Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SWALI LA 1

Mimi Ni Nani?

Mimi Ni Nani?

KWA NINI NI MUHIMU

Kujua wewe ni nani na una viwango gani kutakusaidia kufanya maamuzi yenye hekima unaposhinikizwa.

WEWE UNGEFANYA NINI?

Fikiria hali hii: Karen yuko kwenye karamu na hata kabla ya dakika kumi kwisha anasikia sauti ya mtu anayemfahamu nyuma yake.

“Wewe mshamba, mbona umezubaa?”

Karen anageuka na kumwona rafiki yake Jessica akiwa ameshika chupa mbili za bia zilizofunguliwa. “Usiniambie wewe ni mtoto sana hivi kwamba huwezi kujifurahisha kidogo!” Jessica anamwambia Karen huku akimsogezea chupa moja.

Karen anataka kukataa. Lakini Jessica ni rafiki yake. Na Karen hataki kuonekana mshamba. Isitoshe, Jessica ni msichana mzuri. Na ikiwa yeye anakunywa, basi hakuna ubaya kunywa. ‘Ni bia tu,’ Karen anajiliwaza. ‘Si dawa za kulevya.’

Ikiwa ungekuwa Karen, ungefanya nini?

TUA NA UFIKIRI!

Ili ufanye uamuzi wa hekima katika hali kama hiyo, unahitaji kuwa na viwango. Viwango hivyo vinakutambulisha wewe ni nani. Ukiwa na viwango, utakuwa na uwezo wa kuongoza maisha yako badala ya kuwaruhusu wengine wakuongoze.—1 Wakorintho 9:26, 27.

Unaweza kufanya nini ili usitawishe uwezo huo? Anza kwa kujibu maswali yafuatayo.

1 NINA SIFA GANI NZURI?

Kujua uwezo wako na sifa zako nzuri kutakusaidia ujiamini zaidi.

MFANO WA BIBLIA: Mtume Paulo aliandika hivi: “Hata kama sina ustadi wa kusema, hakika sivyo nilivyo katika ujuzi.” (2 Wakorintho 11:6) Kwa kuwa Paulo aliyafahamu Maandiko vizuri, alisimama imara alipopingwa na wengine. Hakuruhusu maneno ya wengine yadhoofishe imani yake.—2 Wakorintho 10:10; 11:5.

JICHUNGUZE: Andika kipaji au ustadi fulani ulio nao.

Sasa andika sifa nzuri uliyo nayo. (Kwa mfano, wewe unawajali wengine? ni mkarimu? unategemeka? unafanya mambo kwa wakati?)

2 NINA UDHAIFU GANI?

Ni wazi kwamba usipoziba ufa, utajenga ukuta, vivyo hivyo viwango vyako vinaweza kudhoofika sana ukiruhusu udhaifu wako uongoze maamuzi unayofanya maishani.

MFANO WA BIBLIA: Mtume Paulo alitambua udhaifu wake. Aliandika hivi: “Kwa kweli naipenda sheria ya Mungu kulingana na mtu niliye kwa ndani, lakini mimi naona ndani ya viungo vyangu sheria nyingine ikipigana na sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi.”—Waroma 7:22, 23.

JICHUNGUZE: Ni udhaifu gani unaohitaji kujifunza kudhibiti?

3 NINA MIRADI GANI?

Je, unaweza kuingia ndani ya teksi na kumwomba dereva aendeshe gari hilo kuzunguka jengo moja hadi petroli iishe? Huo ungekuwa ujinga unaogharimu sana!

Unajifunza nini? Miradi au malengo yatakusaidia uwe na mwelekeo maishani. Unakuwa na mahali pa kwenda na unapanga jinsi utakavyofika huko.

MFANO WA BIBLIA: Paulo aliandika hivi: “Jinsi ninavyokimbia si bila uhakika.” (1 Wakorintho 9:26) Badala ya kuishi bila mwelekeo, Paulo alijiwekea miradi na akajaribu sana kuifikia.—Wafilipi 3:12-14.

JICHUNGUZE: Andika miradi mitatu ambayo ungependa kutimiza kufikia mwaka ujao.

4 NINAAMINI NINI?

Unapokuwa na viwango thabiti, unakuwa kama mti ulio na mizizi imara inayouwezesha kustahimili dhoruba kali

Bila kuwa na imani thabiti, hutakuwa na msimamo. Kama tu kinyonga, utabadili msimamo wako kila mara ili ukubaliwe na vijana wenzako—ishara ya wazi kwamba huna viwango.

Tofauti na hilo, ikiwa matendo yako yanategemea imani yako thabiti, huwezi kuyumbishwa—haidhuru wengine wanafanya nini.

MFANO WA BIBLIA: Huenda alipokuwa bado kijana, nabii Danieli “aliazimia moyoni mwake” kwamba angetii sheria za Mungu, ingawa alikuwa ametenganishwa na familia yake. (Danieli 1:8) Kwa kufanya hivyo, alishikamana na viwango vyake. Danieli aliishi kulingana na imani yake.

JICHUNGUZE: Unaamini nini? Kwa mfano: Unaamini kwamba kuna Mungu? Ikiwa ndivyo, kwa nini unaamini hivyo? Ni uthibitisho gani unaokusadikisha kwamba yeye yuko?

Unaamini kwamba viwango vya maadili ambavyo Mungu ameweka ni kwa faida yako? Kwa nini unaamini hivyo?

Baada ya kufikiria yote hayo, ungependa kufananishwa na nini—jani lililoanguka na linalopeperushwa na upepo huku na huku au na mti unaohimili hata dhoruba kali? Ukiwa na viwango thabiti, utakuwa kama mti huo, na utaweza kujibu swali hili muhimu, Mimi ni nani?