Hamia kwenye habari

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kujipaka Vipodozi na Kuvalia Vito?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kujipaka Vipodozi na Kuvalia Vito?

Jibu la Biblia

 Ingawa Biblia haizungumzii jambo hilo kwa undani, haishutumu kujipaka vipodozi, kuvalia vito, au aina nyingine ya mapambo. Hata hivyo, badala ya kukazia fikira sura, Biblia inazungumza kuhusu “mapambo yasiyoharibika ya roho ya utulivu na ya upole.”​—1 Petro 3:​3, 4.

Kujipamba hakushutumiwi

  •   Wanawake waaminifu katika Biblia walijipamba. Rebeka, ambaye aliolewa na Isaka, mwana wa Abrahamu, alivaa pete ya dhahabu puani, bangili za dhahabu, na vito vingine vyenye thamani ambavyo alipewa zawadi na baba-mkwe wake. (Mwanzo 24:22, 30, 53) Vivyo hivyo, Esta alikubali “utaratibu wa kurembeshwa” ili kujitayarisha kwa ajili ya uwezekano wa kuwa malkia wa Milki ya Ashuru. (Esta 2:​7, 9, 12) Utaratibu huo wa kurembeshwa ulitia ndani matumizi ya “manukato” au aina mbalimbali za vipodozi.​—Union Version.

  •   Mifano ya Biblia inazungumzia vito kwa njia inayofaa. Kwa mfano, mtu anayetoa ushauri mzuri analinganishwa na “kipuli cha dhahabu . . . kwa sikio linalosikia.” (Methali 25:12) Vivyo hivyo, Mungu mwenyewe alilinganisha jinsi anavyolitendea taifa la Israeli na mume anayempamba bibi harusi wake kwa bangili, mkufu, na vipuli. Mapambo hayo yalifanya taifa hilo liwe kama mwanamke “mrembo kupindukia.”​—Ezekieli 16:11-13.

Maoni yasiyo sahihi kuhusu vipodozi na vito

 Maoni yasiyo sahihi: Kwenye 1 Petro 3:3, Biblia inashutumu “kusuka nywele na kuvaa mapambo ya dhahabu.”

 Ukweli: Muktadha unaonyesha kwamba Biblia inakazia umuhimu wa urembo wa ndani na kuutofautisha na kujipamba kwa nje. (1 Petro 3:3-6) Ulinganifu huo unaonekana pia katika sehemu nyingine za Biblia.​—1 Samweli 16:7; Methali 11:22; 31:30; 1 Timotheo 2:9, 10.

 Maoni yasiyo sahihi: Kwa kuwa Yezebeli alipaka macho yake wanja, basi ni kosa kujipaka vipodozi.​—2 Wafalme 9:​30.

 Ukweli: Yezebeli, ambaye alijihusisha katika ulozi na alikuwa muuaji, alihukumiwa kwa sababu ya matendo yake maovu, lakini si kwa sababu ya mwonekano wake.​—2 Wafalme 9:​7, 22, 36, 37.