Kwa Waroma 1:1-32

  • Salamu (1-7)

  • Paulo atamani kutembelea Roma (8-15)

  • Mwadilifu ataishi kupitia imani (16, 17)

  • Watu wasiomwogopa Mungu hawana sababu ya kujitetea (18-32)

    • Sifa za Mungu zinaonekana kupitia uumbaji (20)

1  Paulo, mtumwa wa Kristo Yesu aliyeitwa awe mtume na kuwekwa kando kwa ajili ya habari njema ya Mungu,+  ambayo aliahidi mapema kupitia manabii wake katika Maandiko matakatifu,  kuhusu Mwana wake, aliyetokana na uzao wa* Daudi+ kulingana na mwili,  lakini ambaye kwa nguvu alitangazwa kuwa Mwana wa Mungu+ kulingana na roho ya utakatifu kupitia ufufuo kutoka kwa wafu+—ndiyo, Yesu Kristo Bwana wetu.  Kupitia yeye tulipokea fadhili zisizostahiliwa na utume+ ili watu wa mataifa yote+ wamtii na kuwa na imani na kulitukuza jina lake,  ninyi pia mmeitwa kutoka kwa mataifa hayo ili muwe wa Yesu Kristo—  kwa ninyi nyote mlio huko Roma mkiwa wapendwa wa Mungu, walioitwa wawe watakatifu: Na muwe na fadhili zisizostahiliwa na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na Bwana Yesu Kristo.  Kwanza kabisa, ninamshukuru Mungu wangu kupitia Yesu Kristo kuwahusu ninyi nyote, kwa sababu imani yenu inazungumzwa ulimwenguni kote.  Kwa maana Mungu, ambaye ninamtolea utumishi mtakatifu kwa roho yangu kuhusiana na ile habari njema kuhusu Mwana wake, ni shahidi wangu wa jinsi ninavyowataja sikuzote katika sala zangu bila kuacha,+ 10  nikiomba kwamba ikiwezekana, hatimaye nifanikiwe kuja kwenu kwa mapenzi ya Mungu. 11  Kwa maana ninatamani kuwaona ninyi ili niwape zawadi ya kiroho kusudi mfanywe imara; 12  au badala yake, tutiane moyo,*+ kila mmoja kupitia imani ya mwenzake, yenu na yangu pia. 13  Lakini, akina ndugu, sitaki mkose kujua kwamba mara nyingi nilikusudia kuja kwenu ili nipate matunda kati yenu pia kama ilivyo katika mataifa mengine, lakini nimezuiwa mpaka sasa. 14  Mimi nina deni kwa Wagiriki na kwa watu wa mataifa ya kigeni,* kwa wenye hekima na wasio na akili pia: 15  kwa hiyo ninatamani kuwatangazia habari njema pia ninyi mlio huko Roma.+ 16  Kwa maana siionei aibu habari njema;+ kwa kweli, hiyo ni nguvu za Mungu kwa ajili ya wokovu kwa kila mtu aliye na imani,+ kwanza kwa Myahudi+ na pia kwa Mgiriki.+ 17  Kwa sababu kupitia habari njema, uadilifu wa Mungu unafunuliwa kupitia imani na kwa ajili ya imani,+ kama ilivyoandikwa: “Lakini mwadilifu ataishi kupitia imani.”+ 18  Kwa kuwa ghadhabu ya Mungu+ inafunuliwa kutoka mbinguni dhidi ya watu wote wasiomwogopa Mungu na wasio waadilifu ambao wanaikandamiza kweli+ kwa njia isiyo ya uadilifu, 19  kwa sababu mambo yanayoweza kujulikana kuhusu Mungu yako wazi kabisa kati yao, kwa maana Mungu aliyaweka wazi kwao.+ 20  Kwa maana sifa zake zisizoonekana, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kupitia vitu vilivyoumbwa,+ yaani, nguvu zake za milele+ na Uungu,+ hivi kwamba hawana sababu ya kujitetea. 21  Kwa maana ingawa walimjua Mungu, hawakumtukuza yeye akiwa Mungu wala hawakumshukuru, bali walikuwa wajinga katika fikira zao na mioyo yao isiyo na ufahamu ikawa na giza.+ 22  Ingawa walidai wana hekima, wakawa wapumbavu 23  na kuugeuza utukufu wa Mungu asiyeweza kuharibika kuwa kitu kama sanamu ya mwanadamu anayeweza kuharibika* na ya ndege na viumbe wenye miguu minne na viumbe wanaotambaa.+ 24  Kwa hiyo, kwa kupatana na tamaa za mioyo yao, Mungu aliwaacha katika uchafu, ili miili yao ivunjiwe heshima kati yao. 25  Waliibadili kweli ya Mungu kwa ajili ya uwongo, nao wakaabudu* uumbaji na kuutolea utumishi mtakatifu badala ya kumtolea Muumba, anayesifiwa milele. Amina. 26  Ndiyo sababu Mungu aliwaacha katika hamu isiyodhibitiwa ya ngono,+ kwa maana wanawake wao walibadili matumizi yao ya asili kuwa kinyume cha asili;+ 27  vivyo hivyo pia wanaume waliacha matumizi ya asili ya* mwanamke na kuwakiana tamaa kali za uchu wao kwa wao, wanaume kwa wanaume,+ wakitenda mambo machafu na kupokea ndani yao wenyewe adhabu* kamili, kwa sababu ya kosa lao.+ 28  Kwa sababu waliona haifai kumkubali Mungu,* Mungu aliwaacha katika hali ya akili isiyokubalika, ili wafanye mambo yasiyofaa.+ 29  Nao wakajaa kila namna ya ukosefu wa uadilifu,+ uovu, pupa,*+ na ubaya, wakiwa wamejaa wivu,+ uuaji,+ mizozo, udanganyifu,+ na nia ya kuwaumiza wengine,+ wakiwa wanong’onezaji,* 30  wasengenyaji,+ wenye kumchukia Mungu, wenye dharau, wenye majivuno, wenye kujidai, wenye kutunga mambo mabaya,* wasiotii wazazi,+ 31  wasio na uelewaji,+ wanaovunja makubaliano, wasio na upendo wa asili, na wasio na rehema. 32  Ingawa wanajua vizuri amri ya uadilifu ya Mungu—kwamba wale wanaozoea kufanya mambo kama hayo wanastahili kifo+—wanaendelea kuyafanya na pia wanakubaliana na wale wanaozoea kuyafanya.

Maelezo ya Chini

Tnn., “mbegu ya.”
Au “kuwe na ubadilishanaji wa kitia moyo.”
Au “wasio Wagiriki.” Tnn., “wabaribari.”
Au “kufa.”
Au “wakauheshimu sana.”
Au “mahusiano ya asili pamoja na.”
Au “malipo.”
Au “hawakukubali kumjua Mungu katika ujuzi sahihi.”
Au “wadaku; wambeya.”
Au “tamaa mbaya.”
Au “yenye kudhuru.”