Kulingana na Yohana 6:1-71

  • Yesu alisha wanaume 5,000 (1-15)

  • Yesu atembea juu ya maji (16-21)

  • Yesu ndiye “mkate wa uzima” (22-59)

  • Wengi wakwazwa na maneno ya Yesu (60-71)

6  Baada ya hapo Yesu akavuka Bahari ya Galilaya, au Tiberia.+  Na umati mkubwa sana ulikuwa ukimfuata,+ kwa sababu walikuwa wakiona ishara za miujiza alizokuwa akifanya kwa kuwaponya wagonjwa.+  Basi Yesu akapanda mlimani, akaketi huko pamoja na wanafunzi wake.  Sasa Pasaka,+ ile Sherehe ya Wayahudi, ilikuwa imekaribia.  Yesu alipoinua macho yake na kuona umati mkubwa ukija, akamuuliza Filipo: “Tutanunua wapi mikate ili watu hawa wale?”+  Hata hivyo, aliuliza swali hilo ili kumjaribu, kwa maana alijua jambo alilokuwa karibu kufanya.  Filipo akamjibu: “Mikate ya dinari* 200 haiwezi kutosha hata tukimpa kila mmoja wao kipande kidogo.”  Mmoja wa wanafunzi wake aitwaye Andrea, ndugu ya Simoni Petro, akamwambia:  “Hapa kuna mvulana mdogo aliye na mikate mitano ya shayiri na samaki wawili wadogo. Je, hivi vitawatosha watu wengi hivi?”+ 10  Yesu akasema: “Waambieni watu waketi.” Basi mahali hapo palikuwa na nyasi nyingi, nao watu wakaketi, karibu wanaume 5,000.+ 11  Yesu akaichukua ile mikate, akatoa shukrani, kisha akawagawia wale waliokuwa wameketi hapo; pia akafanya vivyo hivyo na wale samaki wadogo, watu wote wakala na kushiba. 12  Waliposhiba akawaambia wanafunzi wake: “Kusanyeni vipande vilivyobaki, ili chochote kisipotee.” 13  Basi wakakusanya vipande vilivyobaki wakajaza vikapu 12 baada ya watu kula kutokana na ile mikate mitano ya shayiri. 14  Watu walipoona muujiza aliofanya, wakaanza kusema: “Kwa kweli huyu ndiye Nabii aliyepaswa kuja ulimwenguni.”+ 15  Kisha Yesu akijua walitaka kuja kumkamata wamfanye awe mfalme, akaondoka+ tena akaenda mlimani akiwa peke yake.+ 16  Ilipofika jioni, wanafunzi wake wakashuka kwenda baharini,+ 17  wakapanda mashua ili wavuke bahari kwenda Kapernaumu. Sasa giza lilikuwa limeingia na bado Yesu hakuwa pamoja nao.+ 18  Pia, bahari ikaanza kuchafuka kwa sababu upepo mkali ulikuwa ukivuma.+ 19  Hata hivyo, walipokuwa wamepiga makasia umbali wa karibu kilomita tano au sita,* wakamwona Yesu akitembea juu ya bahari akiikaribia mashua, nao wakaogopa. 20  Lakini akawaambia: “Ni mimi; msiogope!”+ 21  Basi walitaka kumbeba Yesu kwenye mashua, na mara moja mashua ikafika kwenye nchi kavu mahali walipokuwa wakienda.+ 22  Siku iliyofuata umati wa watu waliokuwa wamebaki ng’ambo ya bahari hawakuona mashua nyingine hapo ila mashua moja tu ndogo, na kwamba Yesu hakuwa amepanda kwenye mashua pamoja na wanafunzi wake, bali wanafunzi walikuwa wameondoka peke yao. 23  Hata hivyo, mashua kutoka Tiberia zikafika karibu na mahali ambapo walikula mikate baada ya Bwana kutoa shukrani. 24  Basi umati ulipoona kwamba Yesu na wanafunzi wake hawapo, wakapanda mashua zao wakaenda Kapernaumu kumtafuta Yesu. 25  Walipompata ng’ambo ya bahari wakamuuliza: “Rabi,+ ulifika hapa wakati gani?” 26  Yesu akawajibu: “Kwa kweli ninawaambia, hamnitafuti kwa sababu mliona ishara, bali kwa sababu mlikula mikate mkashiba.+ 27  Msifanye kazi kwa ajili ya chakula kinachoharibika, bali kwa ajili ya chakula kinachodumu kufikia uzima wa milele,+ ambacho Mwana wa binadamu atawapa ninyi; kwa maana Baba, Mungu mwenyewe, amemtia muhuri wake wa kibali.”+ 28  Basi wakamuuliza: “Tufanye nini ili tutimize kazi za Mungu?” 29  Yesu akawajibu: “Hii ndiyo kazi ya Mungu, kwamba mmwamini* yule aliyemtuma.”+ 30  Basi wakamwambia: “Utafanya ishara gani,+ ili tuone na kukuamini? Unafanya kazi gani? 31  Mababu zetu walikula mana nyikani,+ kama ilivyoandikwa: ‘Aliwapa mkate kutoka mbinguni ili wale.’”+ 32  Kisha Yesu akawaambia: “Kwa kweli ninawaambia, Musa hakuwapa mkate kutoka mbinguni, lakini Baba yangu anawapa mkate wa kweli kutoka mbinguni. 33  Kwa maana mkate wa Mungu ni yule anayeshuka kutoka mbinguni na kuupa ulimwengu uzima.” 34  Kwa hiyo wakamwambia: “Bwana, tupe mkate huo sikuzote.” 35  Yesu akawaambia: “Mimi ndio mkate wa uzima. Yeyote anayekuja kwangu hatapata njaa kamwe, na yeyote anayeniamini hatapata kiu kamwe.+ 36  Lakini kama nilivyowaambia, mmeniona na bado hamwamini.+ 37  Wote anaonipa Baba watakuja kwangu, nami sitamfukuza kamwe yeyote anayekuja kwangu;+ 38  kwa maana sikushuka kutoka mbinguni+ kufanya mapenzi yangu, bali mapenzi ya yule aliyenituma.+ 39  Haya ndiyo mapenzi ya yule aliyenituma, kwamba nisipoteze yeyote kati ya wote alionipa, bali niwafufue+ katika siku ya mwisho. 40  Kwa maana haya ndiyo mapenzi ya Baba yangu, kwamba kila mtu anayemtambua Mwana na kumwamini awe na uzima wa milele,+ nami nitamfufua+ siku ya mwisho.” 41  Kisha Wayahudi wakaanza kunung’unika kwa sababu alisema: “Mimi ndio mkate ulioshuka kutoka mbinguni.”+ 42  Nao wakaanza kusema: “Je, huyu si Yesu mwana wa Yosefu, ambaye baba yake na mama yake tunawajua?+ Sasa anawezaje kusema, ‘Nimeshuka kutoka mbinguni’?” 43  Yesu akawaambia: “Acheni kunung’unika miongoni mwenu. 44  Hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba aliyenituma amvute,+ nami nitamfufua siku ya mwisho.+ 45  Imeandikwa katika Manabii: ‘Wote watafundishwa na Yehova.’*+ Kila mtu ambaye amemsikiliza Baba na kujifunza huja kwangu. 46  Hakuna mwanadamu yeyote ambaye amemwona Baba,+ ila yule aliyetoka kwa Mungu; huyo amemwona Baba.+ 47  Kwa kweli ninawaambia, yeyote anayeamini ana uzima wa milele.+ 48  “Mimi ndio mkate wa uzima.+ 49  Mababu zenu walikula mana nyikani na bado wakafa.+ 50  Huu ndio mkate unaoshuka kutoka mbinguni, ili yeyote anayeula asife. 51  Mimi ndio mkate ulio hai ambao ulishuka kutoka mbinguni. Yeyote akila mkate huu ataishi milele; na kwa kweli, mkate nitakaotoa ni mwili wangu kwa ajili ya uzima wa ulimwengu.”+ 52  Kisha Wayahudi wakaanza kubishana wakiulizana: “Mtu huyu anawezaje kutupatia mwili wake tule?” 53  Basi Yesu akawaambia: “Kwa kweli ninawaambia, msipokula mwili wa Mwana wa binadamu na kunywa damu yake, hamna uzima ndani yenu.+ 54  Yeyote akila mwili wangu na kunywa damu yangu ana uzima wa milele, nami nitamfufua+ siku ya mwisho; 55  kwa maana mwili wangu ni chakula cha kweli na damu yangu ni kinywaji cha kweli. 56  Yeyote anayekula mwili wangu na kunywa damu yangu hubaki katika muungano nami, nami katika muungano naye.+ 57  Kama vile Baba aliye hai alivyonituma nami ninaishi kwa sababu ya Baba, vivyo hivyo yule anayekula mwili wangu, ataishi kwa sababu yangu.+ 58  Huu ndio mkate ulioshuka kutoka mbinguni. Si kama vile walivyokula mababu zenu na bado wakafa. Yeyote anayekula mkate huu ataishi milele.”+ 59  Alisema mambo haya alipokuwa akifundisha katika sinagogi* huko Kapernaumu. 60  Waliposikia hivyo, wengi kati ya wanafunzi wake wakasema: “Maneno hayo yanashtua; ni nani anayeweza kuyasikiliza?” 61  Lakini Yesu, akitambua kwamba wanafunzi wake walikuwa wakinung’unika kuhusu hilo, akawaambia: “Je, jambo hili limewakwaza? 62  Basi, itakuwaje mtakapomwona Mwana wa binadamu akipanda kurudi kule alikotoka?+ 63  Roho ndiyo inayotokeza uzima;+ mwili hauna faida hata kidogo. Maneno niliyowaambia ni roho na ni uzima.+ 64  Lakini kuna wengine kati yenu ambao hawaamini.” Kwa maana tangu mwanzo Yesu aliwajua wale ambao hawakuamini na yule ambaye angemsaliti.+ 65  Akaendelea kusema: “Ndiyo sababu nimewaambia, hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa aruhusiwe na Baba.”+ 66  Kwa sababu hiyo, wengi kati ya wanafunzi wake wakarudi kwenye mambo yaliyo nyuma+ nao hawakumfuata tena. 67  Basi Yesu akawauliza wale 12: “Je, ninyi pia mnataka kwenda?” 68  Simoni Petro akamjibu: “Bwana, tutaenda kwa nani?+ Wewe una maneno ya uzima wa milele.+ 69  Tumeamini na tumejua kwamba wewe ndiye Mtakatifu wa Mungu.”+ 70  Yesu akawaambia: “Niliwachagua ninyi 12, sivyo?+ Lakini mmoja wenu ni mchongezi.”*+ 71  Kwa kweli, alikuwa akizungumza kumhusu Yuda mwana wa Simoni Iskariote, ambaye angemsaliti, ingawa alikuwa mmoja wa wale 12.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “karibu stadia 25 au 30.” Angalia Nyongeza B14.
Au “mwonyeshe imani katika.”
Au “kusanyiko la watu wote.”
Au “ibilisi.”