Hamia kwenye habari

Mashahidi wa Yehova Wanaamini Nini?

Mashahidi wa Yehova Wanaamini Nini?

Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tunajitahidi kufuata aina ya Ukristo ambao Yesu alifundisha na mambo ambayo wanafunzi wake walifanya. Makala hii inaelezea kwa ufupi mambo ya msingi tunayoamini.

  1.   Mungu. Tunamwabudu Mungu Mweza-Yote wa pekee na wa kweli, Muumba, ambaye jina lake ni Yehova. (Zaburi 83:18; Ufunuo 4:​11) Yeye ni Mungu wa Abrahamu, Musa, na Yesu.​—Kutoka 3:6; 32:11; Yohana 20:17.

  2.   Biblia. Tunatambua kwamba Biblia ni ujumbe ulioongozwa na roho ya Mungu kwa ajili ya wanadamu. (Yohana 17:17; 2 Timotheo 3:​16) Imani yetu inategemea vitabu vyote 66 vya Biblia, vinavyotia ndani “Agano la kale” na “Agano jipya.” Profesa Jason D. BeDuhn kwa kufaa alielezea jambo hilo alipoandika kwamba Mashahidi wa Yehova wametegemeza “imani yao na matendo yao [juu ya kile ambacho] Biblia inasema bila kujali matokeo ya jambo hilo.” *

     Ingawa tunaiamini Biblia nzima, hatuna imani kali za kidini. Tunatambua kwamba baadhi ya mambo katika Biblia yameandikwa kwa njia ya mfano na hayamaanishi vitu halisi.​—Ufunuo 1:1.

  3.   Yesu. Tunafuata mafundisho ya Yesu Kristo na mfano aliotuwekea na tunamheshimu kwa kuwa yeye ni Mwokozi wetu na Mwana wa Mungu. (Mathayo 20:28; Matendo 5:​31) Hivyo, sisi ni Wakristo. (Matendo 11:26) Hata hivyo, tumejifunza katika maandiko kwamba Yesu si Mungu Mweza-Yote na hakuna msingi wa Kimaandiko unaothibitisha fundisho la Utatu.​—Yohana 14:28.

  4.   Ufalme wa Mungu. Ni serikali halisi iliyo mbinguni, na si hali iliyo katika mioyo ya Wakristo. Ufalme huo utaharibu serikali zote za wanadamu na kutimiza kusudi la Mungu kwa dunia. (Danieli 2:​44; Mathayo 6:​9, 10) Utatimiza mambo hayo hivi karibuni, kwa sababu unabii wa Biblia unaonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho.”​—2 Timotheo 3:​1-5; Mathayo 24:​3-​14.

     Yesu ni Mfalme wa Ufalme wa Mungu mbinguni. Alianza kutawala mwaka wa 1914.​—Ufunuo 11:15.

  5.   Wokovu. Tunapata msamaha wa dhambi na kifo kupitia dhabihu ya fidia ya Yesu. (Mathayo 20:28; Matendo 4:​12) Ili kufaidika kutokana na fidia hiyo, haitoshi tu kumwamini Yesu badala yake watu wanapaswa kubadili mwenendo wao wa maisha na kubatizwa. (Mathayo 28:19, 20; Yohana 3:​16; Matendo 3:​19, 20) Imani ya mtu huonyeshwa kwa matendo yake. (Yakobo 2:​24, 26) Hata hivyo, wokovu hautokani na jitihada zetu​—unatokana tu na “fadhili zisizostahiliwa za Mungu.”​—Wagalatia 2:​16, 21.

  6.   Mbinguni. Yehova Mungu, Yesu Kristo, na malaika waaminifu wanaishi mbinguni. * (Zaburi 103:19-​21; Matendo 7:​55) Idadi ndogo hususa ya watu​—144,000​—watafufuliwa na kwenda mbinguni kutawala pamoja na Yesu katika Ufalme.​—Danieli 7:​27; 2 Timotheo 2:​12; Ufunuo 5:​9, 10; 14:​1, 3.

  7.   Dunia. Mungu aliiumba dunia iwe makao ya milele ya wanadamu. (Zaburi 104:5; 115:16; Mhubiri 1:4) Mungu atawabariki wanadamu waadilifu kwa kuwapa afya kamilifu na uhai wa milele katika dunia paradiso.​—Zaburi 37:11, 34.

  8.   Uovu na kuteseka. Ulianza wakati malaika mmoja wa Mungu alipoasi. (Yohana 8:​44) Baada ya kuasi, malaika huyo aliyeitwa “Shetani” na “Ibilisi,” aliwashawishi wanadamu wa kwanza kujiunga naye, jambo ambalo limesababisha matatizo makubwa kwa wazao wao. (Mwanzo 3:​1-6; Waroma 5:​12) Ili kusuluhisha suala alilozusha Shetani, Mungu ameruhusu uovu na kuteseka, lakini hataruhusu hali hiyo iendelee milele.

  9.   Kifo. Mtu anapokufa hayupo tena. (Zaburi 146:4; Mhubiri 9:​5, 10) Hateseki milele katika moto wa mateso.

     Mungu atafufua mabilioni ya watu waishi tena. (Matendo 24:15) Hata hivyo, wale watakaofufuliwa na kukataa kuishi kupatana na viwango vya Mungu wataangamizwa milele bila kuwa na tumaini la ufufuo.​—Ufunuo 20:14, 15.

  10.   Familia. Tunatii kanuni ya msingi ya Mungu kuhusu ndoa yaani, muungano kati ya mwanamume mmoja na mwanamke mmoja, na uasherati ndio msingi pekee wa talaka. (Mathayo 19:​4-9) Tunasadiki kwamba hekima ya Biblia husaidia familia kufanikiwa.​—Waefeso 5:22–​6:1.

  11.   Ibada yetu. Hatuabudu msalaba wala aina nyingine yoyote ya mifano. (Kumbukumbu la Torati 4:​15-​19; 1 Yohana 5:​21) Yafuatayo ni baadhi ya mambo muhimu katika ibada yetu:

  12.   Tengenezo letu. Tumepangwa katika makutaniko, na kila kutaniko linasimamiwa na baraza la wazee. Hata hivyo, wazee hao si kikundi cha viongozi walioinuliwa juu ya waamini wengine, na hawalipwi mshahara. (Mathayo 10:8; 23:8) Hatutoi fungu la kumi, na hatukusanyi sadaka zozote katika mikutano yetu. (2 Wakorintho 9:7) Shughuli zetu zote zinategemezwa na michango ya hiari.

     Baraza Linaloongoza, ni kikundi kidogo cha Wakristo wakomavu wanaotumikia kwenye makao makuu, na wanasimamia kazi ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote.​—Mathayo 24:45.

  13.   Umoja wetu. Imani yetu imetuunganisha duniani pote. (1 Wakorintho 1:​10) Tunajitahidi kuepuka tofauti za kijamii, kitamaduni, rangi, na matabaka. (Matendo 10:34, 35; Yakobo 2:4) Hata hivyo, hayo ni mambo ya mtu binafsi. Kila Shahidi hufanya maamuzi akitegemea dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia.​—Waroma 14:​1-4; Waebrania 5:​14.

  14.   Mwenendo wetu. Tunajitahidi kuonyesha upendo usio wa kinafiki katika mambo yote. (Yohana 13:34, 35) Tunaepuka mazoea yasiyompendeza Mungu, kama vile matumizi yasiyofaa ya damu yanayotia ndanikutia damu mishipani. (Matendo 15:28, 29; Wagalatia 5:​19-​21) Tunapenda amani na hatushiriki katika vita. (Mathayo 5:9; Isaya 2:4) Tunaheshimu serikali ya nchi tunamoishi na tunatii sheria zake maadamu hazidai tuvunje kanuni za Mungu.​—Mathayo 22:21; Matendo 5:​29.

  15.   Uhusiano wetu pamoja na wengine. Yesu aliamuru hivi: “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” Pia alisema Wakristo “si sehemu ya ulimwengu.” (Mathayo 22:39; Yohana 17:16) Hivyo tunajitahidi “kuwatendea wote mema” lakini hatujihusishi katika siasa wala hatushirikiani na dini nyingine. (Wagalatia 6:10; 2 Wakorintho 6:14) Hata hivyo, tunaheshimu maamuzi ambayo wengine wanafanya kuhusu mambo hayo.​—Waroma 14:12.

 Ikiwa unataka kujua mengi zaidi kuhusu Mashahidi wa Yehova, unaweza kusoma habari zaidi kutuhusu katika tovuti yetu, uwasiliane na moja ya ofisi zetu, uhudhurie mkutano katika Jumba la Ufalme lililo karibu nawe, au uzungumze na Shahidi katika eneo lako.

^ Ona kitabu Truth in Translation, ukurasa wa 165.

^ Malaika waovu walitupwa kutoka mbinguni, hata hivyo bado wapo katika ulimwengu wa roho.​—Ufunuo 12:​7-9.