Kwa Wagalatia 6:1-18

  • Kubebeana mizigo (1-10)

    • Kuvuna ulichopanda (7, 8)

  • Kutahiriwa si muhimu (11-16)

    • Kiumbe kipya (15)

  • Umalizio (17, 18)

6  Akina ndugu, hata mtu akichukua hatua isiyofaa kabla hajajua, ninyi mlio na sifa za kustahili kiroho jaribuni kumrekebisha upya mtu huyo kwa roho ya upole.+ Lakini kila mmoja wenu aendelee kujiangalia,+ kwa kuwa ninyi pia mnaweza kujaribiwa.+  Endeleeni kubebeana mizigo mizito,+ na hivyo mtaitimiza sheria ya Kristo.+  Kwa maana mtu akifikiri yeye ni kitu wakati yeye si kitu,+ anajidanganya mwenyewe.  Lakini kila mmoja na achunguze matendo yake mwenyewe,+ kisha atakuwa na sababu ya kushangilia kuhusiana na yeye mwenyewe, na si kwa kujilinganisha na mtu mwingine.+  Kwa maana kila mtu ataubeba mzigo* wake mwenyewe.+  Zaidi ya hayo, mtu yeyote anayefundishwa* neno na ashiriki katika mambo yote mema pamoja na yule anayetoa fundisho hilo.*+  Msipotoshwe: Mungu si wa kudhihakiwa. Kwa maana lolote analopanda mtu, ndilo atakalovuna pia;+  kwa sababu yule anayepanda kwa mwili wake atavuna uharibifu kutokana na mwili wake, lakini yule anayepanda kwa roho, atavuna uzima wa milele kutokana na roho.+  Basi tusife moyo katika kufanya mema, kwa maana kwa wakati unaofaa tutavuna ikiwa hatutachoka kabisa.*+ 10  Basi, tukiwa bado na nafasi,* acheni tuwatendee watu wote mema, na hasa wale ambao ni ndugu zetu katika imani. 11  Oneni kwamba nimewaandikia kwa herufi kubwa kwa mkono wangu mwenyewe. 12  Wote wanaotaka kujionyesha kuwa wazuri katika mwili* ndio wanaojaribu kuwalazimisha mtahiriwe, wakifanya hivyo ili tu wasiteswe kwa ajili ya mti wa mateso* wa Kristo. 13  Kwa maana hata wale wanaotahiriwa hawaishiki Sheria,+ lakini wanataka mtahiriwe ili wawe na sababu ya kujisifu kuhusu mwili wenu. 14  Lakini sitajisifu kamwe, isipokuwa katika mti wa mateso* wa Bwana wetu Yesu Kristo,+ ambaye kupitia kwake ulimwengu umeuawa* kuhusiana nami, nami kuhusiana na ulimwengu. 15  Kwa maana kutahiriwa si kitu wala kutotahiriwa,+ bali kiumbe kipya ndicho kitu.+ 16  Na wale wote wanaotembea kwa utaratibu kwa kanuni hii ya mwenendo, juu yao na kuwe na amani na rehema, ndiyo, juu ya Israeli wa Mungu.+ 17  Kuanzia sasa mtu yeyote asinitaabishe, kwa maana ninabeba mwilini mwangu alama za mtumwa wa Yesu.+ 18  Akina ndugu, fadhili zisizostahiliwa za Bwana wetu Yesu Kristo ziwe pamoja na roho mnayoonyesha. Amina.

Maelezo ya Chini

Au “mzigo wa wajibu.”
Au “anayefundishwa kwa mdomo.”
Au “fundisho hilo la mdomo.”
Au “hatutakufa moyo.”
Tnn., “wakati unaofaa.”
Au “wanaotaka kuonekana wazuri kwa nje.”
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Au “umeuawa kwenye mti.”