. “Nilipovunja urafiki wetu,” anasema msichana mmoja anayeitwa Lori, “mvulana niliyekuwa na urafiki naye alianza kujifanya kwamba ana huzuni kila wakati. Nafikiri alifanya hivyo ili nimhurumie. Nilimsikitikia. Lakini sikuruhusu jambo hilo libadili uamuzi wangu.” Kama Lori, uwe na hakika kuhusu unachotaka. Shikamana na uamuzi wako. Acha siyo yako imaanishe siyo.​—Yakobo 5:12.