Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Michezo?

Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Michezo?

 Michezo inaweza kuwa mizuri​—au mibaya kwako. Inategemea unacheza nini, jinsi gani, na kwa muda gani.

 Ina faida gani?

 Michezo inasaidia kuboresha afya. Biblia inakubali kwamba “mazoezi ya kimwili ni yenye faida.” (1 Timotheo 4:8) Kijana anayeitwa Ryan anasema hivi: “Kucheza michezo ni njia nzuri ya kufanya mazoezi. Inafaa kufanya hivyo kuliko kukaa ndani na kucheza michezo ya video.”

 Michezo hukuza ushirikiano na kukusaidia kujidhibiti. Biblia inatumia mfano unaohusu mchezo fulani kufundisha jambo lenye kujenga. Inasema hivi: “Wakimbiaji katika mbio wote hukimbia, lakini ni mmoja tu anayepokea tuzo.” Inaeleza hivi pia: “Kila mtu anayeshiriki katika shindano hujizuia katika mambo yote.” (1 Wakorintho 9:​24, 25) Jambo kuu ni kwamba mtu anahitaji kujidhibiti na kuwa na ushirikiano ili acheze kulingana na sheria za mchezo. Kijana anayeitwa Abigail anakubaliana na jambo hilo. Anasema, “Michezo imenifundisha jinsi ya kushirikiana na kuwasiliana na wengine.”

 Michezo inaweza kujenga urafiki. Mchezo huwaunganisha watu pamoja. Msichana anayeitwa Jordan anasema hivi: “Michezo mingi inahusisha mashindano, lakini ikiwa unaona ni kujifurahisha tu, kucheza michezo ni njia nzuri ya kukuunganisha na marafiki.”

 Kuna hatari gani?

 Unacheza nini? Biblia inasema hivi: “Yehova humchunguza mwadilifu na pia mwovu, na mtu yeyote anayependa jeuri nafsi Yake hakika inamchukia.”​—Zaburi 11:5.

 Baadhi ya michezo inahusisha jeuri. Kwa mfano, msichana anayeitwa Lauren anatambua hilo kwa kusema hivi: “Kusudi la mchezo wa ndondi ni kumpiga mtu mwingine. Tukiwa Wakristo, hatupaswi kupigana, hivyo kwa nini tujiburudishe kwa kutazama wengine wakipigwa?”

 Jambo la kufikiria: Je, unacheza au kutazama michezo yenye jeuri, ukijidanganya kwamba ni sawa kwa kuwa haitakufanya utende kwa jeuri? Ikiwa ndivyo, kumbuka kwamba Zaburi 11:5 inasema kwamba Yehova humchukia mtu “anayependa jeuri,” na si tu mtu anayetenda jeuri.

 Unacheza jinsi gani? Biblia inasema hivi: “Bila kufanya jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu wa akili mkiwaona wengine kuwa ni bora kuliko ninyi.”​—Wafilipi 2:3.

 Bila shaka, mchezo wowote unaokuwa na timu zinazoshindana lazima utahusisha kiasi fulani cha roho ya mashindano. Lakini roho ya mtu kufanya chochote anachoweza ili tu kupata ushindi inaweza kufanya mchezo usifurahishe. “Roho ya mashindano inaweza kumwathiri mtu haraka,” anasema kijana anayeitwa Brian. “Kadiri unavyofanikiwa katika mchezo, ndivyo unavyohitaji kuwa na unyenyekevu.”

 Jambo la kufikiria: Msichana anayeitwa Chris anakiri hivi: “Sisi hucheza mpira kila juma, na kuna baadhi ambao wameumia.” Hivyo jiulize, ‘Ni mambo gani yanayoweza kumfanya mtu aumie? Ninapaswa kufanya nini ili nisiumie?’

 Unacheza kwa muda gani? Biblia inasema hivi: “Mhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.”​—Wafilipi 1:​10.

 Unahitaji kupanga mambo unayopaswa kutanguliza; mambo ya kiroho yanapaswa kuwekwa mahali pa kwanza. Michezo mingi huchezwa kwa muda mrefu sana, iwe mtu ndiye anayecheza au anatazama tu. Msichana anayeitwa Daria anasema hivi: “Nilizozana na mama yangu mara kwa mara kwa sababu nilitumia muda mwingi kutazama michezo kwenye televisheni wakati ambapo ningeweza kuwa nikifanya mambo mengine muhimu.”

Kukazia fikira michezo kupita kiasi ni sawa na kutia chumvi nyingi sana katika chakula chako

 Jambo la kufikiria: Je, unasikiliza ushauri wa wazazi wako wanapokueleza kuhusu mambo unayopaswa kutanguliza? Msichana anayeitwa Trina anasema hivi: “Mimi na ndugu zangu tulipokuwa tukiacha kufanya kazi muhimu na badala yake kutazama michezo, mama alikuwa akitukumbusha kwamba wachezaji hao watalipwa pesa nyingi iwe tutawatazama au la. Kisha angetuuliza hivi: ‘Lakini ni nani anayewalipa ninyi?’ Alikuwa akimaanisha kwamba tayari wachezaji wana kazi. Lakini ikiwa tutaanza kupuuza kufanya kazi zetu za shule na shughuli zingine, tutashindwa kujitegemeza baadaye. Jambo la msingi ni kwamba mama alikuwa akituambia kutazama au kucheza michezo hakupaswi kuwa jambo muhimu zaidi maishani mwetu.”