Hamia kwenye habari

Je, Ninaweza Kupata Faraja Katika Biblia?

Je, Ninaweza Kupata Faraja Katika Biblia?

Jibu la Biblia

 Ndiyo. (Waroma 15:4) Chunguza mistari ya Biblia ambayo imewafariji watu wengi wanaokabiliana na hali ngumu na kushuka moyo.

Katika makala hii

 Matatizo

 Zaburi 23:4: “Hata nikitembea katika bonde lenye kivuli kizito, siogopi madhara yoyote, kwa maana wewe uko pamoja nami.”

 Maana: Unaposali kwa Mungu na kutegemea mwongozo wa Neno lake, Biblia, unaweza kukabiliana na matatizo kwa ujasiri.

 Wafilipi 4:13: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yule anayenipa nguvu.”

 Maana: Mungu anaweza kukupa nguvu za kukabiliana na tatizo lolote.

 Kifo cha mpendwa

 Mhubiri 9:10: “Hakuna kazi wala mipango wala ujuzi wala hekima Kaburini.”

 Maana: Wale ambao wamekufa hawateseki na hawawezi kutudhuru. Hawajui lolote.

 Matendo 24:15: “Kutakuwa na ufufuo.”

 Maana: Mungu anaweza kuwafufua wapendwa wetu.

 Kuhisi hatia kupita kiasi

 Zaburi 86:5: “Kwa maana wewe, Ee Yehova, a ni mwema na uko tayari kusamehe; una upendo mwingi mshikamanifu kwa wote wanaokuitia.”

 Maana: Mungu huwasamehe wale ambao wanajutia makosa yao ya zamani na kuazimia kutoyarudia.

 Zaburi 103:12: “Kama mashariki ilivyo mbali sana na magharibi, ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali sana na sisi.”

 Maana: Mungu anaposamehe anaweka makosa yetu mbali sana na sisi. Hatukumbushi makosa hayo tena na tena ili kutulaumu au kutuadhibu.

 Huzuni

 Zaburi 31:7: “Umeona dhiki yangu; unajua mateso makali yaliyo ndani yangu.”

 Maana: Mungu anajua vizuri mateso yote unayokabili. Anaelewa hisia zako za ndani kabisa​—hata wengine wanaposhindwa kukuelewa.

 Zaburi 34:18: “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; huwaokoa waliopondeka roho.”

 Maana: Mungu anaahidi kukutegemeza unapokuwa na huzuni. Anaweza kukupa nguvu za kukabiliana na huzuni.

 Ugonjwa

 Zaburi 41:3: “Yehova atamtegemeza kwenye kitanda chake cha ugonjwa.”

 Maana: Mungu anaweza kukusaidia kukabiliana na ugonjwa kwa kukupatia amani ya akili, nguvu, uvumilivu, na hekima ya kufanya maamuzi yenye busara.

 Isaya 33:24: “Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”

 Maana: Mungu anaahidi kwamba wakati utafika ambapo wanadamu wote watakuwa na afya njema.

 Mkazo na mahangaiko

 Zaburi 94:19: “Mahangaiko yaliponilemea, ulinifariji na kunibembeleza.”

 Maana: Tukimtegemea Mungu wakati ambapo tuna mkazo, atatusaidia tuwe watulivu.

 1 Petro 5:7: “[Tupeni] mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye anawajali ninyi.”

 Maana: Mungu anatujali tunapoteseka. Anatualika tumwambie matatizo yetu kupitia sala.

 Vita

 Zaburi 46:9: “Anakomesha vita katika dunia yote.”

 Maana: Hivi karibuni Ufalme wa Mungu utakomesha vita duniani kote.

 Zaburi 37:11, 29: “Wapole wataimiliki dunia, nao watafurahia kwelikweli wingi wa amani. . . . Waadilifu wataimiliki dunia, nao wataishi humo milele.”

 Maana: Watu wema watafurahia amani duniani milele.

 Wasiwasi kuhusu wakati ujao

 Yeremia 29:11: “‘Ninajua vizuri mawazo ninayofikiria kuwaelekea ninyi,’ asema Yehova, ‘mawazo ya amani, wala si ya msiba, ili niwape ninyi wakati ujao na tumaini.’”

 Maana: Mungu anawahakikishia watu wake kwamba hivi karibuni watafurahia maisha mazuri sana.

 Ufunuo 21:4: “Atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”

 Maana: Mungu anaahidi kukomesha mambo yote mabaya unayoona yakitukia leo.

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala “Yehova Ni Nani?