Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | VIJANA

Jinsi ya Kudhibiti Hasira

Jinsi ya Kudhibiti Hasira

KIKWAZO

“Nilimfokea dada yangu na kuusukuma mlango kwa nguvu hivi kwamba chuma kilichokuwa nyuma ya mlango kikatoboa ukuta. Shimo hilo lilinikumbusha jinsi nilivyokuwa nimetenda kwa njia ya kitoto.”—Diane. *

“Niliinua sauti na kuropoka, ‘Sijui wewe ni baba wa aina gani!’ na kisha nikausukuma mlango kwa nguvu. Lakini kabla haujafungika, nilimtazama baba yangu usoni na kuona kwamba alikuwa amekasirika. Nilijuta sana kwa sababu ya kuropoka maneno hayo.”—Lauren.

Je, umewahi kufanya kama Diane na Lauren? Ikiwa ndivyo, makala hii itakusaidia.

MAMBO UNAYOPASWA KUJUA

Milipuko ya hasira inakuharibia sifa. “Mwanzoni nilifikiri kwamba watu wanapaswa kuelewa kwamba nina hasira,” anasema Briana, msichana mwenye umri wa miaka 21. “Lakini niligundua kwamba ni jambo lisilofaa kufoka ovyoovyo, na kwamba wengine waliniona kuwa mpumbavu!”

Biblia inasema hivi: “Yule anayekasirika upesi atatenda upumbavu.”—Methali 14:17.

Watu humwepuka mtu mwenye milipuko ya hasira kama wanavyokimbia volkano inayolipuka

Hasira inaweza kufanya watu wakuepuke. Kijana mwenye umri wa miaka 18 anayeitwa Daniel anasema hivi: “Unapokasirika unapoteza hadhi yako na heshima ambayo wengine wanayo kukuelekea.” Pia, Elaine msichana mwenye miaka 18 anakubaliana na jambo hilo. Anasema, “Watu hawapendi kushirikiana na watu wenye hasira. Badala yake wanawaepuka.”

Biblia inasema: “Usishirikiane na mtu yeyote mwenye mazoea ya kukasirika; wala usiende pamoja na mtu wa mifoko ya ghadhabu.”—Methali 22:24.

Unaweza kurekebisha hali. Sara, msichana mwenye miaka 15 anasema hivi: “Si rahisi nyakati zote kudhibiti hisia zako, lakini unaweza kudhibiti maneno na matendo yako. Hakuna haja ya kulipuka kwa hasira.”

Biblia inasema hivi: “Asiye mwepesi wa hasira ni bora kuliko mwanamume mwenye nguvu, naye anayezuia roho yake ni bora kuliko mtu anayeteka jiji.”—Methali 16:32.

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Uwe na lengo. Badala ya kusema, “Hivyo ndivyo nilivyo,” jitahidi kuboresha hali yako kwa kipindi fulani hususa—labda kipindi cha miezi sita. Katika kipindi hicho, andika maendeleo unayofanya. Kila mara unapokasirika, andika (1) jambo lililofanyika, (2) jinsi ulivyotenda, na (3) jinsi ambavyo ungetenda kwa njia bora zaidi na kwa nini ungetenda hivyo. Kisha azimia kutenda kwa njia hiyo bora zaidi wakati mwingine unapokasirishwa. Dokezo: Usisahau pia kuandika mambo mazuri unayotimiza! Vilevile andika jinsi unavyohisi baada ya kuonyesha sifa ya kujizuia.—Kanuni ya Biblia: Wakolosai 3:8.

Uwe na subira. Unapokasirishwa, usikimbilie kusema mara moja ulichokuwa ukitaka kusema. Badala yake, subiri. Shusha pumzi. Erik, mvulana mwenye miaka 15 anasema hivi: “Ninaposhusha pumzi ninapata wakati wa kufikiri kabla ya kusema au kufanya jambo nitakalojutia baadaye.”—Kanuni ya Biblia: Methali 21:23.

Panua maoni yako. Nyakati nyingine huenda umekasirika kwa sababu ya kufikiria upande mmoja tu wa jambo lililokupata, yaani, sehemu iliyokukasirisha wewe. Jitahidi pia kuelewa jinsi wengine wanavyohisi. Mwanamke mwenye miaka 24 anayeitwa Jessica anasema hivi: “Hata ikiwa watu ni wakaidi, kwa kawaida mimi hujitahidi kuelewa sababu inayowafanya watende hivyo.”—Kanuni ya Biblia: Methali 19:11.

Ondoka, ikihitajika. Biblia inasema hivi: “Kabla mabishano hayajalipuka, jiondokee.” (Methali 17:14) Kama andiko hili linavyoonyesha, nyakati nyingine jambo bora la kufanya hali inapokuwa mbaya ni kuondoka. Kisha, badala ya kuendelea kukazia fikira jambo hilo na hivyo kuzidi kukasirika, fanya jambo lingine. Mwanamke anayeitwa Danielle anasema hivi: “Nimeona kwamba kufanya mazoezi hunisaidia kupunguza mkazo na hilo limenisaidia nisilipuke kwa hasira.”

Jifunze kusamehe. Biblia inasema: “Fadhaikeni, lakini msitende dhambi. Semeni moyoni mwenu, . . . na kunyamaza.” (Zaburi 4:4) Kwa kweli si vibaya kukasirika. Lakini, utachukua hatua gani baada ya kukasirishwa? Kijana anayeitwa Richard anasema hivi: “Ukiruhusu matendo ya wengine yakukasirishe, hiyo itamaanisha kwamba wao ndio wanaokuamulia jinsi utakavyohisi. Kwa nini usijitahidi kuonyesha kwamba wewe ni mkomavu kwa kumsamehe aliyekukosea? ” Ukifanya hivyo, utakuwa umefaulu kudhibiti hasira yako badala ya kuiruhusu hasira ikudhibiti.

^ fu. 4 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.