Mhubiri 7:1-29

  • Jina zuri na siku ya kufa (1-4)

  • Kemeo la mtu mwenye hekima (5-7)

  • Mwisho ni bora kuliko mwanzo (8-10)

  • Faida ya hekima (11, 12)

  • Siku njema na siku mbaya (13-15)

  • Usipite kiasi (16-22)

  • Aliyoyaona mkutanishaji (23-29)

7  Jina zuri* ni bora kuliko mafuta mazuri,+ na siku ya kufa ni bora kuliko siku ya kuzaliwa.  Ni afadhali kwenda katika nyumba yenye maombolezo kuliko kwenda katika nyumba yenye karamu,+ kwa sababu huo ndio mwisho wa kila mwanadamu, na walio hai wanapaswa kuweka moyoni jambo hilo.  Ni afadhali huzuni kuliko kicheko,+ kwa maana uso wenye huzuni huboresha moyo.+  Moyo wa mwenye hekima uko katika nyumba yenye maombolezo, lakini moyo wa mpumbavu uko katika nyumba yenye nderemo.*+  Ni afadhali kusikiliza karipio la mtu mwenye hekima+ kuliko kusikiliza wimbo wa wajinga.  Kwa maana kicheko cha mjinga ni kama mlio wa miiba inayoteketea chini ya chungu;+ na hili pia ni ubatili.  Lakini ukandamizaji unaweza kumfanya mtu mwenye hekima ashikwe na wazimu, na rushwa huupotosha moyo.+  Ni afadhali mwisho wa jambo kuliko mwanzo wake. Ni bora kuwa na subira kuliko kuwa na roho ya kiburi.+  Usikasirike haraka,*+ kwa maana hasira hukaa katika kifua cha wajinga.*+ 10  Usiulize: “Mbona siku za zamani zilikuwa bora kuliko hizi?” kwa maana hukuuliza hivyo kwa hekima.+ 11  Hekima pamoja na urithi ni jambo jema na huwanufaisha wale wanaoona mwanga wa mchana.* 12  Kwa maana hekima ni ulinzi+ kama pesa zilivyo ulinzi,+ lakini hii ndiyo faida ya ujuzi: Hekima humhifadhi hai yule aliye nayo.+ 13  Tafakari kazi ya Mungu wa kweli, kwa maana ni nani anayeweza kunyoosha kitu ambacho amekipinda?+ 14  Siku iliyo njema, tafakari wema huu,+ lakini katika siku ya taabu,* zingatia kwamba Mungu ameifanya hii na hiyo nyingine,+ ili wanadamu wasiweze kuwa na uhakika kuhusu* jambo lolote litakalowapata wakati ujao.+ 15  Katika maisha yangu ya ubatili+ nimeona kila jambo—nimemwona mwadilifu akiangamia katika uadilifu wake+ na mwovu akiishi maisha marefu licha ya uovu wake.+ 16  Usiwe mwadilifu kupita kiasi,+ wala kujifanya mwenye hekima kupita kiasi.+ Kwa nini ujiangamize?+ 17  Usiwe mwovu kupita kiasi, wala kuwa mjinga.+ Kwa nini ufe kabla ya wakati wako?+ 18  Ni bora kushika kabisa onyo moja bila kuachilia lingine;+ kwa maana anayemwogopa Mungu atatii yote mawili. 19  Hekima humfanya mtu mwenye hekima awe na nguvu zaidi kuliko wanaume kumi wenye nguvu walio jijini.+ 20  Kwa maana hakuna mtu mwadilifu duniani anayefanya mema sikuzote na hatendi dhambi kamwe.+ 21  Pia, usitie moyoni kila neno linalosemwa na watu;+ la sivyo, huenda ukamsikia mtumishi wako akisema mambo maovu kukuhusu;* 22  kwa maana unajua vema moyoni mwako kwamba wewe mwenyewe umesema mambo maovu kuwahusu wengine.+ 23  Niliyapima mambo hayo yote kwa hekima, nikasema: “Nitakuwa na hekima.” Lakini ilikuwa mbali nami. 24  Lile ambalo limekuja kuwapo halifikiki nalo ni lenye kina kirefu sana. Ni nani anayeweza kulielewa?+ 25  Niliuongoza moyo wangu kujua na kuchunguza na kutafuta hekima na maana ya mambo, na kuelewa uovu wa upumbavu na ujinga wa kuwa wazimu.+ 26  Kisha nikagundua hili: Mwanamke ambaye ni kama wavu wa mwindaji anatia uchungu kuliko kifo, ambaye moyo wake ni kama nyavu za kukokotwa, na ambaye mikono yake ni kama minyororo ya gereza. Mtu anayempendeza Mungu wa kweli atamkwepa mwanamke huyo,+ lakini mtenda dhambi hunaswa naye.+ 27  “Tazama, hili ndilo nililogundua,” asema mkutanishaji.+ “Nilichunguza jambo moja baada ya lingine ili nifikie mkataa wangu, 28  lakini jambo nililoendelea* kutafuta, sijalipata. Nimempata mwanamume mmoja* kati ya elfu moja, lakini sijampata mwanamke miongoni mwao. 29  Hili ndilo jambo pekee nililopata: Mungu wa kweli aliwaumba wanadamu wakiwa wanyoofu,+ lakini wao wenyewe wamejitafutia mipango mingi.”+

Maelezo ya Chini

Au “Sifa nzuri.” Tnn., “Kuwa na jina.”
Au “burudani.”
Au labda, “ni dalili ya mjinga.”
Tnn., “Usiwe mwepesi kukasirika rohoni mwako.”
Yaani, walio hai.
Au “kugundua.”
Au “majanga.”
Tnn., “akikulaani.”
Au “ambalo nafsi yangu iliendelea.”
Au “mwanamume mmoja mnyoofu.”