Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Nifanye Nini Ninapokosea?

Nifanye Nini Ninapokosea?

 Wewe ungefanya nini?

 Soma kuhusu mambo yaliyompata Karina, na uwazie mambo hayo yanakupata wewe. Ungefanya nini ikiwa ungekuwa katika hali kama yake?

 Karina: “Nilikuwa nikiendesha gari kwa kasi sana kuelekea shuleni niliposimamishwa na polisi ambaye alinipa risiti ya kunitoza faini. Nilikasirika sana! Nilipomwambia Mama, aliniambia niripoti kisa hicho kwa Baba. Sikutaka Baba ajue kuhusu jambo hilo.”

  Wewe ungefanya nini?

  1.  Uamuzi wa A: Kukaa kimya huku ukitumaini baba yako hatajua.

  2.  Uamuzi wa B: Kumweleza baba yako mambo yote yaliyofanyika.

 Unaweza kushawishika kuchagua Uamuzi wa A. Huenda hata ukajiambia kwamba mama yako atafikiri ulimweleza baba yako mambo yaliyofanyika. Lakini kuna sababu zinazofaa kwa nini unapaswa kufunua makosa uliyofanya​—iwe ni makosa ya kuvunja sheria za barabarani au jambo lingine lolote.

 Sababu tatu kwa nini ukubali makosa yako

  1.  1. Kwa sababu ni jambo linalofaa kufanya hivyo. Inapofafanua kuhusu viwango ambavyo Wakristo wanapaswa kufuata, Biblia inasema: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”​—Waebrania 13:18.

     “Nimejitahidi sana kuwa mnyoofu na kuwajibika kwa matendo yangu na hata kukiri makosa yangu mara tu ninapoyafanya.”​—Alexis.

  2.  2. Kwa sababu watu wana mwelekeo wa kuwasamehe wale wanaokubali makosa yao. Biblia inasema: “Anayefunika makosa yake hatafanikiwa, lakini yeye anayeyaungama na kuyaacha ataonyeshwa rehema.”​—Methali 28:13.

     “Ujasiri unahitajiwa ili ukubali makosa, na ukiyakubali watu watakuamini zaidi. Wataona kwamba wewe ni mnyoofu. Kwa kufanya hivyo angalau kunakuwa na faida fulani katika kosa ulilofanya.”​—Richard.

  3.  3. Jambo muhimu hata zaidi, utamfurahisha Yehova Mungu. Biblia inasema: “Mtu mwenye hila ni chukizo kwa Yehova, lakini urafiki Wake uko pamoja na watu wanyoofu.”​—Methali 3:​32.

     “Baada ya kufanya kosa zito, nilitambua kwamba nilihitaji kuliungama. Yehova hawezi kunibariki nisipofanya mambo kwa njia anayoikubali.”​—Rachel.

 Karina alishughulikiaje kosa lake? Alihakikisha kwamba baba yake hakujua kuhusu risiti ya faini aliyotozwa. Lakini hangeweza kulificha jambo hilo milele. Karina anasema: “Mwaka mmoja hivi baadaye baba yangu alikuwa akipitia rekodi za bima alipoona risiti hiyo yenye jina langu. Nilijipata matatani. Mama yangu alikasirika sana kwa sababu sikufanya jambo alilokuwa ameniambia nifanye!”

 Somo: Karina anasema: “Mtu anapoficha makosa yake anafanya hali iwe mbaya hata zaidi. Unayalipia makosa hayo baadaye!”

 Kujifunza kutokana na makosa unayofanya

 Kila mtu hukosea. (Waroma 3:​23; 1 Yohana 1:8) Kama tulivyoona ni ishara ya ukomavu na unyenyekevu kuyakubali makosa yetu mara tu tukoseapo.

 Hatua inayofuata ni kujifunza kutokana na makosa tunayofanya. Kwa kusikitisha, vijana wengine hawaelewi faida zinazopatikana kwa kufanya hivyo! Wanaweza kuhisi kama msichana mmoja anayeitwa Priscilla alivyohisi. Anasema: “Nilikuwa nikivunjika moyo sana kwa sababu ya makosa niliyofanya. Nilijidharau, na kwa hiyo niliyaona makosa yangu kuwa mzigo mkubwa nisioweza kubeba. Hisia zilinilemea na kujiona sifai.”

 Je, wewe huhisi hivyo nyakati nyingine? Ikiwa ndivyo, basi kumbuka jambo hili: Unapokazia fikira makosa uliyofanya hapo awali ni kama unakazia macho kioo cha kuangalia nyuma ya gari huku ukiendesha gari. Kukazia fikira makosa hayo kutakufanya ujihisi hufai na hata ukose nguvu za kukabiliana na matatizo wakati ujao.

 Badala ya kukazia fikira makosa yaliyopita, jitahidi sana kuwa na maoni yenye usawaziko

 “Kumbuka makosa uliyofanya na ujifunze kutokana nayo ili usiyarudie. Hata hivyo usiyakazie fikira sana kiasi cha kukufanya uhisi umevunjika moyo.”​—Elliot.

 “Mimi hujitahidi kujifunza jambo fulani ninapokosea ili linisaidie kuboresha utu wangu na nijue jinsi ya kushughulikia hali hiyo kwa njia tofauti wakati ujao. Kwa kweli hiyo ndiyo njia inayofaa kwa sababu inanisaidia kukomaa.”​—Vera.